Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwenye Wizara hii ya Viwanda, Uwekezaji na Biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa juhudi ambazo zimeanza kuonekana za kufufua viwanda na hasa kwa kweli viwanda vya korosho. Jimboni kwangu kuna kiwanda wamefufua, lakini na maeneo mengine tumeanza kuona juhudi hizi zinakwenda na nadhani hatua walizochukua zinakwenda vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwamba naunga mkono, vile viwanda vilivyobinafsishwa na havikufanya vizuri, kwa sababu mikataba ipo na wengi hawakufanya sawasawa na mikataba na ukisoma ripoti zote zinaonyesha kwamba, wengi walipobinafsishiwa viwanda hivyo, wakavitumia wakaenda wakakopa na pesa zile zikaenda maeneo mengine. Mheshimiwa Mwijage aache upole, achukue hatua tuwadhibiti watu waliofanya kinyume na tulichokubaliana. Pamoja na kazi nzuri ambayo mmeanza kufanya, ningeshauri maeneo machache yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza Mheshimiwa Mwijage tuna shida kubwa ya tafsiri tuliyonayo juu ya nini tunakiita ni kiwanda. Ukiangalia maeneo mengi ukitaja idadi ya viwanda ambavyo vimeanza kujengwa watu wanaangaliana usoni, kwa nini? Kwa sababu tunalo tatizo la tafsiri ya pamoja ya kukubaliana hivi kiwanda hasa ni nini? Ni lile dubwashika kubwa au hata nikiwa na karanda kangu bado tunakaita viwanda, ndiyo maana Mheshimiwa Waziri akitoa idadi ya viwanda hapa aasema elfu tano, elfu kumi, elfu ngapi, wakati mwingine watu wanaangaliana wanapata mashaka na tunachokisema.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nadhani Mheshimiwa Mwijage kwenye hitimisho lake hebu tuzungumze tunaposema viwanda tunamaanisha nini, tukikubaliana hapa, tutakwenda vizuri. Niliwahi kukutana na wanahabari nikiwahamasisha wazungumze juu ya viwanda. Wakaniambia lakini Nape hata ninyi wenyewe hamna tafsiri moja, sasa tukizungumza tunazungumza nini hasa. Nadhani hili la kwanza kubwa litatuweka mahali pazuri, tunaposema kiwanda tunamaanisha nini, tukikubaliana hapa sasa tutasonga mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, Mheshimiwa Mwijage viwanda ni ukombozi na hasa kwa Mikoa ya Lindi na Mtwara kwa sababu bado maskini sana. Ukombozi wowote una vita na una vita hasa kwa wale ambao wanafaidika na mfumo wa kutokuwepo kwa viwanda. Hapa nitatoa mfano, tumekuwa tukizungumza juu ya ujenzi wa Kiwanda cha Mbolea Lindi, pale Kilwa. Taarifa tulizonazo, Mataifa makubwa yenye interest na mbolea katika nchi hii yanapambana kuhakikisha kiwanda hicho hakijengwi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika jambo ambalo hatutakubaliana nalo Mheshimiwa Mwijage ni pamoja na kuruhusu vita hii iendelee kutuumiza; Wanakusini wanapigana kwa maslahi yao na kama Serikali mtayumba kwenye hili, Wanakusini hatutakubali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tulishalizungumza, mlishakubaliana, mwekezaji alishapatikana na utaratibu uko wazi, sasa vita hii ya wakubwa isituumize, wakapiganie nje ya Lindi lakini tunakitaka kiwanda cha mbolea Lindi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu nyingine, moja ya jambo linalopigiwa kelele na wawekezaji ni vitu vinavyoitwa vivutio (incentives), vinavyowavutia kuja kuwekeza kwenye nchi yetu. Mjadala katika nini vitumike kama vivutio vya kuwekeza inachukua muda mrefu sana na hata katika ranking za urahisi wa uwekezaji katika nchi yetu, katika jambo linaloturudisha nyuma ni pamoja na mjadala juu ya vivutio.

Mheshimiwa Naibu Spika, unajua mjadala uliokuwepo juu ya bomba la mafuta, mjadala juu ya viwanda vya uunganishaji wa vipuri mbalimbali katika nchi yetu, suala la vivutio nadhani ni tatizo kubwa. Sasa umefika wakati Mheshimiwa Waziri na Serikali ya Awamu ya Tano fikirieni kutengeneza vivutio ambavyo tunakubaliana navyo, kwamba wanaokwenda kwenye mjadala waende wakiwa wanajua, huu ndio msimamo wa nchi katika kutoa vivutio katika uwekezaji ili tupunguze muda wa mjadala; kwa sababu wapo wawekezaji wengi wana pesa zao; anakuja akiona mjadala unachukua muda mrefu anaondoka, kwa sababu hatujaweka vipaumbele katika vivutio tunavyotaka kuviweka.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo,ushauri wangu kwa Serikali; umefika wakati kaeni kubalianeni; hivi ndivyo vivutio tutakavyovitoa, vikitokea vya ziada hivyo ndivyo viingie kwenye mjadala, vinginevyo tutashindwa kushindana. Kama mtu anakwenda Rwanda anatumia masaa machache anapata mkataba yuko tayari kuwekeza, halafu akija kwetu anachukua miaka miwili au mitatu, watatukimbia; na wakitukimbia maana yake nchi kinachozungumzwa hakitatekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala la mchango wa sekta binafsi na kuna watu wamezungumza hapa. Nataka kushauri Serikali yangu, hebu tusiingie kwenye mtego wa kuiingiza Serikali kwenye uwekezaji wa viwanda, tuwaachie sekta binafsi. Kazi yetu iwe ni kuwatengenezea mazingira mazuri ya kuwekeza. Dunia ya leo tukitaka kwenda wenyewe tutakwama, lakini tukiwatengenezea mazingira mazuri inawezekana, mchango wao ni mkubwa, tutengeneze mazingira ikiwemo vivutio, lakini pia waone kwamba hili ni eneo sahihi la kuwekeza. Mtaji wa mwanzo wa amani na utulivu tunao, lakini haya maeneo mengine lazima tuyawekee kipaumbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, ni suala kubwa sana la kuhusisha maendeleo ya viwanda na maendeleo ya watu, ni suala la msingi sana. Tusipolihusisha tutawaacha watu wetu nyuma na haya maendeleo hayatakuwa na maana kabisa, kwa hiyo, ni lazima tuhusishe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo moja la kuhusisha ambalo nadhani tushauriane, Serikali, Wizara ya Viwanda na Biashara, Wizara ya Elimu pengine na TAMISEMI kupitia VETA, tuangalie tunawatengeneza akina nani kwenda kufanya kazi kwenye hivi viwanda? Vinginevyo tutajikuta tunaanzisha viwanda na mwisho wa siku wanaokuja kufanya kazi si vijana wetu hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo tuna mtaala wa VETA ambapo nchi nzima mtaala ni huo mmoja, lakini mazingira yanatofautiana. Ukienda Lindi na Mtwara mahitaji yetu ni kuwatengeneza vijana wetu wakafanye kazi kwenye mafuta na gesi, lakini mtaala wa kwao ni sawasawa na mtaala wa Bukoba, mazingira ni tofauti. Wa Bukoba wafundishwe kuchonga mtumbwi na kuvua samaki, lakini wa Mtwara na Lindi wafundishwe namna atakavyofanya kazi kwenye mafuta na gesi. Sasa nadhani tufikirie namna ya kutengeneza mtaala kwa mujibu wa mahitaji ya ukanda na shughuli za kiuchumi zilizoko kwenye eneo husika badala ya kuendelea na utaratibu wa sasa hivi wa mtaala mmoja kwa nchi nzima.

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani tukienda hivi maendeleo ya viwanda pamoja na kuongeza thamani ya mazao yetu, lakini pia utakidhi haja ya wale wanaokwenda kufanya kazi. Ukienda leo pale Mtwara kwenye utafiti wa gesi na mafuta pana shida, mpaka walinzi wanaajiriwa kutoka Kenya, wanaajiriwa kutoka Uganda. Hivi hatuna vijana wetu pale tukawafundisha Kiingereza kidogo na kuwafundisha discipline ya kufanya kazi pale?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nadhani VETA inaweza kuboreshwa zaidi kutoka hapa ilipo ikawaandaa vijana wetu wakakidhi haja ya soko la huko tunakokwenda. Tukifanya hivyo tunaambatanisha maendeleo ya viwanda pamoja na maendeleo ya wananchi wetu na tukifanya hivyo naamini hatutakuwa na matatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, najua iko nia njema ya Rais wangu, najua iko nia njema ya Serikali ya Awamu ya Tano, lakini hebu tuhusianishe basi haya tunayoyafanya yapate tafsiri sahihi, tuweke vigezo sahihi, vile vile tuyahusianishe na maendeleo ya watu wetu. Tukifanya hivi mambo yetu yatakwenda vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, namuunga mkono Mheshimiwa Waziri kwenye bajeti yake na kwa kweli mambo yake nadhani yatakwenda vizuri.