Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Dr. Jasson Samson Rweikiza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi hii kuchangia Bajeti hii ya Wizara ya Maji ambayo kwangu mimi ni moja ya Bajeti muhimu sana kwa nchi hii, ni muhimu sana! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Maji na wasaidizi wake wote katika Wizara kwa kazi nzuri wanayoifanya. Maji ni tatizo kubwa sana kwa nchi yetu. Maeneo mengi sana hayajapata maji safi na salama, hasa hasa majimbo ya vijijini. Ukiwauliza Waheshimiwa Wabunge wote hapa, wa vijijini, wote kilio ni maji. Kilio kikubwa sana ni kuhusu maji safi na salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama walivyoongea waliotangulia, inasikitisha sana kwamba bajeti ya mwaka huu tunayoijadili imepungua kutoka ile ya mwaka jana tunayomalizia. Kutoka bilioni 900 na pointi kwenda bilioni 600, hiki ni kitu cha kusikitisha na kwa kweli si jambo zuri. Serikali iangalie kwa makini hizi fedha zirudishwe katika bajeti ya maji angalau basi ifikie ile ile kama ya mwaka tunaoumalizia huu. Hata kama haikutoka yote lakini ifikie pale ikipatikana, itumike. Bajeti imepanda kutoka trilioni 29 hadi 32, kwa nini ya maji ipungue? Bajeti nzima ya Serikali ikipanda maana yake na za Wizara zote zinapanda, lakini ya maji imepungua, hili sio jambo jema hata kidogo ukizingatia kwamba uko tunakotoka vijijini hali ya maji ni mbaya sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, tulizungumza humu siku nyingi tu kuhusu Wakala wa Maji, tuwe na Mfuko wa Maji. Bahati nzuri ukaanzishwa lakini hauna pesa, kwa hiyo hauwezi kufanya kazi inayotakiwa au inayotegemewa kwa sababu hakuna pesa. Yale aliyoyasema Mheshimiwa Nagu kwamba tulisema itoke sh. 50 iende sh.100 na naiunga mkono. Tuongeze tozo katika mafuta ya diesel na petrol badala ya sh. 50 iwe sh. 100 ili angalau mfuko huu upate fedha ya kutosha kuhudumia maji vijijini. Hili ni jambo kubwa na litasaidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimepata habari kwamba jambo hili lilipofika kwa Waziri wa Fedha akasema kwamba si zuri maana tukiliruhusu litaleta inflation, si kweli! Hakuna inflation kwenye jambo hili. Leo unga umepanda mara nne kutoka bei ya mwaka jana je, ni kwa sababu ya petrol kupanda? Petrol haijapanda. Unga umepanda mara nne kutoka sh. 1,800 mpaka karibu sh. 2500. Kwa hiyo si sababu ya mafuta kupanda ndiyo maana unga umepanda, inflation iko pale pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ukisema watu waendelee kunywa maji machafu vijijini maji ambayo sio safi na salama wataugua matumbo, typhoid, kuharisha na kadhalika utatumia shilingi ngapi kuwatibu hawa? Madawa, vifaa tiba, kulaza hospitalini, gharama yake ni kubwa kuliko hiyo ambayo Mheshimiwa Waziri wa Fedha anasema kwamba itatokana na kupandisha bei ya mafuta kutoka sh. 50 kwenda sh. 100.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo si kweli kwamba kutakuwa na inflation isipokuwa kutokupandisha tozo hii ndiko kunasababisha inflation iwepo kwa sababu watu wanaugua sana. Zahanati na hospitali zinajaa wagonjwa, ambulance zinatumika sana kwa hiyo hali inakuwa ngumu zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna miradi ya maji kwa vijiji 10 kwenye kila Halmashauri, yote imekwama. Miradi hii si ya leo wala si ya jana, ina miaka minne, mitano, nane, imekwama. Pale kwangu kuna kijiji kimoja Ibwera kuna mabomba yaliletwa pale mengi sana, mabomba ya kutosha mradi mzima yako pale kando ya barabara yamekaa miaka minne hadi yamebadilika rangi kutoka nyeusi yamekuwa meupe na yametoboka. Sasa hasara kubwa sana kwa sababu ya kutokuwa na fedha za kumalizia mradi ule. Nashauri sana kwamba bajeti ya maji kwa kweli tuizingatie na tuongeze.

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi ya Kibirizi kule kwangu imekwama, miradi ya Bituntu imekwama, Lubafu, Katoma yote imekwama; Miradi yote vijiji 10 haija-take off haijaweza kukamilika kwa sababu chanzo cha fedha kutoka Benki ya Dunia kimekoma. Lazima tusimamie Mfuko wa Maji upate fedha. Pamoja na kupandisha sh. 50 kwenda sh. 100 kwenye mafuta ya magari diesel na petrol mimi napendekeza yafuatayo yaongezeke.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ni hilo, hiyo tozo mafuta toka sh. 50 kwenda sh. 100 iongezwe. Pia maji haya tunayokunywa mjini haya ya chupa, vijijini hamna maji ya chupa, yako mjini, watu wenye fedha wako mjini; wananunua maji nusu lita sh. 2000. Huku nako tuweke tozo angalau kwa lita sh. 50 kwenye maji ya chupa. Maji ya chupa yawe na tozo sh. 50 iende kwa Wakala wa Maji Vijijiji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bia; wanywaji wa bia wako mjini, nako kuwe na tozo kwa lita moja ya bia angalau sh. 50 iende Mfuko wa Maji Vijijini. Soda; wanywaji soda wako mijini, angalau kwa lita nzima ya soda sh. 20. Pendekezo langu, kiasi hicho kiende kwenye Mfuko wa Maji Vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nipendekeze pia kwamba kwenye bill za maji, mijini kuna maji, miji yote ina maji ya bomba mazuri safi na salama. Kuna bill za maji za kila mwezi au za kila wakati angalau asilimia tano ya ile bill ikatwe iende katika Mfuko wa Maji Vijijini ili nao wapate maji. Wakazi wa mjini ni wa vijijini hawa, wanatoka vijijini wanakuja mjini, walipe angalau asilimia tano ya zile bill ziende kwenye Mfuko wa Maji Vijijini ili Wakala wa Maji Vijijini uwe na uwezo wa kuhudumia miradi ya maji vijijini. Vile vile wakala huu uimarishwe, watafutwe watu wenye uwezo, wajitegemee, watafute fedha ndani na nje ya nchi. Waombe kwa wafadhili, waseme tuna shida vijijini, watu wanaugua matumbo sababu ya maji machafu tutafute fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ilivyo REA, tujifunze REA, REA imefanikiwa baada ya miaka michache, sasa hivi imefanikiwa kwa asilimia 70% nchi nzima. Kwa hiyo wakala uimarishwe uweze kufanya kazi ya kusaidia kupata maji vijijini. Hata hivyo, Serikali na yenyewe kwa kweli kama nilivyosema mwanzoni, kupunguza bajeti ya kutoka milioni 900 kwenda 600 si sahihi. Fedha irudishwe, ibaki angalau 900 hiyo hiyo na itoke; kwa sababu ilikuwa milioni 900 lakini iliyotoka ni asilimia 19, ni kiasi kidogo sana itoke iende kwenye miradi ya maji ili wananchi wa vijijini wapate huduma ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, maji ni muhimu sana, mimi ukiniuliza kati ya maji na umeme nitakwambia maji ni muhimu kuliko umeme. Umeme unaweza ukaona kwa kibatari lakini huwezi kuishi bila maji, kwa hiyo tuyape uzito unaostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa mradi wangu wa maji pale Bukoba Vijijini, mradi wa maji wa miaka mingi, miaka ya 60 na 70 mwanzoni, wa pale Maruku. Nimeshamwambia Mheshimiwa Waziri, mradi huu ni mzuri, ulijengwa na Serikali ya Awamu ya Kwanza, ukafanya kazi nzuri sana, lakini miaka mingi imepita umechakaa. Mradi ule umechakaa yale mabomba tu, matanki yako vizuri na chanzo kiko vizuri. Kama tukipata milioni 300 ama 400 mradi ule unakarabatiwa unakuwa mzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba mradi huu ufufuliwe, upate fedha kidogo ili na wenyewe uweze kuhudumia Kata mbili, Maruku na Kanyangereko…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.