Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. George Boniface Simbachawene

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibakwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa ninashukuru kwa michango mizuri ya Waheshimiwa Wabunge ambayo katika kuchangia wamegusa maeneo ambayo na sisi Wizara ya TAMISEMI ndio ambayo tunayatekeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la kwanza ambalo nataka nitoe ufafanuzi kama sehemu ya mchango, ni suala la elimu bila malipo. Elimu bila malipo imesemwa sana na wachangiaji wengi na kwa namna ilivyokuwa inasemwa ni kama vile elimu bila malipo ni programu maalum ambayo imewekwa, ina fedha zake na kwamba sasa suala la utoaji wa elimu nchini hakuna mpango mwingine wowote ni elimu bila malipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani hili siyo sawa sawa lakini elimu bila malipo dhana na falsafa yake ilikuwa ni kujaribu kuondoa gharama za mapema hasa kwa wazazi na hasa wale wazazi wasiokuwa na uwezo kutakiwa kuchangia michango mingi sana ili watoto wao waweze kupata elimu. Jambo hili lilikuwa baya zaidi pale ambapo linawaweka kwenye jukumu la kwanza kabisa wale watoto wanaoandikishwa darasa la awali na darasa la kwanza, wazazi wao walipaswa kulipa kulingana na mpango uliowekwa na shule kiasi cha kuanzia shilingi 10,000 hadi shilingi 100,000. Sasa jambo hili liliwafanya wazazi wengi sana washindwe kuwaandikisha watoto wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka kuonesha tu namna ambavyo ongezeko la wanafunzi limekuwa kubwa kutokana na kuondolewa kwa gharama hizo ambazo sasa Serikali inazilipa, utaona kwa mfano kwa mwaka 2014 uandikishaji wa wanafunzi wa awali na darasa la kwanza ulikuwa kwa jumla yao walikuwa 915,000. Mwaka 2015 tulipoanza kuchukua gharama hii Serikali na kuzuia wazazi kutoa pesa hii ili wawaandikishe watoto, uandikishaji wa darasa la kwanza na awali walifika jumla ya 2,200,637. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2016 waliongezeka zaidi watoto kwa sababu wazazi wameondolewa ule mzigo na udahili wa watoto wa darasa la kwanza na darasa la awali ulifika 2,909,894. Kwa mwaka 2017 umeongezeka zaidi kwa maana ya kwamba sasa wazazi wameshaona kwamba Serikali imewapokea huu mzigo wa kulipa zile gharama za awali, udahili wa darasa la awali na darasa la kwanza kwa mwaka 2017 hadi Machi juzi tulivofunga usajili, tumeandikisha watoto 3,188,149. Kwa upande huu kwamba sasa tunampatia kila mtoto wa Tanzania elimu sasa hili tumefanikiwa, kinachobakia ni changamoto ya kuboresha tu kutoa elimu iliyo bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na Waheshimiwa Wabunge waliosema kwamba hii elimu bure imesaidia na ninawapongeza sana Wabunge wanaoliona hilo. Kitendo cha Serikali kupokea mzigo huu ikiwa ni pamoja na kulipa ada kwa wanafunzi wa Sekondari, kulipa ada wale waliokuwa wanasoma shule za bweni walikuwa wanatakiwa kulipa ada shilingi 70,000 na wale wa kutwa walitakiwa kulipa ada shilingi 40,00 Serikali inazilipa hizi fedha siyo tena zinalipwa na wazazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kulikuwa na gharama za mitihani wa kidato cha pili ilikuwa ni shilingi 10,000 na mitihani mingine ya Taifa ya form four ilikuwa ni shilingi 50,000 gharama hizi pia Serikali imezichukua. Kwa hiyo, utaona wazazi wamepata nafuu kubwa sana pia wanafunzi wengi sasa hawafukuzwi shuleni kwa ajili ya kwenda kufuata michango hii na hawazuiliwi vyeti vyao na Baraza la Mitihani kama ilivyokuwa siku za nyuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali pia inagharimia kwa kutoa shilingi 10,000 kwa mtoto wa shule ya msingi na shilingi 25,000 kwa mtoto wa shule ya sekondari kwa ajili ya uendeshaji wa shule ambazo fedha hizi zinapelekwa moja kwa moja shuleni. Jambo hili limewapa faraja sana wazazi na kuondoa mzigo kwao, kwa hiyo wazazi wamebakia tu na jukumu la kuhakikisha kwamba watoto wao wanakuwa na sare na vitu vinavyowasaidia ili kujifunza ikiwa ni pamoja na madaftari, kalamu na vitu vingine vidogo vidogo pamoja na nauli kwa wale wanaokwenda shuleni na kurudi, lakini na kuhakikisha kwamba watoto wao wanakula wale ambao hawakai shule za bweni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali pia inatoa hela ya chakula kwa ajili ya wanafunzi walio bweni. Kwa mwezi Serikali inatumia kiasi cha shilingi bilioni 20.8 kwa kila mwezi kwa ajili ya kugharamia gharama ambayo ingepaswa kulipwa na wazazi au walezi wa wanafunzi hawa. Mafanikio haya ni makubwa sana na hii nirudie kuwaomba Waheshimiwa Wabunge ambao tunafahamu kwamba bado tunalo jukumu kubwa ikiwa ni pamoja na majukumu mengine yanayohusiana na kuwasaidia watoto wetu ili waweze kupata elimu nzuri. Siyo kweli kwamba kwa sababu elimu bila malipo basi gharama zote Serikali imechukua na kila kitu ni Serikali hapana, hakuna programu hiyo, hatujawahi kupitisha mpango huo hapa, lakini jambo hili ilikuwa ni kuwapunguzia mzigo wazazi na walezi wa watoto ili waweze kupata haki yao ya elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya mafanikio haya sasa tunapata tatizo jingine na ambalo nalo limechangiwa na Waheshimiwa Wabunge wengi nalo ni suala la miundombinu katika utoaji wa elimu. Tuna upungufu mkubwa sana sasa wa madarasa na tuna upungufu mkubwa sana wa nyumba za walimu na tunao upungufu bado wa matundu ya vyoo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwashule za msingi upungufu wa madarasa ni 119,275 na kwa sekondari upungufu wa madarasa ni 7,458 na kwa nyumba za walimu kwa shule za msingi upungufu ni nyumba 182,899 na kwa sekondari ni nyumba 69,811. Hali kadhalika tuna upungufu wa matundu kwa shule za msingi na sekondari ya vyoo. Nitoe rai kwa Waheshimiwa Wabunge na wadau wengine nchini, kuhakikisha kwamba tunaendelea kusaidiana na Serikali kama tulivyofanya siku za nyuma kwa kushiriki katika miradi iliyopangwa katika maeneo yetu kwa kushirikiana na wananchi ili tuweze kuisaidia Serikali kupunguza kazi hii/mzigo huu ambao uko mbele yetu. Hata hivyo, Serikali tunapanga bajeti kwa mfano kwa mwaka unaoisha tulipanga karibu kiasi cha shilingi bilioni 59 kwa ajili ya uimarishaji wa miundombinu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado naendelea kutoa rai na kuwaomba Waheshimiwa Wabunge na kuwaomba wananchi wote wa Tanzania, nchi yetu inafuata siasa ya ujamaa na kujitigemea, kila mmoja analo jukumu la kuhakikisha kwamba anashiriki katika kujenga nchi yetu. Sote tunajua, miundombinu ya elimu inatusaidia siyo tu Taifa kupata wanafunzi na wananchi walioelimika pia wazazi wanafanya uwekezaji kwa sababu watoto hawa ni wa kwao. Kwa hiyo, tushirikiane na Serikali kwa sababu bado mzigo huu ni mkubwa na Serikali peke yake haiwezi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge na wananchi wote ambao wanaojitolea kwa namna moja au nyingine na wadau wengine wote nawashukuru, tuendelee kushirikiana ili kupambana na upungufu huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga hoja mkono.