Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Anthony Calist Komu

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. ANTONY C. KOMU: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nianze mchango wangu kwa kueleza masikitiko yangu juu ya kauli ya Mheshimiwa Elibariki Kingu, kijana mdogo ambaye kwa kweli niliamini kwamba angekuwa ni mtu makini, mtu ambaye anasema ukweli na mtu ambaye angekuwa analiongezea hili Bunge hadhi (value) kuliko kuzungumza vitu ambavyo kimsingi mtu yeyote anayesikiliza, hataelewa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wewe umetoa sifa, leo umetoa complement kwamba katika hotuba ambazo zimeshatolewa hapa ndani ya Bunge kutoka upande huu, hii ni moja ya hotuba ambazo ni role model. Sasa anatokea mtu mmoja anasimama na anasema ukurasa wa kwanza mpaka wa mwisho hakuna kitu chochote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza huu ni uongo. Maneno kama haya yakivumiliwa ndani ya Bunge hili, maana yake hata hadhi ya hili Bunge na Kiti chako wewe mwenyewe vitakwenda kuathirika.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Nilichokuwa nataka kusema ni kwamba waliosoma hiki kitabu kwa sababu wanacho, kina ushauri mwingi sana. Mtu akikushauri, maana yake anakupa alternative. Sasa huyu Mheshimiwa Kingu anavyosema hakuna ushauri wowote, ni malalamiko na hakuna mkakati wowote; Mheshimiwa Lwakatare amerejea hapa maeneo ambayo yanaonesha mkakati ambao unaweza ukatumika kama mbadala.

Kwa hiyo, naomba iingie kwenye record kwamba Mheshimiwa Kingu amesema uongo na amejaribu kupotosha na kwa kweli kitu alichofanya kinafedhehesha hata Bunge lenyewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na naamini kwamba utakuwa umetunza muda wangu, kwa sababu kwa kweli umetumika ndivyo sivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kusema na hii ni kauli ambayo nairudia mara kwa mara kwamba ni vizuri Serikali ikaweka vipaumbele vichache. Tukiwa na vipaumbele vichache, maana yake tunaweza kujipima na kujua kwamba tunatoka wapi na kwenda wapi.

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wengi hapa wamezungumza habari ya Mchuchuma na Liganga. Kama tungekuwa tunajiwekea vipaumbele na tukaamua kujua kwamba ni kipi ambacho tunataka kukifanya na kwa wakati gani, haya malalamiko ambayo yameelezwa hapa yasingekuwa yamejitokeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo napenda kulishauri kwa nguvu zote ni suala la Serikali kufanya biashara, kujiingiza katika shughuli za kiuchumi moja kwa moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda Waheshimiwa Wabunge tuwe kitu kimoja na tuishauri Serikali kwa nguvu zetu zote kama Bunge kwamba suala hili ni jambo ambalo huko siku za nyuma lilishafanyiwa uamuzi na baada ya kufanyiwa uamuzi ingekuwa ni busara kama tunataka kutoka hapa tukapata muafaka sasa wa Kitaifa kwamba sasa tunaondoka kwenye utaratibu huu, kwenye utamaduni huu, kwenye sera hii tukaenda kwenye huo utaratibu mwingine wa Serikali kufanya biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakumbuka mchango wa Mheshimiwa Shabiby ambaye alizungumza hapa from practical point of view kwamba yeye ni mfanyabiashara na akashauri kwa nguvu zake zote kwamba hata hii biashara ya ndege ambayo Serikali imeamua kuingia, kama tunataka ifanikiwe, Serikali ikae mbali na hiyo management ambayo imewekwa kwa ajili ya kuendesha hiyo biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ukichukua mifano kama hiyo, utaona kwamba ni vigumu na haitawezekana kabisa kwamba Serikali ikafanya biashara. Tunao mfano mmoja ambao ni mdogo. Juzi juzi hapa; na bahati nzuri wewe mwenyewe ndio ulihusika kikamilifu, mlikabidhi Serikali shilingi bilioni sita kwa ajili ya kwenda kutengeneza madawati. Wakaamua kutengeneza madawati yale kwa kutumia vyombo vyake vya Ulinzi na Usalama (SUMA JKT na Magereza). Mpaka tunavyoongea hapa siku ya leo, shilingi bilioni sita madawati hayajaweza kukabidhiwa kila mahali ambapo yalipaswa kupelekwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi mwenyewe katika Halmashauri yangu ya Moshi hatujapewa hayo madawati kwa sababu tuliambiwa tukachukue hayo madawati kule Nachingwea na watu wengine wengi bado wanadai hayo madawati. Katika utaratibu wa namna hii, unakuta kwamba malengo ambayo yamepangwa hayawezi kufikiwa; hakuna tija wala ufanisi. Huo uamuzi wa Serikali ambao ulikuwa sahihi sana wa kutumia fedha zile wa kwenda kutatua tatizo la madawati, maana yake haikuwezekana. Kwa sababu kama kweli kulikuwa na kero ya madawati, mpaka leo miezi kadhaa hayajafika sasa tunafanya kitu gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia jambo lingine ambalo ni la msingi sana kwenye masuala haya ya viwanda na biashara, hili suala la Serikali kushindana na wadau wa biashara katika nchi; na lenyewe linayumbisha sana uchumi wetu. Kwa mfano, sasa hivi Serikali imeamua kwamba fedha zake zote zitoke kwenye benki za biashara na benki binafsi ziende kukaa Benki Kuu kwa sababu tu wanafikiri kwamba zile fedha za Mashirika au za Serikali zinatumiwa na benki zetu kwa ajili ya biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, nini jukumu la Serikali katika kufanya nchi istawi kiuchumi? Mahali pengine Serikali inatoa hata ruzuku kwa ajili ya benki zisianguke, zifanye vizuri; lakini kwetu pesa ziko pale, hazina kitu chochote ambacho kinainyima Serikali, Serikali inaamua tu kuwa na wivu fulani, kuwa na msimamo ambao ni hasi kwa wafanyabiashara wake na benki zake, zinakwenda kuwekwa Benki Kuu, zinakaa pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukijiuliza, hivi huo uchumi ni uchumi gani ambao unakufanya wewe uone wivu dhidi ya benki zako kufanya vizuri? Kwa sababu benki zikifanya vizuri, maana yake hiyo ni ajira inayotokana na watu wanaofanya kazi ndani ya benki. Benki zikifanya vizuri, zitakopesha watu ambao watakwenda kufanya biashara. (Makofi)

Mheshimia Naibu Spika, hata haya aliyouliza Mheshimiwa Lwakatare pesa ziko wapi, niseme pesa ziko Benki Kuu kwa sababu zimeondoka kwenye mzunguko wa kawaida. Kwa hiyo, ni vizuri Serikali ikaelewa kwamba inao wajibu wa kujenga mazingira rafiki na wezeshi kwa ajili ya watu na sekta binafsi kufanya biashara kama hizo Benki na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna maamuzi mengi ya Serikali ambayo yanafanywa bila kujali kwamba biashara au uchumi katika nchi utaathirika kwa kiasi gani. Haya nimeyaeleza kwenye hotuba yangu, lakini napenda nitie msisitizo kwenye jambo hili kwa sababu ni jambo ambalo linaathiri sana biashara na mara nyingi ukikutana na wafanyabiashara, ukikutana na wenye viwanda na wawekezaji, malalamiko yao ni hayo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, unajua jinsi ambavyo Serikali inakuwa au wanakuwa wakali inapokuwa kwamba wanadai labda fedha kwa ajili ya ushuru, wanadai fedha kwa ajili ya kodiā€¦

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Komu. Muda wako umekwisha.