Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 - Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa

Hon. Yussuf Haji Khamis

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Nungwi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 - Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa

MHE. YUSSUF HAJI KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa neema kubwa ya uhai na uzima. Ninakushukuru wewe kwa kunipatia nafasi na mimi nichangie ingawa kwa muhtasari. Nianze kwa kupongeza utamaduni mzuri wa vijana wetu wanaomaliza vyuo na wale wengine kujiunga na Jeshi la Kujenga Taifa, kwa mujibu wa sheria na wale wa kujitolea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili ni jema sana kwani vijana wetu hupata mafunzo mbalimbali yakiwemo ya ulinzi na usalama na yale ya ujasiriamali, vijana wanaopatiwa mafunzo ya ujasiriamali katika shughuli za kilimo, ufugaji, fundi uashi, fundi uchongaji, na mengine mengi hufanikiwa vizuri wakiwa kambini, wakishaondoka kambini elimu yote waliyopata hupotea kwa sababu vijana hawawezeshwi wanabakia vijiweni tu hawajui la kufanya na elimu waliyopata inapotea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu vijana hawa wakusanywe vikundi mbalimbali, wasajiliwe kisheria, Serikali iwalee na kuwawezesha ili wajiajiri na kuendeleza elimu waliyopata kambini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa vijana wanapata mafunzo ya kijeshi na wana uwezo wa kutumia silaha mbalimbali, Serikali haiwezi kuwaajiri vijana wote, wengi wao hurudi nyumbani wakiwa hawajui la kufanya, vijana wanakuwa rahisi kujiunga na makundi ya uhalifu, hivyo ni hatari kwa Taifa na usalama kwa ujumla wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu vijana hawa wawekwe katika orodha maalum sekta za ulinzi zinapohitaji kuajiri wafanyakazi, kwa mfano, Polisi, Magereza, Zimamoto, Usalama wa Taifa hata kampuni za ulinzi wa binafsi basi wapewe kipaumbele vijana wetu ambao wamepitia Jeshi la Kujenga Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile wabakie kama Jeshi la Akiba hivyo wapangiwe utaratibu kila baada ya muda fulani wanakusanywa kwa kukumbushwa majukumu yao juu ya wajibu wa Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie muingiliano wa kambi za Jeshi na makazi ya raia. Hili ni tatizo ambalo linahitaji kuangaliwa kwa makini sana. Shughuli za kijeshi ni maalum kwa Jeshi mambo mengi ya hatari ambayo yanawahusu wenyewe, mfano maghala ya milipuko mbalimbali ambapo ikitokea bahati ambayo inasababisha maafa makubwa kwa wote. Mfano, mkubwa na hai ni ule wa Gongo la Mboto na Mbagala taharuki kubwa kwa nchi na wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali ifanye juhudi za makusudi, kuepusha kambi zote za Jeshi zenye ghala za milipuko zitengwe na makazi ya raia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie ajira katika Jeshi na vyeti fake. Tatizo hili ni la Taifa zima na katika taasisi mbalimbali, lakini taasisi hii muhimu ina athari kubwa na ni hatari kuwaajiri askari na ukawapa mafunzo yote na siri zote za Jeshi wanazifahamu wamefanya kazi zaidi ya miaka 10 au 15 ndiyo unakuja kugundua vyeti vyao ni fake na kumfukuza kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii siyo vizuri kwa sababu hili ni kundi kubwa sana tunalolikufukuza na tunalifukuza wakiwa na taaluma. Naomba Serikali iangalie kwa umakini suala hili mwanzo wa kuajiri wabaini kasoro zote ambazo hazifai ikiwemo vyeti fake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho niombe usawa wa ajira kati ya pande mbili za Muungano kwa kuwa Muungano wetu ndiyo unaunda taasisi hii muhimu ya ulinzi naomba ajira zake zifanywe kwa uwazi mkubwa tena kwa uwiano mzuri. Hii itajenga heshima na uimara katika Jeshi letu na kupata ushirikiano kwa pande zote na kwa watu wote.