Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Rashid Abdallah Shangazi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mlalo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kutoa mchango wangu kwenye Wizara hii hasa kwenye eneo la uwezeshaji na uwekezaji. Katika Jimbo la Mlalo, Halmashauri ya Lushoto, wakulima wadogo wameanzisha kilimo cha mazao ya mchaichai ambacho kina tija kubwa kwa sababu ni malighafi ya bidhaa mbalimbali. Tatizo kubwa ni udhaifu mkubwa wa Idara ya Biashara ya Halmashauri kuziona fursa za kiuchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa soko pekee tunalolitegemea ni Kisiwani Pemba ambalo ni soko la kati na siyo soko la moja kwa moja kwa mlaji. Tunaomba kwa dhati, Wizara hii iwatafutie wananchi wa Mlalo masoko ya moja kwa moja ya bidhaa ghafi ya mchaichai ili waweze kukuza uchumi na kipato chao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia mdau wa ndani wananchi wa Mlalo wamethubutu kukopa mtambo wa kusaga na kukamua majani ya mchaichai kuepuka adha ya kusafirisha majani ghafi kwenda Pemba ambako kwa sasa ndiko soko la kati lilipo. Kupitia kampuni ya kukopesha mitambo ya EFICA mdau ameweza kukopa mtambo na sasa wananchi wamepata hamasa kubwa ya kuchangamkia fursa hii adhimu tatizo pekee sasa ni soko la moja kwa moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kiwanda cha Kusindika Chai cha Mponde kule Bumbuli bado ni changamoto. Wawekezaji teule wa Mfuko wa Hifadhi wa LAPF bado hawajaonyesha dhamira ya dhati ya haraka ya kufanikisha zoezi hili. Kata zaidi ya 15 zinategemea chai kama zao kuu la kiuchumi, tozo za Halmashauri zinapatikana kupitia chai, tunaiomba Serikali ilione hili kwa jicho la huruma sana kuwasaidia wananchi wa Bumbuli.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kiwanda cha AFRITEX Tanga kinachotengeneza nguo pale Tanga mjini kimefungwa kwa sababu ya kodi. Tafadhali naomba tufuatilie ili kuona tatizo hili ambalo limefanya ajira zaidi watu 2,000 za moja kwa moja ziwe hatarini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kiwanda cha RHINO CEMENT kimeshusha uzalishaji baada ya kukosa malighafi za kutosha za makaa ya mawe kutoka Liganga na Mchuchuma. Napendekeza sana wapewe mrahaba kama waliopewa wawekezaji wa Dangote ile waweze kupata malighafi ya kutosha. Kiwanda kina uwezo wa kuzalisha saruji tani 20,000 kwa mwezi lakini upatikanaji wa malighafi ni chini ya tani 1,000 kwa mwezi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na nia njema ya Serikali ya kuelekea uchumi wa kati unaotokana na uchumi wa viwanda, bado hatupaswi hata kidogo kupuuza matatizo ya viwanda vilivyopo. Kiwanda cha Sabuni cha Foma, TIP Soap Industries vyote vimekufa, Tanga kunani?

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.