Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Felister Aloyce Bura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Mheshimiwa Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa kazi nzuri, kadhalika na Watendaji wa Wizara hii. Suala la Makaa ya Mawe, Mchuchuma na chuma cha Liganga, Ludewa ni la muda mrefu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri, hakuna maelezo yanayojitosheleza kuhusu utekelezaji wa mradi. Kila kipindi cha bajeti, maelezo ni hayo hayo ya Kamati ya Watalaam kupitia mapendekezo ya mwekezaji. Serikali ieleze Bunge lako Tukufu tatizo la uwekezaji Mchuchuma na Liganga. Tunajenga reli tunahitaji chuma! Tutaagiza chuma kutoka nje ya nchi wakati Mungu katujaalia chuma Liganga!

Mheshimiwa Naibu Spika, CAMARTEC ni kiwanda kinachotengeneza zana za kilimo. Hata hivyo, vifaa vya CAMARTEC havipatikani kwa wingi kwa wakulima; wangeweza kufanya kazi kubwa na kwa wepesi zaidi kwa kutumia vifaa vya CAMARTEC; vifaa vya kupandia, kupalilia, kuvunia na kuchakata mazao. Kwa kuwa viwanda vingi vya hapa nchini vinategemea malighafi ya mazao ya hapa nchini, naomba Serikali kuhakikisha kuwa vifaa vinavyoweza kumrahisishia mkulima kazi, viuzwe kwa wingi na kwa bei nafuu kwa wakulima.

Mheshimiwa Naibu Spika, Watanzania tunatamani kuwa na viwanda vingi kila Wilaya au kila Mkoa, lakini je, tumejiandaa vipi kuhusu malighafi, barabara, umeme, mifugo bora, mazao bora na yanayolimwa mwaka mzima na kadhalika? Maandalizi yanahitajika sana kwa wananchi kulima mazao bora yanayolimwa mwaka mzima, ufugaji wa kisasa na umeme usio na shaka kwa wenye viwanda na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiamini Serikali ya Awamu ya Tano, hivyo ni kukumbushana mambo muhimu kwa maandalizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, waliouziwa viwanda na kuvigeuza maghala na vingine havitumiki kabisa: Je, Serikali inasema nini juu ya viwanda hivyo? Naomba maelezo ya Kiwanda cha Maziwa Utegi, Rorya kilichobinafsishwa na kilikuwa na mali nyingi na mpaka sasa hakifanyi kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania tuna mifugo ya kutosha na tungeweza kuuza bidhaa/mazao ya mifugo na kuingiza fedha nyingi nchini. Tatizo letu ni viwanda vya mazao ya mifugo. Hatuna viwanda vya nyama, ngozi, maziwa na kadhalika. Serikali ina mpango gani wa kuanzisha viwanda vya kusindika nyama, maziwa na ngozi? Viwanda vilivyopo vya watu binafsi havikidhi mahitaji ikilinganishwa na mifugo iliyopo. Naamini tukitumia vizuri Sekta ya Mifugo kelele/ ugomvi kwa wakulima na wafugaji ungekwisha kwa amani na kwa urahisi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mifuko ya Hifadhi ya Jamii inafanya kazi nzuri kwa maendeleo ya Taifa hili. Mifuko hiyo imejenga majengo makubwa mazuri katika miji yetu; na kwa sababu mifuko hiyo, inatarajia kujenga viwanda katika maeneo mbalimbali. Kwa taarifa zisizo rasmi, Mfuko wa PSPF haupo vizuri sana kifedha: Je, utakuwa na uwezo wa uwekezaji kama Hotuba ya Mheshimiwa Waziri inavyojieleza ukurasa wa 170?

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.