Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Jumaa Hamidu Aweso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Pangani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. JUMAA H. AWESO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia hotuba muhimu katika maendeleo ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Rais wangu, Mhshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa anayoifanya kwa wananchi wa Tanzania. Imani huzaa imani, kwa namna anavyofanya kazi tutaendelea kumuunga mkono; na hata kama uchaguzi ungekuwa mwaka 2020, mimi kura yangu ningempigia tena Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli aendelee kuwa Rais wa nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine napenda niwapongeze Mawaziri pamoja na Naibu wake na Watendaji wote wa Wizara hii kwa namna wanavyofanya kazi. Nawaona ni namna gani wanavyoweza kushiriki na wakulima, wafugaji na wavuvi katika matatizo yao. Kikubwa nawaombea Mwenyezi Mungu awabariki waendelee kufanya kazi, lakini kubwa lililonifurahisha ni namna gani walivyoweza kuondoa tozo ambazo zilizua kero, ambazo zilikuwa zinadumaza maendeleo ya wavuvi, wakulima na wafugaji. Hongereni sana, Mwenyezi Mungu awabariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesimama hapa, nilikuwa nataka nizungumzie kuhusu suala zima la zao la nazi. Pamoja na kwamba kilimo ni uti wa mgongo, lakini kila kilimo kinategemeana na mazingira yake. Ukienda Shinyanga wanategemea suala la pamba, Tabora wanategemea tumbaku na sisi wananchi wa Pangani tunategemea zao la nazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapozungumzia nazi, ninazungumzia uchumi na maisha ya wananchi wangu wa Jimbo la Pangani. Wananchi wa Pangani wamekuwa maskini kwa sababu ya mabadiliko ya tabianchi. Minazi ile imekufa, imekauka, hali ya maisha imekuwa duni sana. Naiomba Wizara hii ifanye tafiti ya dhati kabisa ili kulifufua zao hili la mnazi. Kwa sababu tunapozungumzia suala la zao la mnazi, ni moja ya kitega uchumi. Sisi binafsi tulikuwa tukichangia pato kubwa la Taifa kipindi cha nyuma; tulikuwa tukizalisha nazi kiasi cha 500,000 kwa mwezi lakini sasa hivi imeshuka tunazalisha chini ya 100,000. Kwa hiyo, tafiti zifanyike kwa haraka ili tuweze kujua ni namna gani tunaenda kulifufua zao hili la mnazi ili na sisi Wilaya yetu ya Pangani tuweze kuchangia pato la Taifa katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia juzi nilihudhuria kongamano la kuhusu suala zima la zao la korosho. Kwanza nampongeza Mkurugenzi wa Bodi hii ya Korosho kwa mkutano mzuri unaonipa matumaini. Na sisi katika Wilaya yetu ya Pangani tuna mazingira mazuri kabisa ya kufufua zao hili la korosho. Naiomba Wizara hii ituhakikishie kwamba inatupatia mbegu kwa haraka na bora ili kuhakikisha kwamba tunaenda sambamba, badala ya mnazi tunaenda sasa na zao hili la korosho kwa sababu tunaona kabisa Korosho ni zao la kijani. Kwa hiyo, tunapopanda korosho na tafiti zinafanyika kwa ajili ya kuinua zao la mnazi, nina imani uchumi wa Pangani utakuwa kwa kasi na maendeleo yatakuwa kwa kasi nasi tutaweza kuchangia pato la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo nataka nizungumzie, tunaona kabisa nchi yetu inaelekea katika suala zima la viwanda. Kama tunahitaji suala zima la viwanda, lazima tuwekeze kwa dhati kabisa katika suala zima la kilimo. Ukiangalia kilimo tunacholima sasa, tunategemea kudra za Mwenyezi Mungu. Leo mvua ikinyesha kwa wingi, kilimo kinakuwa na athari kubwa, mvua isiponyesha, pia kuna athari kubwa. Ili tuweze kuingia katika uchumi wa viwanda na tupate maendeleo makubwa ya viwanda ni lazima tuwekeze katika kilimo cha umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu imejaaliwa kuwa na mito mingi mbalimbali. Sisi katika Jimbo letu la Pangani tumekuwa na Mto Pangani, lakini tunashindwa kunufaika nao, leo mto unamwaga maji baharini kwa kukosa miundombinu mizuri ya maji. Namuomba Mheshimiwa Waziri akae na Waziri wa Maji ili watuhakikishie kwamba wanatutengenezea miundombinu ya maji ili sisi wananchi wa Pangani tuwekeze katika kilimo cha umwagiliaji. Tukiwekeza katika kilimo cha umwagiliaji, leo tunaweza tukaulisha Mkoa wa Tanga, lakini tunaweza tukailisha Zanzibar na kanda ya Kaskazini kupitia mto huu wa Pangani.

Kwa hiyo, naomba tusiishie Pangani, lakini hii iwe ajenda ya nchi ili kuhakikisha kwamba tunawekeza katika kilimo cha umwagiliaji ili tuweze kupata manufaa makubwa na malighafi ambayo itatumika katika suala zima la viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo nataka nilizungumzie hapa ni kuhusu suala zima la wavuvi. Wilaya yetu ya Pangani ina bahari ya Hindi, lakini wavuvi wale wanashindwa kunufaika kwa sababu ya kukosa uwezeshwaji wa nyenzo. Leo mvuvi wa Pangani anatumia ndoano na chambo. Hivi leo ikitokea samaki ameshamla samaki mwenzake kashiba, hivi kweli anaweza akamvua huyo samaki?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Wizara sasa tuangalie namna gani tunaweza tukawawezesha wavuvi hawa wadogo ili kuhakikisha kwamba wanapata nyenzo za kisasa ambazo zitaweza kuwasaidia ili waweze kunufaika na rasilimali bahari iliyokuwepo katika Jimbo langu la Pangani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine Mheshimiwa Waziri ambalo nataka nilizungumze ni kwamba, pamoja na kuwekeza katika bahari lakini pia tuna wafugaji katika Wilaya yetu ya Pangani. Ni sekta muhimu na ambayo inachangia mapato ya Halmashauri lakini ukiangalia wamekuwa wakikabiliwa na changamoto nyingi sana; hawana majosho wala hawana malambo.

Naiomba Wizara hii na Mheshimiwa Waziri aangalie namna anavyoweza kutusaidia. Wanasema unapozuru wengine, naomba na sisi utukumbuke, usitupite kwa kuhakikisha kwamba unatupatia majosho na malambo ili wale wafugaji wa Pangani waweze kunufaika na Wizara hii.
(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sina maneno mengi sana, ila kubwa naomba niwapongeze sana Mawaziri hawa kwa namna wanavyofanya kazi. Naiomba Serikali itoe fedha kwa dhati na kwa haraka ili iweze kutekelezeka bajeti hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsanteni sana, Mwenyezi Mungu awabariki sana.