Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Amb Dr. Diodorus Buberwa Kamala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkenge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Jambo la kwanza, mpaka wa Tanzania na Uganda uko Mtukula, Minziro, Kakunyu na hauko Bunazi. Kwa hiyo, wale wote wenye mawazo ya kufikiri kwamba ukifika Bunazi umemaliza Tanzania na hivyo wanazuia mchele, mahindi na sukari kufika Mtukula. Naomba kuanzia leo ninapozungumza hapa wakome mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbili, Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi inaeleza na kubainisha kwamba kuna nia ya dhati ya kuanzisha masoko ya mpakani, masoko ya kimkakati. Huwezi ukaanzisha masoko haya na huwezi ukatekeleza mkakati huu kama una watu ambao wanafikiria mpaka wa Tanzania ni Bunazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, kuondoa tozo kama tulivyoziondoa ni jambo jema, lakini itakuwa na maana tu kama faida itamfikia mkulima moja kwa moja. Lengo pia liwe kuhakikisha sasa tunaongeza fedha anazozipata mwananchi kutoka asilimia 88 ya sasa walau tupandishe hadi asilimia 90 ya bei ya soko la dunia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nne, makato ya 0.75% yaliyopunguzwa mpaka 0.375% ni jambo jema. Hata hivyo, lengo na best practice ni kufuta kabisa mwisho wa siku.
(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tano, kinachoitwa mifuko ya mazao ambapo kuna fedha zinakatwa na kupelekwa kusaidia mifuko hiyo ni makosa kwa sababu tulipoamua kuondoa gharama za kuendesha bodi mbalimbali hatukumaanisha kuleta makato mengine tukayaita makato ya mifuko ya mazao. Jambo hilo likome mara moja kwa sababu ni kumbebesha mkulima gharama ambazo tulishaziondoa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sita, cess 5% ambayo tunamtoza mkulima wa kahawa kupitia kwenye vyama vya msingi si jambo jema. Nchi zilizoendelea duniani kama vile Vietnam, Mexico na India, hivi sasa hutoza 1% tu kwenye border na si vinginevyo. Huu utaratibu tunaweza kuufuata na ukatusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, saba, kumkata mkulima wa kahawa kilo mbili kila gunia kwamba hiyo ndiyo gharama ya gunia si jambo jema na ni wizi wa mchana. Ukienda maeneo mengi vijijini unakuta mizani haikaguliwi na matokeo yake unaweza ukapeleka kilo 50 ukaambiwa hizo ni kilo 45, huo ni wizi wa mchana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kule Kigarama, kuna mtawala mmoja anaitwa Pastory Kabeba, mtawala huyu amekuwa akisababisha hasara kubwa kwa kupima mwenyewe kwa kufikiria anachoona kinafaa na kumbebesha hasara mkulima. Jambo hilo likome. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nane, soko la kahawa katika Afrika Mashariki tulikuwa tukifikiria sehemu tatu, tunazungumzia Jumuiya ya Ulaya, Sudan na Honduras lakini sasa South Sudan imeshajiunga na Afrika Mashariki. Kwa hiyo, badala ya kuzungumzia soko la Ulaya ambalo kwa maamuzi yetu tumeanza kujiondoa na kwa kuwa hatuwezi kuzungumzia Honduras, basi Mheshimiwa Tizeba peleka tume ya wataalam hapo South Sudan na tujiunge na Sudan tukauze kahawa yetu kwa sababu kuna soko kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule Kyakakera Wizara ilitumia shilingi milioni 497 kwa ajili ya maji ya umwagiliaji, maji hayo hata ukitaka kikombe kimoja hauwezi kukipata. Naomba hilo jambo ahangaike nalo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.