Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Juma Kombo Hamad

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Wingwi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nikushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia mawili, matatu katika Wizara hii muhimu, Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana wakati tuko katika Bunge la Bajeti, Mheshimiwa Waziri aliyekuwa na dhamana muda huo au mwaka jana aliwaambia Wabunge wa Bunge hili Tukufu na Watanzania kwa ujumla kwamba jembe la mkono litakuwa historia, lakini jembe la mkono litaonekana au litatumika katika maeneo matatu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo ambalo jembe la mkono litatumika kwa mujibu wa Mheshimiwa Waziri wa kipindi hicho alisema jembe la mkono litaonekana kwenye majumba ya kumbukumbu (makumbusho), alisema jembe la mkono litatumika kwa ajili ya kuchimbia makaburi lakini alisema jembe la mkono litaonekana kwenye Nembo ya Chama cha Mapinduzi na kwamba jembe la mkono halitatumika tena kwa shughuli za kilimo na alisema haya kwa sababu sasa Tanzania inaelekea kwenye uchumi wa kati na uchumi wa viwanda. Kwa hiyo, kama tunaelekea kwenye uchumi wa viwanda lazima tuboreshe kilimo na lazima tuwe na zana bora kwa ajili ya kuendeleza kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kufanya winding-up ya hotuba yake atueleze hadi sasa shughuli hii au azma/dhamira hii tumefika katika eneo gani. Tumevuka pale ambapo tulikuwa tunahitaji kuvuka au bado Watanzania wanaendelea kuhenyeka na kuumia kwa kutumia jembe la mkono. Nadhani ni wakati sasa wa kupata angalau maelezo ya Serikali kupitia Wizara hii kuwaeleza Watanzania tumefikia katika hatua gani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ambalo nataka kuchangia ni la uvuvi. Tanzania tumebarikiwa kuwa na eneo kubwa la bahari lakini Tanzania ni pamoja na Zanzibar. Zanzibar ni visiwa ambavyo vimezungukwa na eneo lote la bahari, bahari kubwa ni bahari ya Hindi. Kiuhalisia ni kwamba hatujaitumia bahari ipasavyo katika masuala ya uvuvi wa samaki lakini katika kutumia resource zilizomo ndani ya bahari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimtaarifu Waziri kama atakuwa hajui, lakini nina imani anajua kwa sababu naamini ni mlaji wa samaki. Hivi Waziri anajua kwamba hapa Dodoma tunakula vibua kutoka China?
Hivi Waziri anatambua kwamba tunakula vibua kutoka South Africa? Namwomba Mheshimiwa Waziri atambue hili, hivi sisi Watanzania tuna sababu gani kwa eneo kubwa la bahari ambalo limejaa resource ya samaki kwa nini hadi leo tunakula vibua vya South Africa. Mheshimiwa Waziri tunaomba na eneo hili atufafanulie kidogo tuone uhalisia na ukweli hasa wa matumizi ya bahari yetu ambayo tunayo katika Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zao la korosho. Wachangiaji wengi wamezungumza hapa kwamba zao la korosho linastawi zaidi na sana pembezoni mwa Ukanda wa Bahari au Ukanda wa Pwani. Natambua kwamba Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi si miongoni mwa Wizara za Muungano lakini kila siku hapa tunajivunia kwamba Wizara zilizoko katika Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Wizara ambazo zinafanya kazi kwa niaba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania zinafanya kazi kwa pamoja. Hebu tueleze hivi mmekaa lini kusaidiana na Wizara ambayo iko kwenye Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika masuala ya utafiti na kuangalia labda kwa kiasi gani zao la Korosho tunaweza kuliimarisha kwa upande wa Zanzibar na likawa ni sehemu na mbadala wa zao la karafuu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.