Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. George Malima Lubeleje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nikushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hoja hii. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Makatibu Wakuu na Watendaji wote wa Wizara hii. Wanafanya kazi nzuri lakini katika mazingira magumu ya ufinyu wa bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitazungumzia mambo matatu; kwanza. nitaanza na suala la Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI). Taasisi hii ina vituo saba; kuna kituo cha Mpwapwa, Mabuki, Kongwa, Tanga, Naliendele na Uyole, lakini mimi nitazungumzia Kituo cha Utafiti wa Mifugo Mpwapwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kituo hiki kilianzishwa mwaka 1905, sasa hivi umri wake ni zaidi ya miaka 100. Hata hivyo, Kituo hiki kinakabiliwa na changamoto nyingi sana, kituo hiki ndicho kinachohudumia wafugaji Kanda ya kati, Mikoa ya Singida na Dodoma kwa sababu wanakwenda kuchukua madume bora, wanakwenda kuchukua majike yale ambayo yana mimba kwa ajili ya kufunga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 1992 na 1993, Serikali ilipunguza watumishi, lakini bahati mbaya sana Serikali ilipunguza wahudumu wote. Kwa hiyo, hata wale wahudumu wachungaji wote waliondolewa, wakamuaji wa maziwa waliondolewa, kwa hiyo wakabaki watafiti tu. Sasa najiuliza, Mheshimiwa Waziri, kama wahudumu wote walipunguzwa kazi na kituo kile kina ng’ombe zaidi ya 800, kina Mbuzi zaidi ya 400, ni nani atakaechunga? Au watafiti watapanga zamu ya kuchunga na kwenda kukamua? Wasomi wenye degree mbili, degree tatu; kwa hiyo wapange ratiba nani leo aende akachunge, nani leo aende akakamue, ni kitu ambacho hakiwezekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inapoamua mambo mengine kwa kweli wawe wanafikiria, wanaangalia uzito wa jambo. Sasa unapoondoa wahudumu; na namshukuru sana Mkurugenzi wa Taasisi, aliajiri vibarua 90, akawapanga wengine wanachunga, wengine ndiyo wanakumua na wengine wanafanya bush clearing yaani kusafisha mashamba yale ambayo mifugo wanachungwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri anisikilize vizuri. Hawa vibarua wameanza kazi tangu mwaka 2015 mpaka leo hawajalipwa mishahara yao; wana familia, wanasomesha. Kwa hiyo naomba majibu kutoka kwa Mheshimiwa Waziri, hawa vibarua wanafanya kazi nzuri, kwa sababu kama Mkurugenzi asingeajiri vibarua hii kazi ya uchungaji, ukamuaji ni nani angefanya?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna changamoto zingine; kuna upungufu wa magari, matrekta pamoja na pikipiki kwa ajili ya wale Extension Officers.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine kuhusu kuhamisha kituo cha uchunguzi wa magonjwa ya mifugo na kukileta Dodoma. Mheshimiwa Waziri naomba anisikilize vizuri sana; Mawaziri wote wa mifugo waliopita akiwemo Mheshimiwa Rais Magufuli aliwahi kuwa Waziri wa Mifugo alikataa ile Taasisi ya Uchunguzi wa Magonjwa isihamishiwe Dodoma. Sasa walipoona Mheshimiwa Lubeleje mwaka 2010, 2015 amepata likizo siyo Mbunge wakaihamishia haraka haraka Dodoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Dodoma hakuna majengo ya Maabara. Pale Mpwapwa kuna jengo zuri, mwaka juzi wamejenga jengo zuri sana la Maabara, kwa hiyo wamehama vifaa vingine wamekuja navyo Dodoma, vingine wamefungia kwenye stoo pale Mpwapwa; yale majengo Mpwapwa yanaharibika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na sababu gani ya kuhamisha kile kituo? Kwa sababu waliojenga kituo cha utafiti wa mifugo Mpwapwa ndio waliojenga Taasisi ya Uchunguzi wa Magonjwa kwa sababu vinakwenda pamoja. Ng’ombe akiugua kwenye Taasisi ya utafiti analetwa pale VIC kwenye Taasisi ya Uchunguzi wa Magonjwa wanamchunguza ana tatizo gani, lakini baadaye wamejenga chuo cha Maafisa wa Mifugo kwenye Chuo cha Mifugo ili practicals wawe wanachukua pale VIC.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale chuo cha mifugo wanasoma theory lakini practicals walikuwa wanafanya hapa Taasisi ya Uchunguzi wa Magonjwa, maana hawa ni wataalam wa mifugo; wanasoma anatomy physiology, animal deseases pamoja na meat inspection; sasa practicals lazima wakafanyie pale Taasisi ya Uchunguzi wa Magonjwa hata meat inspection, maana wale wanajifunza ant-mortem inspection na post-mortem, sasa practicals lazima wakafanyie kwenye Taasisi ya Uchunguzi wa Magonjwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanapochukua yule ng’ombe wanaanza kumchunguza ana tatizo gani, amekufa kwa ugonjwa gani. Kuna vidudu vingine vya magonjwa ya mifugo vinaonekana kama liver flukes, Cysticercus bovis vinaonekana, vile vile kama anthracis bacillus na Tubercle bacilli mpaka utumie darubini kali. Sasa ninyi wanahamisha kituo kile wanaleta Dodoma, hao wanafunzi wawe wanatoka Mpwapwa wanakuja kujifunza Dodoma? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana Mheshimiwa Waziri arudishe kituo kile haraka sana Mpwapwa la sivyo leo nashika shilingi. Kuna mtaalam mmoja pale ndiye aliyelazimisha kituo kihame, akasema Lubeleje ndiye Mbunge ambaye anazuia sasa ameondoka na bahati mbaya amestaafu, ndiye amelazimisha kituo kuhamia hapa. Sasa Waziri anieleze ametenga fedha kiasi gani, wanafunzi watoke Mpwapwa kuja kuchukua practicals huku Dodoma? Kwa hiyo, naomba anieleze Mheshimiwa Waziri mpango wa kuhamisha kituo hiki kirudi Mpwapwa haraka iwezekanavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ni upungufu wa chakula katika Mkoa wa Dodoma Wilaya ya Mpwapwa na Mkoa wa Dodoma. Mheshimiwa Waziri alitoa kauli ya Serikali hapa Bungeni kwamba kuna Halmashauri 55 zina upungufu wa chakula, alikiri mwenyewe hapa na alisema kwenye maghala yetu ya hifadhi kuna chakula cha kutosha lakini nashangaa hawakugawa hata gunia moja kwenye vijiji ambavyo vimeathirika na chakula. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge tunasema majimbo yetu yana njaa, yana upungufu wa chakula tunaomba watusikilize. Sasa kama chakula kiko kwenye maghala na hapa tunapitisha, mwaka wa jana tumepitisha bajeti bilioni 18, zimetolewa bilioni tisa, hizo bilioni tisa ndizo zimenunua chakula kwahiyo kama chakula kidogo kipo, basi wasambaze kwa maeneo ambayo hakuna chakula ikiwa ni pamoja na Wilaya ya Mpwapwa na Mkoa wa Dodoma…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naomba wagawe hicho chakula ili wananchi wasiweze kununua debe la mahindi kwa Sh.25,000/= na gunia la mahindi kwa Sh.120,000/=.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.