Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Grace Victor Tendega

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi nichangie katika hotuba hii. Naomba niungane na wenzangu kwa kuwapa pole wafiwa wote wa watoto waliopata ajali Mkoani Arusha, Mungu azilaze roho za marehemu mahali pema peponi Amina.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na maneno ya wanazuoni ambayo yanasema ukitaka Taifa bora, boresha elimu; ukitaka kuboresha elimu boresha walimu na ukitaka Taifa la watu wanaojiheshimu, heshimu walimu. Ninazungumza hivi kwa sababu walimu wetu kwa kweli wamekuwa na kinyongo cha kufanya kazi yao, wengi wamekuwa na malalamiko mengi na wamekuwa hawapati haki zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, walimu zamani walikuwa wakipata posho ya mazingira magumu ya kazi na hasa wale wa vijijini ili yawavutie, lakini sasa hivi hakuna posho hizo. Napenda kusema kwamba mimi pia ni mwalimu, wakati huo tukifundisha kulikuwa na posho, wale walimu wa sayansi walikuwa wana posho ya ziada ya walimu wengine wa masomo ya arts na biashara, maslahi hayo yalikuwa yanatia moyo na mwalimu anafundisha kwa nguvu kubwa sana na wanafunzi walikuwa wakifaulu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile unaona kwamba kada hii ni kada inayofanyakazi kwa saa 24. Mwalimu anaandaa somo, mitihani na anasahihisha, mwalimu anapanga matokeo, muda wote wa siku mwalimu anafanya kazi hizi, lakini Serikali hii imekuwa haiwalipi posho ya kufundishia walimu ambayo ilikuwa ni kilio chao cha siku nyingi na walimu wamekuwa hawapati hizo posho. Tunaomba Serikali iangalie suala hili ili walimu wetu waweze kupata posho ya kujikimu na waweze kufanya kazi vizuri, hasa walimu wanaokaa kwenye mazingira magumu. Tumeona wengine wakifuata mishahara yao wanafunga shule kabisa. Mimi nina shule yenye walimu wawili kutoka mkoani kwangu, wakati wa kufuata mishahara mmoja anabaki, mwenzake anakaa na darasa la kwanza mpaka la saba. Kwa kweli, hii ni kazi kubwa kwa walimu, tuwatizame kwa jicho lingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna uhaba wa walimu wa masomo ya sayansi hawapo, tunaomba Waziri alitizame suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie sasa suala la vitabu. Vitabu ndiyo moyo wa mwalimu katika kufundisha, tuna mitaala, vitabu na vilevile tuna masuala mengine ambayo yapo katika ufundishaji. Mwalimu akikosa kitabu, akipata kitabu ambacho kinamwongoza mwanafunzi vibaya Taifa zima litakwenda kwenye fikra hizo na tutatengeneza Watanzania wenye fikra ambazo zimepotoshwa. Vitabu hivi kama tulivyokwisha kuviona na wenzetu wamevionesha hapa asubuhi vimekuwa na mapungufu mengi, hivi Serikali inataka tuende wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri anafahamu, alikuwa kwenye Bodi ya Taasisi ya Elimu na amefanya kazi anajua jinsi ya kuandaa vitabu anafahamu kabisa. Baada ya kumaliza kazi hii inatakiwa watu wa kuhakiki, kuna panels za masomo ambazo zinatakiwa zipitie. Kweli kama panel zile zilipitia na makosa haya yakatokea basi hawa waliofanya kazi hiyo wachukuliwe hatua, kwa sababu hii ni hasara kubwa kwa Taifa letu, Watanzania na watoto wetu wanakwenda kufundishwa vitu ambavyo vitawapoteza na vitawapotosha. Kwa sababu wanasema unapopata elimu ya msingi bora ndiyo itakayokuongoza mpaka kwenye maendeleo ya baadae. Hivyo, ukimkosea mtoto hapa toka kwenye msingi kwa kweli utamfikisha mahali ambapo siyo panakotakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye suala sasa la ufundishaji hasa kwa watoto wa kike na masuala ya mazingira ya watoto wa kike katika elimu. Tumeona kwamba kuna changamoto nyingi…

(Hapa kengele ililia kuashiria muda wa mzungumzaji kuisha)

MWENYEKITI: Ahsante.