Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Katani Ahmadi Katani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tandahimba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii. Pia nami naomba tu kuwapa maelezo ndugu zangu hao wa upande wa pili kwa maana ya chama tawala, kama Mheshimiwa Kingu na Kaka yangu Mheshimiwa Ulega pale; Serikali hii ya Awamu Tano inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, siyo ukipiga piga maneno ndiyo anakupa Uwaziri, hakupi Uwaziri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wote ukiwaangalia waliopewa Uwaziri, Unaibu Waziri, ni watu makini, wametulia, siyo maneno maneno ya siasa. Sasa kama mnataka Uwaziri kwa namna hiyo, Uwaziri huo haupo na bahati nzuri hakuna reshuffle, nimenusa! Kwa hiyo, mnapokuja hapa, muwe na hoja za msingi za kuishauri Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nami nikubaliane na wewe Mheshimiwa Kingu, sisi Wapinzani tutasema na Serikali ndiyo inatekeleza. Kwa hiyo, unaposema hatuna alternative, sisi hatuko kwenye mamlaka. Kweli hatuna alternative! Tutashauri tu. Nyie wenye mamlaka ndiyo mna wajibu sasa tunayoyashauri kuyafanya au kutoyafanya. Sitarajii tukija kwenye Wizara nyingine mtapiga ngonjera hapa na kwaya zenu za vyama vya siasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niende kwenye michango yangu kuhusu Wizara hii ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji:-

Mheshimiwa Waziri, sisi watu wa Mtwara na Lindi mara nyingi nasema tumesahaulika sana. Nikikukumbusha Mtwara na Lindi tulikuwa na viwanda vya kubangua korosho takribani 11. Pale Newala Mjini tulikuwa na viwanda viwili, Mtama tulikuwa na kiwanda kimoja, Masasi tulikuwa na kiwanda kimoja, Lindi tulikuwa na kiwanda kimoja, lakini viwanda hivi tunavyozungumza, Serikali ya Awamu ya Tatu, ilivibinafsisha viwanda hivi na baadaye ikaja kuviuza viwanda hivi kwa bei chee. Wengine waliouziwa wamekuja kufanya ma-godown viwanda vya kubangua korosho; lakini wengine ni watumishi wa Serikali. Unaona ni dili lilifanywa! Nami naamini Mheshimiwa Waziri yuko makini na Serikali hii ya Awamu ya Tano iko makini, mtakwenda kuvichukua viwanda vile. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda Newala pale, vile viwanda viwili, bei iliyouziwa haifiki shilingi milioni 300, viwanda viwili! Hebu tukimaliza Bunge hili Mheshimiwa Waziri aende ufuatilie haya ninalomwambia. Sasa wanataka tuwe na Tanzania ya viwanda, viwanda ambavyo Mwalimu Nyerere alifanya kazi kubwa; akaona Kusini kuna fursa ya kuweka viwanda vya kubangua korosho kwa ajili ya kuongeza thamani. Leo korosho tunai-export mpaka inatoa ajira. Wahindi wanakuja kununua korosho hapa, Vietnam wanakuja kuchukua korosho hapa, tuna-export ajira zinakwenda India pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda India, wale Wahindi wanaofanya kazi ya kubangua korosho kazi ambazo Wamakonde wanaweza. Bahati nzuri viwanda vya kubangua korosho havihitaji mitaji mikubwa kama watu wanavyofikiri. Nami nampongeza sana Mheshimiwa Waziri, watu wanakuwa hawamwelewi, lakini mimi namwelewa kweli kweli!

Mheshimiwa Naibu Spika, juzi nilimtumia memo moja nikawa naulizia suala la kiwanda cha sabuni, alinipa alternative. Kweli nilipokwenda Kibaha pale, ile thamani aliyoniambia nimeikuta iko hivyo hivyo, shilingi milioni nane. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna watu walitaka kuleta kiwanda cha kubangua korosho chenye thamani ya shilingi bilioni 37, hata India hakuna kiwanda cha namna hiyo. Sasa fursa ya viwanda vile ambavyo vimechukuliwa na Serikali ya Awamu ya Tatu kwa bahati mbaya, najua kwa bahari mbaya; kuna watu wapiga dili na kuna watu wanakuja kwa ajili ya kazi; nami naamini Mheshimiwa Waziri umekuja kwa ajili ya kazi. Twende kule maeneo ya Kusini uone viwanda vile vilitolewaje na namna gani tunaweza kuvirudisha ili sisi wakulima wa korosho sasa tunufaike na viwanda vile. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukitoka kwangu Kitama, Kijiji nilichozaliwa ukaenda Kijiji jirani cha Miuta, palikuwa na kiwanda pale cha NDC; kile kiwanda kimekufa. Ukija Kitama ambapo mimi nipo, pana kiwanda cha kubangua korosho pale, kile kiwanda kinahitaji mtaji mdogo wa kuongezewa. Nasi kwenye korosho umeona taarifa; kwa kupitia Export Levy tumekusanya kwa taarifa ya Serikali mpaka mwezi wa Pili mwaka huu zaidi ya shilingi bilioni 980.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa taarifa ya sasa, tumekusanya zaidi ya shilingi trilioni moja kwenye korosho. Sasa pesa zile za Export Levy kwa sababu zinakaa tu, uangaliwe utaratibu aidha, hata kwa kupitia SIDO, watu wakopeshwe pesa wajenge viwanda vidogo kule.

Mheshimiwa Waziri, Mtwara Mjini pale eneo lile la Mikindani kulikuwa na viwanda pale. Zamani wakati mimi nakua, palikuwa na Kiwanda cha Mashua, Mikindani pale. Vile vile palikuwa na kiwanda cha Coca Cola Mikindani pale. Viwanda vie vimepotea na wala hatujui vimepoteaje.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa wakati Mheshimiwa Waziri anafanya majumuisho, nataka ajaribu kunipa maelezo, vile viwanda vimetekwa, vimekwenda wapi? Maana havipo! Ilikuwa fursa kubwa kwa watu wa Mtwara- Mikindani na maeneo ya Uwanda wa Pwani kwenda kununua vifaa vya uvuvi pale kwa sababu kulikuwa na viwanda pale. Leo tunapozungumza, hakuna kinachoendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshauri Mheshimiwa Waziri, kwa nafasi yake, najua anaweza; leo wafanyabiashara wakubwa, wawekezaji wakubwa kama Bakhresa anatengeneza juice. Niwaambie Waheshimiwa Wabunge, juice bora kabisa yenye Vitamin C ambayo haina shaka kabisa, inatokana na Mabibo ya Korosho. Sasa Mheshimiwa Waziri amshauri mwekezaji yule mkubwa aje Tandahimba pale na Halmashauri inaweza ikampa eneo tu la kutosha aweke kiwanda pale atengeneze juice ya matunda na Waheshimiwa Wabunge wapate vitamin ya kutosha hapa kwa ajili ya mustakabali wa afya zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, japo kuna wakati walikuja wawekezaji kadhaa na nimwombe Mheshimiwa Waziri ili alifuatilie, ajaribu kuwasiliana na Profesa Aba Mpesha aliyepo Marekani. Wapo wawekezaji wazuri na najua ana mawasiliano nao mazuri, wako tayari kuja kujenga viwanda vya kubangua korosho Tandahimba, lakini kuna watu wanaleta chenga pale katikati.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa namwamini Mheshimiwa Waziri, ni mtu muhimu sana na mara zote huwa nawaambia, mkiwa mnafanya mambo mazuri Watanzania wakayaona, watawapongezeni. Kwa mfano, Kusini ambako viwanda hatuna, barabara hakuna, kila kitu hatuna; umeme shida, maji balaa! Mtakaa mkitegemea CCM mtachaguliwa kwa matatizo haya? Hebu mje mmalize haya matatizo kwanza; myamalize haya mambo! Msije mkafanya Kusini kama scraper.

Mheshimiwa Naibu Spika, wazungumzaji wamezungumza hapa, wakati tunazungumza hata suala la reli ile ya kutoka Liganga, ni stori tu. Stori hizi siyo kwamba zimeanza kwenye Serikali yenu. Nimesoma bajeti kipindi cha Awamu ya Nne, kuanzia 2010 historia hiyo ipo kwenye makabrasha; 2011/2012 ipo kweye makabrasha; 2012/2013 ipo kwenye makabrasha; 2014/2015 kwenye makabrasha; mwaka jana (2016/2017) tumepiga makabrasha kwenye Wizara hii; mwaka huu, tumeizungumza tena. Ile ilikuwa inatoa fursa kwa watu wa Kusini kule kote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Bandari ya Mtwara ingefunguka kwa kiwango kikubwa. Mikoa hii ya Kusini; Mbeya, Ruvuma, Njombe, watu wangefanya kazi na ajira hizi ambazo leo Tanzania ambako kuna bahati mbaya kwamba watu wake hawaajiriwi, eti kwa sababu hawawezi Kiingereza, lakini ukienda Dangote pana Wachina sijui 700 na hawajui Kiingereza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ya viwanda, kwanza huu utaratibu huu wa Kiingereza, wakija Wachina wasiojua Kiingereza wanaajiriwa na Kiswahili hawajui, wanaajiriwa; Watanzania wenyewe wanakosa fursa kwa vitu vya ajabu ajabu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba sana, mimi namwamini sana Mheshimiwa Mwijage, nakuamini sana. Namwomba sana aone mambo haya anayafanyia kazi kwa uzuri ili at least watu wa Tandahimba na wenyewe wakipata kiwanda cha juice pale, wakipata viwanda vidogo vile ambavyo Profesa Aba Mpesha, tayari ana wawekezaji mkononi, watu wale watapandisha thamani ya korosho zao, watapandisha thamani ya mabibo, yale ambayo badala ya kuanika tukapika gongo, tutakunywa juice watu mkapata vitamin C na mambo yakaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii.