Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Abdallah Haji Ali

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kiwani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. ABDALLA HAJI ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu muweza wa mambo yote kutujalia kama hivi alivyotujalia. Pia nakushukuru wewe Mwenyekiti kwa kunipa nafasi hii ndogo na mimi nichangie angalau machache katika mengi ya Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa langu ni moja tu, napenda kuzungumzia kidogo suala la utafiti kwamba Taifa lolote duniani haliwezi kuendelea ikiwa halitatilia maanani suala zima la utafiti wa sayansi na teknolojia. Suala zima la utafiti wa sayansi na teknolojia ni lazima lipewe kipaumbele ndiyo maendeleo yapatikane katika nchi. Tanzania si kisiwa ni nchi kubwa, Tanzania ni nchi hai na ipo hatuwezi kuwa kinyume na teknolojia hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa Tanzania chombo kikubwa kinachodhibiti masuala ya utafiti ni Tume ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH). Hiki ni chombo kinachodhibiti masuala ya utafiti na ndiyo chombo mama wa mambo yote ya utafiti yanayofanyika hapa Tanzania. Chombo hiki kazi yake kubwa kisheria ni kufanya utafiti katika nyanja za sayansi na teknolojia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mataifa yaliyoendelea tunaona kwamba wamekuwa wakitenga asilimia kubwa ya bajeti yao katika kuendeleza masuala ya utafiti. Hapa kwetu Tanzania tunaona kwamba Serikali inakuwa inaitengea sana Tume hii katika kufanya utafiti lakini tukiri kwamba pesa zinazotengwa katika kufanya utafiti hazitoshi, ni kidogo. Hapa Waziri mwenye dhamana wewe ndiyo mwenye kilio, ulie na sisi wa kando tukuone tulie pamoja Serikali ikuongezee mapato juu ya suala zima la utafiti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiangalia takwimu za hizi karibuni za miaka iliyopita utaona viwango vilivyokuwa vikitolewa kwa ajili ya Tume hii. Mwaka 2010/2011 kilichotengwa ni shilingi bilioni 30, lakini kilichotolewa hakikuzidi shilingi bilioni 19. Aidha, mwaka 2011/2012 zilitengwa shilingi bilioni 25.7 lakini kilichotolewa kwa ajili ya masuala ya utafiti hakikuzidi shilingi bilioni 7.3.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka 2012/2013 zilitengwa shilingi bilioni 21.4 zilizotolewa ni shilingi bilioni 12.8. Mwaka 2013/2014 zilitengwa shilingi bilioni 16 na hapa kwa bahati mbaya hakuna chochote kilichotolewa. Mwaka 2014/ 2015 zilitengwa shilingi bilioni 16.5 na zikatoka shilingi bilioni
3.8 na mwaka 2015/2016 zilitengwa shilingi bilioni 4.3 na hakujulikana kitu gani kilichotokezea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa naishauri Serikali, Taifa lolote linalotaka kuendelea...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. ABDALLA HAJI ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.