Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa ya kuchangia hoja hii iliyoko mbele yetu. Kwanza niunge mkono hoja na niwapongeze Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri wake kwa kazi nzuri wanayoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vitu vingi ambavyo Waheshimiwa Wabunge wanavisema ndiyo vitu ambavyo Profesa na Injinia huyu wanahangaikia kila leo, katika kazi waliyotumwa na Mheshimiwa Rais kuhakikisha kwamba wanarekebisha baadhi ya maeneo ambayo kama Watanzania tunayaona yakiwa na kasolo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wangu baadhi ya mambo yaliyogusa Wizara yangu niongelee moja, Mheshimiwa Mahawe pamoja na Wabunge wengine waliongelea jambo lililohusu masuala ya usafiri hasa wakigusia usafiri wa wanafunzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kama nilivyosema wakati wa bajeti yangu nitoe pole kwa familia pamoja na Watanzania wote tuliokubwa na tatizo hilo. Sasa nitoe maelekezo kwamba baada ya jambo hili kutokea, askari wetu wasifanye kwa zimamoto jambo hili.

Katika wiki mbili hizi ambazo shule nyingi zinaelekea likizo, wawaandalie vitu vinavyotakiwa kuwa kwenye magari yanayobeba wanafunzi. Wawaandalie masharti yanayotakiwa kuwa kwenye magari na shule zitakapofungwa wamiliki wote wa magari hayo, pamoja na wamiliki wa shule wanaotumia magari hayo waweze kufanyia kazi mambo hayo na kabla ya shule kufunguliwa watoe taarifa ni namna gani wametekeleza masuala hayo ambayo yatakuwa yameainishwa yanayohitajika katika shule hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukishughulikia tunayemkamata peke yake, yule ambaye tutakuwa hatujaweza kumkamata ataendelea kuwa na gari bovu na tutamtambua siku ambapo litakuwa Limeshaleta matatizo, hiki ndicho kilichojitokeza katika siku hizi zilizopita.

Kwa hiyo, Idara zinazoshughulikia masuala ya usafiri likiwepo hili la mashuleni pamoja na maeneo mengine yanayobeba abiria, wabainishe vitu ambavyo vinatakiwa, wawapatie wamiliki na kwa shule wiki hizi mbili, zinatosha kuwaandalia masharti hayo. Kipindi cha likizo kinatosha kwa wamiliki wa magari pamoja na wamiliki wa shule kutimiza masharti hayo, lakini shule zitakapofunguliwa watoe taarifa, ukaguzi ufanyike na masharti kwa wanafunzi wanaosafiri mwendo mrefu lazima magari yale yawe yamepitishwa kwamba yanaweza yakabeba abiria kama ambavyo tunafanya kwa mabasi. Tusikamate moja moja kwa rejareja halafu tukaacha wale ambao hatukuweza kuwaona ama kuwakamata na tukaacha kuwapa masharti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili lililosemwa kwa kirefu ni hili jambo la mimba kwa wanafunzi/mimba za utotoni. Waheshimiwa Wabunge, niwaombe kwenye jambo hili tuelewane vizuri na niwaombe tusikilizane vizuri. Moja sisi ni viongozi, na siyo tu viongozi, tena watunga sheria, ni lazima jambo hili tulibebe kwa upana wake, tusilibebe kwa kipengele kimoja kimoja ambapo tutajikuta tunatunga sheria zinazokinzana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, siku tulipokuwa tunapitisha bajeti ya Wizara ya Katiba na Sheria, mjadala mzito ilikuwa kuhakikisha tunatimiza sheria inayotaka ndoa zifanyike baada ya miaka 18 na kuendelea. Bunge hili na Wabunge hawa pia, Bunge ni Taasisi tulitunga sheria inayosema mtu akibaka ama akampa mimba mwanafunzi anatakiwa kufungwa miaka isiyopungua 30. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo tukisema hilo ni kosa, lakini leo hii tukichukua kipengele kimoja kimoja tena kwa kutumia kigezo cha huruma, tukahalalisha makosa hayo kuna sheria zingine tutashindwa kuzitunga na tutashindwa kuzitekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu tu jambo ambapo huwa likitokea baya, tunatafuta namna ya kulihalilisha, watu wakipata njaa hatuhangaika kujiuliza kwa nini watu wanapata njaa, tunataka wapewe chakula kama vile kitashuka toka mbinguni. Watoto waki-fail sana mtihani hatuhangaiki kwa nini wana-fail tunabadilisha fail grade ili wafaulu vilevile, leo hii watoto wengi wakipata mimba hatuhangaiki ku-protect kwa nini wanapata mimba, kwa nini tuzuie wasipate mimba utotoni, tunahangaika kutaka kunahalisha wapate mimba. Hatuwenzi tukaipa dhambi jina zuri na baadae tukaitukuza, dhambi ni dhambi itabakia kuwa dhambi, hatuwezi tukaipa jina zuri na hatimaye tukaitukuza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi atakaye mpa mimba mwanafunzi tutamkamata, atafika kwenye mikono ya sheria na mzazi atakayeshabikia mwanafunzi kupewa mimba na yeye atakuwa ameshiriki kwenye uovu wa aina hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtoto mdogo aliyeko shuleni atakayeruhusu masuala ya kupata mimba ajue anakiuka maadili ya elimu, anakiuka maadili ya mila, anakiuka maadili ya imani na anakiuka maadili ya kisheria za nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge, mimi naijua vizuri Tanzania hii, kuna watu wanaijua Tanzania hii kwa vipande vipande. Kwa mfano, katika nchi yetu hata ukiruhusu watoto kurudi shuleni wanaopata mimba, watoto wa Kilimanjaro uwezekano wa kuwepo wanaopata mimba ni mdogo sana. Kwa sababu Kilimanjaro level yake civililazition, level yake ya sensitization ya elimu ilishafika juu…

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila mpangilio)

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwango chake ni kikubwa, lakini leo hii ukiruhusu watoto kupata mimba na kuendelea na shule, halafu ulishaondoa viboko mashuleni, ulishaondoa adhabu mashuleni, huku Bara kwetu wanapomaliza mtihani wa kidato cha nne nusu yao ama wote wa kike watakuwa walishaolewa wana mimba wanasuburi wazae warudi mashuleni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niseme moja kubwa la ngazi ya watunga sheria kama Wabunge, tuangalie, tusichukue sheria moja tuangalie kwa ukubwa wake. Jimboni kwangu hivi nilivyoongea siyo kwamba natukuza watoto kupata mimba, lakini kama Kiongozi nimefanya hamasa Umoja wa Vijana wa CCM wote wafyatue tofali, nimetoa Mfuko wa Jimbo nikapeleka cement, nimepeleka nondo, nikatafuta na wadau tumeanzisha ujenzi wa hostel kwa shule zote 20 za kata kwenye Jimbo letu, ili kuwatengenezea watoto mazingira yatakayowaondoa kwenye mazingira ya kupata mimba.

Hatuwezi viongozi leo hii tukasema kwa sababu wanapata mimba basi turuhusu waendelee kupata mimba halafu waendelee na shule. Utaratibu gani huu wa nchi gani hii ambao watu wanarahisisha mambo kwa namna hiyo? Hatuwezi tukaruhusu vitu vya aina hiyo, halafu leo hii tukiruhusu aliyepewa mimba akaonekana hana kosa kwa neno lolote zuri tutakaloliweka, yule tunayemshtaki tunamshtaki kwa kosa gani? (Makofi)

Mambo makubwa matatu ninayoyasisitiza, moja Wabunge ni watunga sheria, tuangalie sheria hizi zinazokizana kwa mapana yake. Pili, tusiangalie sana suala la mimba hata tukaacha vigezo vingine, manaa yake tunaongelea mimba kama vile mimba inaweza ikaingia halafu mtoto asipate UKIMWI. Tunawasisitizia watoto wakafanye mambo hayo kama vile watapata mimba waendelee na shule, kama vile mimba itaingia halafu asipate UKIMWI. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge na Watanzania ni vema tukaweka uzito kwenye suala la maadili, kwenye suala la malezi, tukaweka na mazingira bora ya watoto kukaa bila kupata mimba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi wakati naenda kuanza form one baba yangu aliniambia ukipata mjukuu mjini usimuache kule, lakini mama yangu akaniambia unavyoenda kule mjini uwe makini kuna UKIMWI kuna mtu tumemzika juzi. Hata kwenda disco sikuenda nikidhania wote wanaocheza disco wana UKIMWI, lazima tuwasisitizie watoto wetu madhara ya matatizo wanayoweza kuyapata wakifanya ngono katika umri mdogo na siyo kuwaambia fanyeni ngono mtarudi muendelee na masomo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo Serikali imeendelea kuweka mazingira ambao yanawa… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji )

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri ahsante.