Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Saumu Heri Sakala

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. SAUMU H. SAKALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii mimi niweze uchangia katika Wizara hii ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi. Wizara ambayo binafsi naiona ni muhimu sana na imebeba kauli mbiu ya Rais ya Tanzania ya viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu kweli kabisa tusipoimarisha Wizara hii, Tanzania ya viwanda inakwenda ku-fail. Kilimo ndicho ambacho kimeibeba nchi yetu. Tangu enzi za Ukoloni tumekuwa tukisikia kwamba kilimo ni uti wa mgongo na mpaka sasa bado tunaendelea kuamini hivyo. Kilimo kimekumbwa na changamoto nyingi sana kiasi ambacho hata hiyo kauli ya kwamba kilimo ni uti wa mgongo ni kama vile inachezewa haileti maana sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze moja kwa moja kwa kusema kuwa kilimo kama ambavyo nimesema kimezungukwa na changamoto nyingi sana hasa ukizingatia wakulima walioko vijijini ambao ndiyo wanabeba kauli hii ya kwamba kilimo ni uti wa mgongo bado wanalima kwa asili, kwa mazoea, tangu enzi za mababu wamekuwa wakirithi. Shamba ni lile lile ambalo mimi nalijua bibi yangu alikuwa akilima na ndiyo hilo hilo sasa hivi mama yangu analima na ndiyo hilo hilo najua mimi nitalima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nalima sina mbolea, mbolea imezungukwa na urasimu mwingi tena mkubwa sana na hata nikiipata mbolea nyingi zinakuwa ni fake wakulima tunaathirika sana. Pia wakulima sisi tunalima kwa kutegemea mvua kitu ambacho sasa hivi kimepitwa na wakati. Mabadiliko ya tabianchi yameathiri kwa kiasi kikubwa Tanzania, mvua siyo za kutegemea tena tunatakiwa twende kwenye kilimo cha kisasa, lakini Serikali imekaa kimya hakuna elimu ya kutosha inayopelekwa vijijini kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji. Hakuna miundombinu inayopelekwa vijijini kwa ajili ya kilimo cha umwangiliaji tunategemea kilimo hili kitatubeba vipi? Kwa kweli Serikali kama kweli imedhamiria kumbeba Rais na kauli yake mbiu ya Tanzania ya viwanda ni lazima ihakikishe kilimo kinawekewa mazingira ambayo yatakuwa ni wezeshi kwa wakulima hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitolee mfano Wabunge wa Mkoa wa Tanga hapa wamesimama hapa wakasema tulikuwa na zao la nazi katika Mkoa Tanga katika Wilaya ya Pangani na Wilaya ya Muheza, sasa hivi zao lile limekufa lakini wote tunafahamu zao la nazi jinsi lilivyo na faida katika nchi yetu. Licha tu ya kuuza nchi jirani Kenya na sehemu nyingine lakini pia ilikuwa ndiyo kitu ambacho kilikuwa kinatusaidia sisi katika kupika, kupaka, urembo na vitu vingine. Pia nazi sisi tunajengea, ni mbao kule kwetu Pangani, lakini zao hili limekufa na hakuna mtu ambaye anajali. Haya yote ni mazingira ambayo yanasababisha kilimo kiweze kurudi nyuma. Kwa hiyo, mimi nawasihi sana muangalie hali halisi ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia hata viwanda navyo vya mazao yetu ambayo yanapatikana kwa kudra ya Mwenyenzi Mungu. Nasema hivyo kwa sababu tunalima kwa kutengemea mvua, siku mvua ikiwa nzuri maana yake ndiyo mazao yanapatikana sasa yakipatikana tunayapeleka wapi hata hilo soko nalo pia siku hizi hakuna. Hakuna soko la kuaminika, hakuna barabara za kuaminika ili mkulima aweze kutoa mazao yake pale na kuyafikisha sehemu inayohusika, naomba tuangalie sana sehemu hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Tanga tunalima matunda katika Wilaya ya Muheza, tuna matunda mengi sana pale, tuna machungwa sijui uende wapi usisikie chungwa la Muheza, nina imani hata huko Kusini kuna chugwa la Muheza pia, lakini Mkoa wa Tanga hatuna kiwanda cha kuchakata matunda yale. Wananchi wale wanalima machungwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Sakala.