Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii. Nami nianze kwa kuipongeza Serikali kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya. Nampongeza Mheshimiwa Rais kwa dhamira ya dhati ya kuleta viwanda nchi nzima. Sera ya Viwanda ni sera nzuri sana ambayo kimsingi, yeyote atakayeipinga ni yule ambaye hajui umuhimu wa viwanda katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sera hii imeoanisha mazingira mazuri kwamba kila mkoa ni lazima kuwe na viwanda ambayo vitawasaidia wananchi wetu kuweza kukuza uchumi ndani ya maeneo yao. Nzuri zaidi ni pale ambapo sera hii inaonesha maeneo ambayo yalisahaulika hasa pembezoni, yapewe kipaumbele ili yaweze kunufaika na mpango wa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niishauri tu Serikali kwamba, katika sera ambayo imewekwa, Sera ya Viwanda ni vyema wakaangalia mazingira ili tupeleke viwanda mahali ambapo uhitaji wa viwanda unafanana na mazingira yenyewe. Leo hii unapopeleka kiwanda cha kusindika ngozi kwenye maeneo ambayo hayana hata mifugo, hujawasaidia wananchi pale, hasa wale ambao wanatoka kwenye maeneo ya ufugaji. Ni vyema vile viwanda ambavyo vitakuwa vinahusiana na Sekta ya Mifugo, tukawapelekea kwenye maeneo husika ya uzalishaji ili viweze kutoa ajira kwenye maeneo ambayo wananchi wenyewe wanahusika na kulengwa moja kwa moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile tulikuwa tunaomba kuangalia mazingira ya kuboresha Sekta ya Viwanda hasa viwanda vidogo vidogo. Kwenye maeneo haya ni vema Serikali sasa wakawa na mipango thabiti itakayokuwa inaunganisha nchi nzima na kwa kuwashirikisha Wakuu wa Mikoa ili waweze kutenga maeneo ambayo yatakuwa rafiki kuwasaidia wananchi ambao kimsingi tukiboresha kwenye Sekta ya Viwanda vidogo vidogo, tumewasaidia wananchi walio wengi. Huko ndiko ambako ajira zinatengenezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri, lazima aje na mpango mkakati wa kuwashirikisha Wakuu wa Mikoa ili kuhakikisha maeneo ya viwanda vidogo vidogo yanapewa kipaumbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali itusaidie mikoa ya pembezoni; kule tunazalisha. Mkoa wangu ulishatenga maeneo ya uwekezaji. Nafikiri kila kitu kipo sawa, lakini tunaomba sasa ielekeze suala zima la kuwekeza kwenye mazao yanayozalishwa na wananchi hasa kwenye Sekta ya Kilimo. Tukielekeza huko, tutawasaidia sana wananchi ambao ni wengi. Mazao ya mafuta yanayozalishwa, tukiweka mipango mikakati mizuri, kwamba yale mazao ya mbegu za mafuta ambayo yanazalishwa, tukajenga viwanda vidogo vidogo huko, tutakuwa tumewasaidia sana wananchi ili waweze kujikwamua kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yapo mazao ya chakula. Mkoani kwangu tunazalisha chakula kingi na tunauza mazao ambayo bado hayajasindikwa. Naiomba Serikali, pale ambapo tunafikiria mikoa ya pembezoni; Mkoa wa Katavi, Mkoa wa Rukwa na Mkoa wa Kigoma ni vema sasa tukawa na viwanda ambavyo vitafanya kazi ya kuwasaidia wananchi kwenye maeneo hayo na eneo hilo likawa na ukuzaji wa kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bado tuna mazao ya biashara; tuna zao la tumbaku kwenye Mikoa hiyo ya Tabora, Kigoma na Katavi. Hatujakuwa na kiwanda maalum ambacho kitasaidia kukuza zao hili. Ni vema sasa Serikali ikaja na mpango ambao utasaidia maeneo hayo ili kupata kiwanda ambacho kitasaidia kukuza uchumi ndani ya maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna maeneo mazuri ya kivutio cha uwekezaji. Lipo zao la miwa, kama Mkoa wa Kigoma wangepewa fursa, wana mabonde mazuri. Mfano, bonde la Mto Malagarasi; katika Mkoa wa Katavi, Rukwa vile vile; tunahitaji tupate Kiwanda cha Sukari kwenye maeneo haya ili tuweze kupunguza bei ya sukari kwenye maeneo ya pembezoni.

Mheshimiwa Naibu Spika, bado naiomba Serikali iandae mazingira ya kujenga Kiwanda cha Saruji kwenye maeneo haya; ni maeneo ambayo bei za saruji ni kubwa kweli kwa sababu viwanda vingi vimeelekezwa Mkoa wa Dar es Salaam, Mkoa wa Pwani lakini maeneo ya pembezoni hakuna. Naiomba Serikali iweze kutengeneza mazingira mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho nizungumzie dhamira ya Serikali. Serikali imeonesha wawekezaji wengi kwa kushirikisha Mifuko ya Maendeleo ya Jamii; NSSF, PPF, PSPF na mengine, mashirika ambayo tukiweka ubia yana nafasi ya kuweza kusaidia kukuza uchumi. Ni dhamira nzuri ambayo Serikali imeweka; ni vizuri sasa tukawa na uwiano kwenye maeneo yote yasiwe yanaelekezwa kwenye maeneo maalum tu hasa Kanda ya Mashariki. Naomba Serikali iangalie mazingira haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, nizungumzie eneo ambalo watu wengi wamekuja wanafananisha bei za chakula nchini Kenya na bei za kwetu hapa. Niwaambie wananchi tu kwamba, zipo propaganda ambazo zinaenezwa. Tukiangalia uhalisia, bado bei ya sukari kwa nchi yetu ipo chini kuliko bei ya sukari kwenye maeneo ya nchi ambazo ni jirani zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kenya leo hii bei ya sukari ni Sh.3,195/=, Uganda ni Sh.3,550/= mpaka Sh.4,000/=, Burundi ni Sh.3,700/= mpaka Sh.4,000/=. Tanzania bei ya sukari ipo kati ya Sh.2,700/= mpaka Sh.3,000/=. Bado maeneo mengine yote yanayotuzunguka yanahitaji kutoka kwetu kupata bidhaa muhimu kama hiyo. Ni vema sasa watu wakaacha kutumia propaganda ambazo kimsingi wenzetu sasa hivi wanazitumia kwa masuala ya kisiasa. (Makofi)

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.