Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimshukuru Mungu kwa kunipa uhai na nguvu za kuwepo mahali hapa na kuendelea kuwatumikia wananchi wangu wa Jimbo la Kyerwa. Pia namshukuru Mungu kuweza kuchangia Wizara hii muhimu kwa wananchi wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara hii kwa kazi nzuri zinazofanyika, kuisimamia vizuri Wizara hii muhimu hakika matunda yake yanaonekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza sana Serikali kwa kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi la kutoa elimu bure, kwa kweli imewapunguzia mzigo wazazi na matokeo yameonekana watoto wengi wanapelekwa shule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niipongeza Wizara baada ya tetemeko lililoupata Mkoa wetu wa Kagera, Mheshimiwa Naibu Waziri alifika Kyerwa na kuahidi kusaidia miundombinu iliyoharibiwa na tetemeko, namshukuru sana Naibu Waziri kwa msaada huo mkubwa kwa wananchi Kyerwa ingawa bado tunaendelea kuomba msaada wa kusaidiwa miundombinu mingi Kyerwa imechakaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kyerwa miundombinu mingi ya shule zetu imechakaa sana, kitu kinachosababisha watoto wetu kusoma kwenye mazingira magumu sana. Mfano, shule ambayo namuomba sana Mheshimiwa Waziri kutusaidia kuboresha miundombinu ni shule za msingi Kaisho, Mabila, Murongo, Businde, Songambele, Nyakatuntu, Bugomora na Isigiro ambazo shule hizo zina upungufu wa vyumba vya madarasa ni 94 vyenye gharama ya shilingi 1,880,000,000. Kwa upande wa vyoo kwenye shule hizo ni mbaya sana mapungufu ni matundu ni 198 yenye thamani ya shilingi 217,800,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa sekondari na kwenyewe hali ni mbaya tunaomba kusaidiwa na kuomba sana Waziri Mheshimiwa Ndalichako, naomba sana msaada wako maana sehemu kubwa wananchi ndiyo waliochangia kuweka hiyo miundombinu, ninaiomba kusaidiwa angalau ili kuunga mkono juhudi za wananchi Kyerwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wamejitahidi sana lakini mahitaji ni makubwa sana kitu kinachopelekea shule nyingine wanafunzi wanasomea nje. Mfano, shule ya msingi Maendeleo iko katika Kata ya Businde, walimu sita wako kwenye nyumba moja kitu ambacho kimesababisha kushindwa kuleta familia zao hasa wenza wao. Naiomba sana Wizara kuziangalia shule za namna hii jinsi ya kuzisaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee shule za sekondari za kata, wananchi wamejitahidi maeneo mengi kujenga madarasa na maabara lakini zaidi ya asilimia 85 hazina vifaa vinavyotakiwa kwenye maabara, naiomba sana Wizara kuzipatia vifaa hizo shule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kyerwa hatuna Chuo cha Ufundi, niiombe sana Serikali inapoangalia maeneo ambayo hawana vyuo vya ufundi naomba Kyerwa tuangaliwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika michango yangu naweza nikawa nimeongelea masuala yanayohusu Wizara ya TAMISEMI, lakini Wizara ya Elimu ndiye bosi wa elimu nchini. Miundombinu ikiwa mizuri, maabara zikiwa na vifaa vinavyotakiwa, tukapata walimu wa sayansi, elimu itakuwa nzuri na Wizara ya Elimu itakuwa imefanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaipongeza Wizara kwa motisha wanayopewa walimu, lakini bado walimu wanadai stahiki zao, niombe sana walimu wanaodai walipwe ili waweze kutulia na kuwafundisha watoto wetu bila usumbufu wowote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee utaratibu wa Chuo Kikuu Huria ambao ulikuwa unawapa nafasi wale ambao hawakufanikiwa kufaulu kidato cha nne kwenda kidato cha sita, utaratibu wa kusoma foundation mwaka mmoja halafu mtu akifaulu anaenda kusoma digrii. Hili jambo limewasaidia wengi wakiwemo wanasiasa ambao wengi wao humu ndani ya Bunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namuomba Mheshimiwa Waziri suala hili liruhusiwe lakini lisiwe vyuo vyote ila Chuo Kikuu Huria kiendelee kutoa elimu hii ambayo wengi leo hii chuo hiki kimepata Profesa, Madaktari na wengine wengi wamepitia chuo hiki. Wako Wabunge wengi ambao wanataka kujiendeleza lakini kwa zuio la Mheshimiwa Waziri tumeshindwa. Ninakuomba Waziri uliangalie ili kutusaidia wanasiasa tujiendeleze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo narudia kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wa Wizara kwa kazi nzuri inayofanyika tunawaombea kwa Mungu awape hekima katika kutimiza majukumu yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Ahsante.