Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi hii nami niweze kuchangia hotuba ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi. Awali ya yote naomba niunge mkono hoja hii. Pia napenda niipongeze Serikali ya Awamu ya Tano kwa namna inavyojitahidi kufanya utafiti kuhusiana na zao la pamba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara hii imekuwa ikifanya utafiti wa aina mbalimbali hatimaye ulitoa mbegu aina ya manyoya kwenda kwenye mbegu ambayo haina manyoya. Pamoja na changamoto zilizopo katika mbegu hiyo, Serikali imejitahidi kutoa elimu kwa wakulima na hatimaye wakulima wameweza kufanya kama inavyotakiwa na hapa tunaona ongezeko la pamba mbegu kutoka tani 122,000 mpaka 150,000. Kwa hiyo, kuna kuwa na ongezeko la tani 28,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakiri kwamba zao hili ni zao la uchumi katika Mikoa yetu ya Magharibi. Ni zao ambalo linategemewa lakini limeonekana haliwezi kumnufaisha mkulima kama inavyotakiwa. Pamoja na elimu inayotolewa hii mbegu ambayo imetolewa manyoya ambayo ni UK 91 imekaa muda mrefu sokoni na kupoteza ubora wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika michango yangu iliyopita niliweza kuchangia kuhusu udhaifu wa mbegu hii, mbegu hii imekuwa ina matunda machache sana ukilinganisha na wakati ilivyokuwa inaanza. Kwa sasa inakuwa ina matunda kumi tu kwenye shina hadi ishirini kwenye shina moja, kwa hiyo inasababisha uvunaji wa kilo 300 katika heka. Kwa hiyo, pale bado hatujamsaidia vizuri mkulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru Serikali baada ya kusikia michango yetu iliyopita sasa imeweza kuja na mbegu mbya aina ya UK M08. Sisi Wabunge tunaotoka Mkoa wa Simiyu tunaelewa kwamba mbegu hii imefanyiwa majaribio katika Kata ya Mwabusalu na kuanzia inavyoota majani yanavyotoka mbegu hii imekuwa ikiweka matunda kuanzia chini mpaka juu na mpaka sasa takribani kuna wastani wa matunda 50 mpaka 100 katika shina moja na hivyo kutegemea katika msimu huu kilo zitaongezeka kwa heka moja kutoka kilo 300 mpaka 1000 au 1200. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshangaa Mbunge mwenzangu wa Mkoa wa Simiyu ambaye bado anaongelea mbegu ya manyoya; Simiyu hatupo huko. Huyo haudhurii vikao vya RCC, hajui Simiyu tunaendaje, kwa hiyo asiturudishe nyuma kwenye mbegu za manyoya, sisi tupo na mbegu ya UK M08.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri, kabla pamba hii haijaanza kuvunwa katika Kata ya Mwabusalu aende akaingalie kwa namna ilivyostawi ili walete sasa mbegu ya kutosha katika Mkoa wa Simiyu, hatutegemei tena kutumia mbegu ya UK 91. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo tatizo lingine la pembejeo; wakulima wa pamba walizoea dawa ya pembejeo ya mafuta, lakini nimefuatilia na kuona kwamba dawa hii imekataliwa kwa sababu ina sumu nyingi na kuletwa aina nyingine ya dawa ya maji aina ya bametrim. Dawa hii bado haiui wadudu vizuri, tunaomba pia utafiti uendelee kufanyika ili dawa hii iweze kuwaua wadudu vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zao hili pia linakaribiwa pia na kupungua kwa mbolea katika ardhi, tunaomba wakulima wahamasishwe kwa hiyari waweze kuweka samadi, tunao ng’ombe wengi hivyo waweke samadi ambayo itaweza kuiboresha ile rutuba ambayo muda mrefu mbolea yake imeonekana kupungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo changamoto zingine; mzunguko dhaifu wa usambazaji wa pembejeo. Taasisi zenye msaada dhaifu kiufundi na kifedha kama Mfuko wa Uendelezaji Zao la Pamba (CDTF) pamoja na Bodi ya Pamba zimekuwa hazina msaada wa karibu kwa wakulima. Mkulima anakatwa Sh.15/= kwa kilo kwa ajili ya kuongeza uboreshaji wa zao hilo lakini matokeo pembejeo zimekuwa haziletwi kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunamwomba Mheshimiwa Waziri Mkuu aziangalie hizi taasisi, ziimarishwe au zifanyiwe kama kule kwenye Bodi za Korosho kulivyofanywa ili na sisi wananchi wa Simiyu wakulima wa pamba tunahitaji tija katika zao letu la pamba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nichangie tozo katika sekta ya mifugo; naipongeza Serikali kwa namna inavyoendelea kufuta tozo katika sekta hii ya mifugo. Kabla sijachangia naomba niweke kumbukumbu sahihi, siyo kweli kwamba mfugaji anapopeleka ng’ombe wake mnadani anatozwa ushuru wowote, mfugaji huyo ambaye kwa jina lingine anajulikana kama muuzaji. Serikali ilifuta ushuru wa aina yoyote kwa mfugaji anaepeleka mfugo wake mnadani toka mwaka 2003. Baadhi ya ushuru kama wa Halmashauri ulifidiwa na Serikali kuu kwa ile general purpose. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwahiyo, Mheshimiwa Mbunge naposema kwamba wananchi wa Simiyu wale wafugaji wanatozwa ushuru anapotosha. Ushuru unaotozwa ni kwa mnunuzi; kuna ushuru wa Halmashauri na ushuru wa kusafirisha mifugo nje ya Wilaya. Nashukuru Serikali imeazimia kuufuta ushuru huo nami naiunga mkono.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiunga mkono kwa sababu ushuru huu haukuwa na tija yoyote kwa Halmashauri au Serikali Kuu. Serikali iangalie vyanzo vya Serikali Kuu vinavyotozwa kule chini kwa kutumia ERV na stakabadhi yoyote inayotoka Serikali Kuu, fedha nyingi haiingii katika Mfuko wa Serikali, inaingia katika mifuko ya watu binafsi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama unataka kushuhudia hilo, tafuta wiki moja yoyote uangalie makusanyo ya ushuru yaliyotokana na mifugo kwa wiki katika Halmashauri moja ulinganishe na zile permit zilizokusanywa na Serikali Kuu kwa idadi ya ng’ombe. Obviously, ng’ombe waliokusanywa na halmasahuri wako juu kuliko waliokusanywa na Serikali Kuu, kwa hiyo fedha nyingi inaingia katika mifuko ya watumishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna huu mnada wa upili, Mnada wa Mhunze, mnada huu ni secondary market. Wafanyabiashara wengi wa mifugo…
…naomba itozwe ile tozo ya Sh.2,500/= kwa sababu Sh.5,000/=…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.