Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na mimi naanza moja kwa moja kwa kuunga mkono hoja hii, na kipekee namshukuru sana Waziri wa Fedha pamoja na Naibu wake, Makatibu Wakuu na uongozi mzima wa wizara kwa kuja au kwa kuandaa bajeti hii nzuri sana ya Serikali kwa mwaka 2017/2018. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na mimi niungane na wasemaji waliotangulia kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa namna ambavyo amekuwa akisimamia rasilimali zetu, maliasili na madini katika kuhakikisha kwamba zinatumika kwa manufaa ya taifa letu. Waheshimiwa Wabunge kama tutakumbuka mwaka 2015 wakati Mheshimiwa Rais alipokuwa akizindua Bunge hili, alieleza vipaumbele kadhaa na nipende tu kupongeza sana bajeti hii ya Serikali kwa kiasi kikubwa imeweza kutimiza vipaumbele vile au imeanza kufanyia kazi vipaumbele hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, alieleza namna ambavyo atahakikisha kwamba anakuza uchumi, alielezea namna ambavyo ataziba mianya ya mapato ya Serikali; na kwa kweli nipongeze sana Wizara ya Fedha, tumeweza kuona e- government payment system namna ilivyoanza, tumejionea mifumo ya kielektroniki katika Serikali za Mitaa, lakini pia tumejionea namna TRA pamoja na ZRB namna ambavyo wameboresha mifumo yao ya malipo. Ni kwa kufanya hivi ndipo tutapata bakaa ya kuweza kupata fedha na kuboresha huduma nyingine za Kiserikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia aliahidi kupunguza matumizi yasiyo ya lazima ya Serikali. Tumeweza kujionea namna ambavyo hata sasa safari za nje ya nchi ni zile tu ambazo ni za lazima. Hata kwa wale ambao wanaenda, ukiangalia ujumbe wao (delegation) kidogo kwa kiasi kikubwa imepungua na kwa kweli imekuwa ikileta tija na kutusaidia kupata fedha kwa ajili ya huduma zingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zaidi tumeona namna utawala bora unavyoendelea kudumishwa, tumeona namna ambavyo mapambano dhidi ya rushwa yanavyoendelea, na mmeona katika wiki kadhaa kesi zinazidi kwenda mahakamani. Nipende tu kusema kwamba kupitia TAKUKURU na Serikali nzima kwa ujumla hatutafumbia macho mtu yeyote ambaye atataka kuchezea rasilimali, ambaye atafanya ubadhirifu wa mali za umma akifikiri tu kwamba ataweza kuchezea kwa kuwa Serikali haipo macho.

Mheshimiwa Spika, nipende tu kusema kwamba TAKUKURU iko macho, itaendelea kufanya hivyo na tutaendelea kuhakikisha kwamba tunafuatilia miradi yote ya maendeleo na tunaomba tu Waheshimiwa Wabunge na wananchi watupatie ushirikiano ili kuhakikisha kwamba haya yanafanyika.

Mheshimiwa Spika, moja ya vipaumbele vingine ilikuwa ni kufanya mabadiliko makubwa ya utendaji Serikalini. Wote mtashuhudia sasa hivi mkienda katika taasisi mbalimbali za umma kwa kiasi kikubwa huduma imeboreka sana. Tunaomba Waheshimiwa Wabunge na wananchi muendelee kutupatia ushirikiano, itakapotokea unaenda kupata huduma unaombwa rushwa tafadhali toa ripoti katika namba 113 ili tuweze kuchukua hatua dhidi ya yeyote ambaye anataka kukupatia haki yako mpaka uwe umefanya malipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niombe sasa nielekee katika hoja chache ambazo zilijitokeza kuhusiana na ofisi yangu au masuala ya kiutumishi. Ilikuwepo hoja kwamba katika bajeti hii ya mwaka 2017/2018 nyongeza ya mshahara haijaonekana katika bajeti. Nipende tu kusema kwamba ukiangalia bajeti ya mwaka 2016/2017 ilikuwa ni ya shilingi trilioni 6.6; bajeti ya mwaka huu 2017/2018 ni shilingi trilioni 7.205, kuna nyongeza hapo ya zaidi ya shilingi bilioni 605 ambayo ni sawa na asilimia 9.18. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, fedha hizi tumepanga sasa zitatumika kwa ajili ya kulipia mishahara ya watumishi mbalimbali, lakini pia fedha hizi zitatumika katika kulipia malimbikizo ya maslahi mbalimbali ambayo watumishi wanadai, pia tutatumia katika ajira mpya. Kama nilivyoeleza tumepanga kuajiri watumishi 52,436. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wapo ambao wamekuwa wakisema kwamba uhakiki umekuwa ukiendelea muda mrefu. Nipende tu kusema kwamba kama una Serikali makini ni lazima pia uweze kufanya uhakiki ili kujiridhisha kwamba unalipa watumishi wale tu ambao kweli ndio umewakusudia; tumeondoa zaidi ya watumishi hewa 19,708. Endapo watumishi hawa wangeendelea kuwepo katika orodha ya malipo ya Serikali au payroll, kila mwezi Serikali ingepoteza takribani shilingi bilioni 20, si fedha ndogo. Sasa hivi tunatumia shilingi bilioni 18.8 kila mwezi kulipia elimu katika shule za msingi na sekondari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa wewe ujiulize kama mafanikio yote haya yanapatikana kwa fedha hizo halafu upande mwingine kulikuwa kuna zaidi ya shilingi bilioni 20 kila mwezi zilikuwa zinaondoka kwa ajili ya watumishi hewa. Kwa hiyo, nipende tu kusema kwamba watasema tunaendelea na uhakiki, tunaonekana tumekuwa maarufu kwa uhakiki, naomba bora niwe hivyo na nitaendelea kuwa Waziri wa uhakiki ikibidi ili kuhakikisha kwamba hakuna hata fedha moja ya Serikali ambayo inapotea; na kwa kufanya hivi ndipo tunapata walau ahueni ya fedha nyingine ya kuweza kuboresha maslahi ya watumishi pamoja na huduma nyingine mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wapo ambao wanasema ajira hazijatoka, sio kweli. Tumeshaajiri ajira zaidi ya 9,000. Katika vyombo vyetu vya ulinzi na usalama watumishi mbalimbali wameajiriwa, wapo ambao walisema hawajaona ajira katika vyombo vya ulinzi na usalama; wameshaajiriwa wote waliotoka katika mafunzo ya depo wameshaajiriwa, labda aseme kama kuna wengine ambao wako katika mafunzo ambao bado hawajaajiriwa.

Mheshimiwa Spika, tumeshaajiri walimu wa sayansi na hesabu, wataalam wa maabara na tutaendelea kufanya hivyo kwa kadri uwezo wa Serikali unavyoruhusu. Niwatoe tu hofu wahitimu wetu kwamba ajira wakati wowote zitaendelea kutolewa kwa awamu kwa mujibu wa sekta husika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, labda niseme tu kwamba katika sekta ya elimu zaidi ya watumishi 16,516 tutawaajiri mwaka huu, lakini pia katika sekta ya afya zaidi ya watumishi 14,102 tutaweza pia kuwaajiri na hii pia ni pamoja na kuongeza na nyongeza nyingine ya ku-replace wale ambao waliondoka kwa mujibu wa zoezi la uhakiki wa vyeti fake ambalo lilikuwa likiendeshwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja nyingine, nadhani ni ya Mheshimiwa Nsanzugwanko; kwamba Serikali baada ya kumaliza uhakiki wa vyeti feki ifanye performance audit. Nipende tu kumueleza kwamba ufanisi katika utoaji wa huduma unapimwa kwa kutumia vigezo vingi ikiwemo uwezo wa kutumia rasilimali zilizopo, usahihi na uadilifu lakini vile vile kuangalia viwango na ubora wa huduma hiyo inayotolewa kwa mujibu wa fedha inayotolewa...

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: ...nipende tu kumwambia mifumo ipo, tunayo mifumo ya tathmini ya uwazi kabisa ya OPRAS, na kuanzia mwezi Julai, tutaanza kupima utendaji wa Taasisi zote za umma, tutawaanzishia performance contract watendaji wote wa taasisi za umma katika kuhakikisha kwamba wanaenenda kwa mujibu wa viashiria na kuona kwamba kunakuwa na utendaji mzuri.

Mheshimiwa Spika, nikushukuru na niseme na mimi kwa ufupi naunga mkono hoja.