Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kuipongeza Wizara katika usimamizi wa elimu. Nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri aliyofanya. Vilevile nimpongeze Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu umejikita zaidi katika elimu na mafunzo ya ufundi stadi (VETA). Katika kitabu cha bajeti cha mwaka 2017/2018 Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) imepanga kutimiza malengo yafuatayo; itaendelea kufuatilia ujenzi wa Vyuo vya Ufundi Stadi vya mikoa mipya ya Njombe, Geita, Simiyu na Rukwa. Maelezo yanapatikana katika kitabu cha hotuba ukurasa wa 96.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa sera ya Taifa inasema kila Mkoa na kila Wilaya kuwepo na Chuo cha VETA, nikiangalia katika Mkoa wa Geita wenye Wilaya tano hakuna kabisa Chuo cha VETA katika Wilaya zote na katika Mkoa. Wananchi wa Mkoa wa Geita tunayo mahitaji makubwa sana ya elimu ya ufundi stadi. Watoto wengi sana wanaomaliza elimu ya msingi na sekondari ambao hawaendelei na masomo ya ngazi za juu hawana ujuzi wa kuwawezesha kujiendeleza katika maisha yao ya kila siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo tukiwa na vyuo vya VETA katika kila Wilaya itasaidia kuwawezesha vijana hawa kuwa na ujuzi. Vilevile Serikali ya Awamu ya Tano imekusudia kuwa na Tanzania ya viwanda. Hivyo tunahitaji vijana wawe na ujuzi ili tuweze kufikia azma ya Tanzania ya viwanda. Kwa melezo haya ningependa kujua na kupata maelezo ya kina ni lini ujenzi wa Chuo cha VETA Mkoa wa Geita utaanza rasmi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimewiwa kuuliza kutokana na maelezo kwenye bajeti kwamba Serikali itandelea kufuatilia ujenzi, lakini haielezi bayana juu ya kuanza kwa ujenzi wa chuo hicho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya machache, naunga mkono hoja.