Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Naibu Spika, kabla ya kuanza kuchangia kwanza nitoe pole kwa wananchi wa Mikumi kwa tahayari kubwa na mshtuko mkubwa ambao umetokea jana baada ya vijana saba kupotea kwenye mazingira ya kutatanisha kwenye Hifadhi ya Mikumi. Hatuna uhakika kama hawa wenzetu wako salama huko waliko au itakuwa ule utaratibu wa kuzika nguo ndugu zetu hatuwaoni. Niwaambie tu ndugu zangu wa Mikumi kwamba tupo pamoja, na mimi nitaungana nao kesho kuangalia ndugu zetu wana hali gani. Niwatoe hofu tu kwamba tumeshalifikisha kwenye sehemu zinazohusika, naamini watatumia muda wao na upendo wao kama Watanzania kuweza kujua wenzetu wapo wapi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kuchangia kwenye Wizara hii nyeti, Wizara ambayo ni uti wa mgongo wa Tanzania, ambayo inatoa zaidi ya asilimia 75 ya ajira, lakini pia kwa mwaka 2016 imeweza kutoa asilimia 29 ya pato la Taifa. Pia katika Wizara hii ambayo tunasema ni nyeti kumekuwa na changamoto nyingi sana, lakini changamoto kubwa ambayo tunaiona ni changamoto ya bajeti yenyewe. Kwa kuwa kwa mwaka 2016/2017 tunaona kwamba fedha za maendeleo zilikuwa zimetengwa shilingi bilioni 100 lakini mpaka Mei 4, 2017 ilikuwa imekwenda asilimia tatu tu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unaweza ukaona ni jinsi gani ambavyo bado kama nchi tuna tatizo. Hii ni shida kubwa sana kama kweli tunasema kilimo ni uti wa mgongo na unatoa ajira kubwa kwa Watanzania kama hivi; nadhani tunapaswa kujiongeza zaidi ili tuweze kuona jinsi gani tunaweza kuwasaidia wakulima wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hizo pesa ambazo ni shilingi bilioni 100 kuwa zimetengwa, lakini fedha za ndani zinaonekana ni shilingi bilioni 23 tu na fedha ambazo tunategemea wafadhili ni shilingi bilioni 78. Kwa hiyo, hapo napo unaweza ukaona kwamba wafadhili wakileta migomo kama ambavyo inaonekana sitofahamu nyingi, hii nchi inaelekea pabaya zaidi na ndiyo maana kila siku na kila kona unasikia watu wanalia njaa, watu wanalia kuna uhaba wa chakula ingawa visingizio ni vingi kwamba tabianchi nayo inachangia. Hata hivyo pia sisi wenyewe kama nchi hatujajipanga ipasavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mwaka 2017/2018 inaonekana bajeti kwa ujumla imetengwa shilingi bilioni 267 na kati ya hizo shilingi bilioni 156 ni za maendeleo, shilingi bilioni 150 zipo kwenye Kilimo, shilingi bilioni nne kwa ajili ya Mifugo na shilingi bilioni mbili kwa ajili ya Uvuvi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ninatokea kwenye Mkoa wa Morogoro ambao Serikali ina mpango wa kuufanya Mkoa wa Morogoro kuwa Ghala la Taifa, kwa sababu Morogoro tumebarikiwa ardhi nzuri, lakini pia ina rutuba na pia inalima aina nyingi za mazao na kila mmea unakubali, na ndiyo maana tumeamua kuwa hivyo, na sababu pia Morogoro ni center na vitu kama hivyo. Lakini kwa style hii ya kutenga bilioni nne kwa ajili ya mifugo si dhani kama tunakwenda kumaliza tatizo la migogoro ya wakulima na wafugaji. Pia kwenye bajeti hiyo kwa miaka mitatu mfululizo pale Wilayani kwangu Kilosa pesa za bajeti hiyo hazijaweza kufika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nikuombe Mheshimiwa Waziri, utakapokuja utuambie ni kwa nini Kilosa inakuwa inasahaulika sana na kuna upendeleo wa maeneo mengine mengine, lakini Wilaya ya Kilosa ambayo ni Wilaya nyeti yenye ardhi nzuri na yenye rutuba, imekuwa ikiwa nyuma sana ikipelekewa pesa za maendeleo basi ni kwa miaka mitatu mfululizo. Na kwa style hii Mheshimiwa Waziri nataka nikuahidi tutakabana sana mashati kwa sababu sasa tumeamua kuwekeza kwenye kilimo na tunajua ndicho kitakachotutoa kama nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo wananchi wa Tindiga, Mabwerebwere, Kilangali, Masanze, Muhenda, Malolo ambao wanategemea sana kilimo wamekata tamaa kwa sababu wanaona kama Serikali inawaacha peke yao. Hata zile pembejeo pamoja na madawa, mbolea zinaonekana hazifiki kwa wakati, na ndiyo maana wananchi wa kule wamekuwa na tabu kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu kingine ni kuhusu wakulima wa miwa ambao ni asilimia kubwa sana katika jimbo letu la Mikumi kwenye kata za Ruhembe, Kidodi pamoja na Ruaha, lakini pia hata watu wa Vidunda na Mikumi wameonekana kulima kilimo hiki cha miwa. Kilimo cha miwa kimetoa ajira kubwa sana kwetu na ninashukuru sana kiwanda cha Ilovo juzi wametangaza bei ya muwa kutoka shilingi 79,000 sasa hivi ni shilingi 101,000, hilo Mheshimiwa Waziri nitakupongeza kidogo; hii ni kwa sababu wakulima wamekuwa wakilia kwa muda mrefu. Hata hivyo bado haitoshi, tunataka kusema kwamba wakulima wa miwa bado wamekuwa na shida kubwa na Mheshimiwa wanakusubiri kwa hamu kwa sababu kilio chao kimeonekana bado hakiwezi kupata solution ya kudumu.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakulima wa miwa sasa hivi wameambiwa na wamepata agizo kutoka Serikalini watoke kwenye vyama vyao vya hiyali vyama vyao vya kiraia waweze kujiunga na vyama vya ushirika. Hilo ni wazo zuri ni wazo jema na mimi kama Mbunge nali-support lakini naona kama muda ambao tumewapa wale wakulima ku-shift kutoka kule kwenda huku bado ni muda mdogo sana wanahitaji kupata elimu kwa sababu tumeona vyama vingi vya ushirika vikiwa na matatizo kadha wa kadha lazima tuwaeleze faida na hasara hiyo iliwakiweza kujitoa wajitoe kwa umuhimu na wajue jinsi gani ya kushirikiana na sisi, maana naamini tukiwapa elimu ya kutosha wanaweza nao kushirikiana na sisi. Lakini sasa hivi kuna mgomo baridi Mheshimiwa Waziri wakulima wengine wanagoma wengine wanaenda lakini tunasema tukienda kwa pamoja tukawapa elimu tunaweza tukafanikiwa kwenye hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakulima wa miwa wamekuwa na tatizo lingine, wananchi wengine na wakulima wa nchi zingine wanalipwa pia masuala ya bagasse lakini na wanalipwa masuala ya molasses. Bagasse ni tatizo kubwa ambalo pia kiwanda kinawalipa utamu peke yake yaani sucrose. Lakini ingeweza kuwalipa bagasse ambayo inatengeneza mashudu, mbolea, pia umeme lakini wakulima hawapati faida yoyote kupitia hiyo. Vilevile molasses ambayo inatengeneza spirit na inatengeneza pombe, pale pale ilovo kwa pembeni kuna kiwanda cha pombe; lakini wakulima wa kule bonde la Ruhembe hawanufaiki kwa njia yoyote na vile vitu, wanalipwa utamu peke yake, yaani sucrose. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na hata huo utamu wenyewe umekuwa ukionekana kuwa na walakini, inaonekana gauge yenyewe inakwenda kwenye saba mpaka nne wakati wataalamu waliokuja kule wanasema hakuna gauge ya saba wala ya nne bali utamu unatakiwa kwenye gauge 11 na kuendelea Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ikumbuke kwamba wakulima wa bonde la Ruhembe wanalalamikia kuhusu utamu na wanalalamika sana kwa kusema kwamba hakuna gauge nne wala gauge saba bali wanapunjwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia wana tatizo lingine la mzani, wamekuwa wakiomba kila siku kwamba wanataka wakulima wa nje wawe na mzani wao binafsi kabla ya kuingiza kule kiwandani kwa sababu mtu wa kiwanda yeye ndiye anayepima, yeye ndiye anayepanga bei na yeye ndiye anayefanya kila kitu inawaumiza sana wakulima wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwa sababu nchi hii inajua umuhimu wa sukari na inatoka kwa wingi kule Kilombero basi jaribu kuwashika mkono wakulima wa miwa wa kule Kilombero ili waweze kufanya na kulima kwa bidii, naamini wakilipwa kwa uwiano huo itawasaidia sana. Ndiyo maana juzi Mheshimiwa Waziri mmekamata magari ya kupeleka miwa ya kutoka Kilombero kwenda Kenya, ni kwa sababu watu wanakimbilia bei nzuri, na hawalipwi utamu peke yake wanalipwa bagasse, wanalipwa molasses na vitu vingine. Kwa hiyo na sisi naamini tukijiongeza tutaweza kuwatengeneza wakulima.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia wakulima wamekuwa wakilalamika kuhusu DRD, wanasema zile asilimia za kuingiza miwa mule kiwandani zimekuwa ndogo, iko 40 kwa 60 angalau ingekuwa 50 kwa 50 au 55 kwa 45 ingeweza kuwasaidia kidogo ili miwa iweze kuwa inapatikana kwa wingi. Lakini pia kulikuwa na wazo la kutengeneza kiwanda kingine kule Mfilisi, sasa hatujui hicho kiwanda kimefikia wapi sasa nategemea Mheshimiwa Waziri utakuja kunijibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni kuhusu migogoro ya wakulima na wafugaji. Nashukuru sana wakati ndugu yangu Augustine Mtitu alipopigwa mkuki wa mdomoni ukatokea shingoni, baada ya kilio kidogo Mheshimiwa Waziri ulifika ingawa ulininyatianyatia, hukufika kwa wakati na hukanishtua vizuri nilisikia tu kwamba umetokea na ukaingia mitini. Napenda siku nyingine ukija jimboni unitaarifu nikiwa kama Mbunge na muwakilishi wa wananchi ili tuweze kujadiliana kwa kina na tuweze kujua jinsi gani tunaweza tukawasaidia wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini migogoro ya wakulima na wafugaji halijakwisha, bado kuna migogoro mingi na ninaamini hili suala ni mtambuka linahitaji Waziri wa Ardhi, Waziri wa Maliasili na Utalii lakini pia na Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi na pamoja na Waziri wa Mambo ya Ndani tuweze kukaa na kulijadili kwa sababu inaonekana upimaji wa ardhi imekuwa ni tatizo kubwa kule Kilosa, lakini pia yale maeneo tengefu yamekuwa yanaongezwa kila siku, vile vile ardhi imekuwa ni tatizo sana kwa wananchi wa Jimbo la Mikumi na Wilaya ya Kilosa kwa ujumla. Kwa hiyo niombe Mheshimiwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, tumekuomba sana, utakapokuja uturudishie yale mashamba makubwa, mashamba kama Sumagro, Kisanga, Kilosa Estate, Miyombo Estate ni mashamba ambayo yameachwa mengi nimashmba pori tunaomba uturudishie iliwananchi waweze kufanya kazi yake yao…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)