Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Maftaha Abdallah Nachuma

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtwara Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kumshukuru Mwenyezi Mungu na Kiti chako, napenda kuchangia Wizara hii kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, korosho wakulima hawajalipwa; kutokana na taarifa za TAKUKURU mwaka 2015/ 2016 wakulima wa Mkoa wa Mtwara wa zao la korosho hawajalipwa bilioni thelathini na vyama vya msingi. Hali hii imekuwa inawavunja nguvu sana wakulima kwa kuwa Serikali ilijigamba kwa kiasi kikubwa kuwa Mfumo wa Stakabadhi Ghalani unamsaidia mkulima. Hata hivyo, pamoja na wizi wote huu kwa wakulima wanyonge, hakuna hatua yoyote iliyochukuliwa kwa wahusika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Malipo ya Korosho 2016 Mtwara Mkindani; Mtwara Mjini kuna AMCOS mbili, moja ya Naliendele na nyingine ya Mikindani. Wananchi wameniambia wamepeleka korosho zao kwenye vyama hivi vya msingi lakini cha ajabu;

(a) Baadhi yao mpaka sasa hawajalipwa.

(b) Kuna minada mine ambayo ilifanyika mfululizo lakini vyama hivi vimelipwa minada ya tatu na nne (ya mwisho na kuacha ya kwanza ambayo ilikuwa na bei kubwa).

(c) Korosho kuuza kwenye mnada Sh.4,000/= lakini wananchi wamelipwa Sh.3,100/= (elfu tatu na mia moja) tu au chini ya hapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba wakulima hawa walipwe pesa zao haraka iwezekanavyo na wahusika wote wachukuliwe hatua stahiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Pembejeo ya Salfa (sulfur). Naomba sana Serikali inunue pembejeo na kugawa bure kama ilivyoahidi. Kuna wakulima ambao wanahitaji salfa ya maji ambayo wanadai ni nzuri kuliko ya unga, hivyo, wasikilizwe wakulima hawa juu ya salfa hii ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Uvuvi Mtwara. Mtwara kuna Bahari ya Hindi yenye samaki wengi sana. Naomba Wizara ijenge viwanda vya samaki kama ilivyo Mwanza. Viwanda vya samaki vikijengwa itasaidia watu wetu kupata ajira na kuondokana na umaskini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Zana za Kisasa za Uvuvi; Wizara hii kazi zake ni pamoja na kuhakikisha inawasaidia Watanzania wavuvi waweze kuvua uvuvi wa kisasa. Naomba Wizara itenge pesa ya kutosha ili kununua zana za uvuvi, mfano boti za kisasa na mashine za boti hasa kwa wavuvi wa Mikindani, Misete na Kianga ambako wanavua uvuvi ambao hauna tija kwa sababu hawana vifaa vya kisasa. Serikali itenge pesa za kutosha kwa ajili hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Cooperate Social Responsibility. Wizara kwa mwaka 2016/2017 imekusanya pesa nyingi sana za mapato ya korosho, lakini jambo la ajabu hivi vyama vya msingi havina mchango wowote kwenye kusaidia jamii. Hakuna shule hata moja kupitia fedha nyingi zinazokusanywa katika korosho, Bodi ipo, vyama vya ushirika vipo wanakusanya pesa nyingi sana, kwa nini hawasaidii katika elimu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara itoe miongozo ili pesa za korosho Kusini zitumike kuinua kiwango cha elimu Kusini. Serikali inakusanya pesa nyingi kwenye korosho kuliko zao lolote lile nchini, vyama vya ushirika vya korosho viwe vinasaidia elimu kwa lazima Mtwara.