Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, nami nichangie kidogo kwenye Wizara hii ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji. Jimboni kwangu Mikumi kuna kiwanda cha Sukari cha Kilombero ambacho kinafanya kazi nzuri sana ya uzalishaji wa sukari, lakini kumekuwa na malalamiko ya muda mrefu sana kutoka kwa wafanyakazi zaidi ya 3,000 waliofukuzwa kazi bila kulipwa mafao yao mwanzoni mwa mwaka 2000.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa sana Mheshimiwa Waziri atakapokuja kujumuisha afafanue ni lini hawa wafanyakazi waliokuwa wakifanya kazi Kilombero Sugar Company kabla haijabinafsishwa kwa Illovo watalipwa mafao yao? Pia kumekuwa na malalamiko kutoka kwa wakulima wa nje (outgrowers) ambao wamekuwa wakilalamika kuhusu kupunjwa sana kwenye mzani ambao unamilikiwa na wenye kiwanda. Je ni lini Serikali itawaagiza wenye kiwanda cha Illovo kuweka mzani utakaokuwa wa uwazi ili kuwafanya wakulima kupata haki yao ya kujua mazao yao yanayoingizwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, pia wakulima wa miwa wa Bonde la Ruhembe wamekuwa na malalamiko ya muda mrefu ya kipimo cha Sucrose (utamu) ambayo wamekuwa wakipunjwa kwa kuambiwa utamu wa miwa yao ni mdogo sana hivyo kulipwa fedha kidogo sana pia. Wakulima wa bonde la Ruhembe wamekuwa wakiomba sana kwamba pamoja na kulipwa sucrose pia walipwe na molasses na buggers ambazo zinatumiwa na watu wa kiwanda cha Illovo kutengeneza mashudu, mbolea, spirit na hata umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wakulima wa Bonde la Ruhembe wanalia sana bila matumaini kwa nini wanalipwa utamu (sucrose) peke yake wakati mazao yao yanatoa pia products zingine ambazo wenye kiwanda cha Illovo wanazitumia na kuuza bila kuwalipa tofauti na nchi za jirani kama Kenya na Malawi ambako wakulima wanalipwa pia fedha za bugger na molasses na kuwasaidia sana kufaidika zaidi na kilimo hicho cha miwa na kuwaongezea zaidi uchumi wao.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana Mheshimiwa Waziri, atakapokuja ku-wind up atuambie ni kwa nini Serikali haiwaagizi wamiliki wa viwanda kwanza kuwalipa wakulima wa miwa bei nzuri za Bugger na molasses? Sambamba na hilo kwa nini bado bei ya tani ya miwa kutoka kwa wakulima wa nje bado inasuasua?

Mheshimiwa Naibu Spika, tuliambiwa kuwa pale Kijiji cha Mufilisi kingejengwa kiwanda kingine kidogo cha Sukari ifikapo mwaka huu wa 2017, lakini mpaka sasa hakuna dalili yoyote ya kujengwa kwa kiwanda hicho cha sukari pale Mufilisi ambacho kingesaidia sana kuleta ajira na pia kurahisisha usafirishaji wa miwa kutoka Kata za Mikumi na Kisanga. Je mpango huo wa kiwanda cha sukari cha Mufilisi kimefikia wapi na ni lini kitakamilika na kuanza kazi? Au ndiyo yale yale ya kwenye utaratibu bila kutekelezeka?

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa kwenye Jimbo la Mikumi Kata za Malolo, Masanga, Mhenda, Mabuerebuere, Kilangali na Tindiga kuna mazao ya aina mbalimbali tena kwa wingi sana, nadhani sasa Serikali ili iweze kufikia malengo yake ya kuifanya Tanzania kuwa nchi ya viwanda basi ingeangalia sana umuhimu wa kujenga viwanda vidogo vidogo kwenye Jimbo la Mikumi, ambayo pia vingeenda sambamba na kuhakikisha umeme unafika kwenye kata hizi za Jimbo la Mikumi na Wilaya ya Kilosa kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia katika kurekebisha miundombinu ya barabara, naamini kabisa kilimo kinacholimwa Jimboni Mikumi kitasaidia sana kufanikisha kutoa ajira kwa wananchi wengi zaidi; pia kufikia malengo ya Serikali hii ya kuifanya Tanzania kuwa nchi ya viwanda, lakini vile vile kufanikisha kuufanya Mkoa wa Morogoro kuwa ghala la Taifa. Tumebakiwa na ardhi nzuri, kubwa na yenye rutuba na Wanamorogoro wapo tayari kulima kwa bidii; cha msingi ni kuwawekea viwanda ili wapate uhakika wa masoko ya mazao yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.