Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue nafasi hii ya awali kabisa kukushukuru kwa dhati kabisa kwa kunipa nafasi ya mwanzo jioni ya leo ili kujadili hoja ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijafika huko, naomba niungane na Waheshimiwa Wabunge waliotangulia na wewe Mheshimiwa Naibu Spika, kuwapa pole wale wote waliofiwa na wanafunzi wa shule ya St. Vincent na wengine wote waliopata ajali kwenye maafa mbalimbali na kufariki. Mwenyezi Mungu alaze roho zao mahali pema peponi. Amina.

Mheshimiwa Naibu Spika, naupongeza sana uongozi wa Bunge la Jamhuri la Muungano wa Tanzania kwa kutambua umuhimu na unyeti wa Sekta ya Maji na kuipangia Sekta hii siku tatu za majadiliano. Naomba Waheshimiwa Wabunge wasirudi nyuma kutumia siku hizi tatu kuijengea hoja ili Mheshimiwa Rais wetu mwema aweze kumtua mama ndoo kichwani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda vile vile kumpongeza Mheshimiwa Rais na Serikali kusikiliza ushauri wa Wabunge wetu. Vile vile kwa kututeulia Waziri Lwenge na Naibu Waziri Kamwelwe ambao ni mahiri sana katika kuongoza Wizara hii pamoja na watendaji wote; na Mungu awape afya njema waweze kusikiliza wanayosema Wabunge na watekeleze. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namwamini sana Mheshimiwa Rais na nampongeza sana. Naisihi Serikali yake kuona kwamba inapokea kilio cha Wabunge kuhusu Bajeti ya Maji kwa sababu maji ni uhai na usafi wa mazingira ni utu wa binadamu. Hivyo sina shaka changamoto nitakazozitoa hapa zitachukuliwa na kufanyiwa kazi kwa kuzitolea uamuzi kwa manufaa ya Taifa letu na wananchi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Bajeti ya 2016/2017 iliyotengwa ilikuwa sh. 939,631,302,771 na kati ya hizo fedha zilizotengwa kwa ajili ya Miradi ya Maendeleo ni sh. 915,193,937,771. Hata hivyo, fedha zilizotolewa kwa Miradi ya Maendeleo mpaka Machi mwaka 2017 ni sh. 181,209,313,609 sawa na asilimia 19 peke yake. Mbaya zaidi Bajeti ya Mwaka huu wa 2017/2018, iliyotengwa ni sh. 623,606,748,052 ambayo ni ndogo ukilinganisha na mwaka uliopita lakini mahitaji ya maji yameongezeka, population nayo imeongezeka, mahitaji ya viwanda yameongezeka na mahitaji ya jumla ya maendeleo yameongezeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana, kwa sababu mwenendo huu unasikitisha na utawasikitisha Watanzania, naomba Serikali bajeti yetu irudi kama ilivyokuwa mwaka jana ili kuona kwamba ndoo hii ambayo mwanamke ameteseka nayo kwa muda mrefu inatua kutoka kwenye kichwa chake. Naomba bajeti hii iongezeke kama ilivyokuwa bajeti ya mwaka jana. Maji ni uhai narudia tena na usafi wa mazingira ni utu. Bila maji hakuna maendeleo, bila maji hakuna uhai, bila maji jamani viwanda hivyo tunavyovisema haviwezi kuwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, ili tuwe na uhakika wa kutekeleza miradi ya maji na maendeleo ya maji ambayo matokeo yake ni maji kupatikana, naomba sana kama tulivyoomba mwaka jana na Kamati yangu imerudia mwaka huu kwamba Mfuko ule wa Maji unaochangiwa sh. 50 kwa kila lita ya diesel na petrol uongezewe sh. 50 ili iwe sh100. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivyo kwa sababu Serikali yenyewe iliahidi kuifanyia kazi. Nina hakika kwa mwaka mmoja hiyo kazi itakuwa imefanyika na naomba mwaka huu tufanye hivyo hasa tukizingatia bajeti yenyewe inayotengwa huwa haitolewi na fedha hizi zitasaidia sana miradi ya maji iende kwa kasi zaidi. Ukiangalia mpaka mwisho wa mwezi Machi, 2017 utaona kwamba hela iliyotolewa ni kidogo sana. Nchi hii inakabiliwa na njaa na inakabiliwa na ukame, hakuna kitu ambacho kitai-rescue au itasaidia nchi hii kama miradi ya umwagiliaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tuone kwamba fedha zinazotengwa kwenye umwagiliaji zitasaidia kuongezeka kwa uhakika wa chakula, uhakika wa kupata mazao ya biashara unaongezeka. Kwa hiyo, naomba Tume ya Umwagiliaji nayo iangaliwe kwa jicho la huruma na kuongezewa fedha ili nchi hii iwe na uhakika wa chakula.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningeshukuru sana kuona kwamba katika bajeti hii, bwawa ambalo nimeliomba kwa miaka saba lingelijitokeza lakini sikuona na nimekuwa nikiomba kila mwaka hata pale ambapo nipo kwenye Sekta hiyo ya Maji, bwawa la Gidahababiel halikuonekana na nasema naipenda sana Serikali, naiamini sana lakini kwa bwawa hili la Gidahababiel nitatoa shilingi kwa sababu watu wa Hanang hawawezi kuelewa hili, wataniona naimba tu halafu Serikali haichukui hatua yoyote.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba mjue kwamba bwawa hili lilikuwepo toka wakati wa ukoloni lakini likapasuka wakati wa el-nino. Mpaka leo hakuna ambaye amelihangaikia bwawa hili. Namuomba Waziri na Watendaji wake waone umuhimu wa bwawa hili. Sisi tuko kwenye bonde la ufa na wilaya ambazo ziko kwenye bonde la ufa zina matatizo makubwa sana ya maji. Hanang ikiwa moja ya Wilaya ya Bonde la Ufa haina maji ya kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile zaidi ya bwawa la Gidahababiel naomba visima vile ambavyo tumeviomba viweze kuchimbwa ili wananchi wa Hanang waweze kupata maji. Mpaka hapa tulipo wananchi wanaopata maji kwenye Wilaya ya Hanang nafikiri ni asilimia 46, na sisi ni wilaya ya mifugo. Wananchi wa Hanang wamehama wilaya ile kutokana na ukame na kwenda wilaya zingine na kutoa adha kwa watu wengine. Naomba sana, wale waliobaki na mifugo, wasihame, wabakie Wilaya ya Hanang kwa kuhakikisha kwamba mabwawa na visima vinachimbwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zaidi ya hapo naomba vile vile katika kuimarisha Sekta ya Maji, tunaomba kuwe na maafisa wa kutosha wa maji, wahandisi wenye uwezo wa kukabiliana na tatizo la ukame. Sasa hivi tuna wahandisi wachache, Wilaya ya Hanang ilikuwa na wahandisi wazuri, wamehamishwa, basi na mimi ningeomba TAMISEMI ione umuhimu wa kuwaleta wahandisi imara ambao watakabiliana na tatizo hilo ambalo ni kubwa katika wilaya yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Waheshimiwa Wabunge waone umuhimu wa kuongeza bajeti ya maji iwe angalau kama ile ya mwaka jana. Naomba Waheshimiwa Wabunge waunge mkono hoja ya kuongeza sh. 50 kwa kila lita ya diesel na petrol ili mfuko wa maji uwe na fedha za kutosha kutekeleza miradi mbalimbali. Tukifanya hivyo, Mheshimiwa Rais wetu atakuwa na uwezo, na ana upendo mkubwa sana na wananchi wake wa kutua ndoo kwenye kichwa cha akinamama ambao ndio wanapata adha kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nishukuru sana kwa nafasi hii na naunga mkono Bajeti hii ya Sekta ya Maji au ya Wizara ya Maji kwa moyo wangu wote, lakini yale niliyoyasema myazingatie na wakati wa kutoa majibu myatolee majibu.