Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Stella Ikupa Alex

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi hii adimu. Nami moja kwa moja niipongeze sana Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi, Mheshimiwa Rais wetu mpendwa, Makamu wa Rais pamoja na Waziri Mkuu kwa jinsi ambavyo wameyashughulikia masuala haya ya watu wenye ulemavu kupitia Wizara hii ya Elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nimpongeze sana Mheshimiwa Profesa Ndalichako pamoja na Mheshimiwa Stella Manyanya wamekuwa ni mama zetu kwa maana kwamba wamekuwa ni wasikivu sana. Muda wote ambapo tumekuwa tukiwahitaji kwa ajili ya masuala ya watu wenye ulemavu wamekuwa wakipatikana kirahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa ni mpungufu wa fadhila nisipoishukuru Serikari kwa jinsi ambavyo imetoa kipaumbele cha elimu kwa wanafunzi wenye ulemavu. Kwa sababu ya muda nitataja baadhi ya maeneo na si kwa umuhimu basi hakuna mengine. Kuna ukurasa wa 22 aya ya 45; ukurasa wa 23 aya ya 46, lakini kuna ukurasa wa 26 aya ya 53, hiyo nitaomba niisome kwa sababu ni kitu kigeni kidogo. Inasema:-

“Imeandaa Kiongozi cha Mwalimu wa Masomo ya Sayansi kwa wanafunzi wasioona na wenye uoni hafifu. Uwepo wa kiongozi hiki utasaidia wanafunzi wasioona wa sekondari kwa mara ya kwanza kuwezeshwa kusoma masomo ya sayansi”.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hii ni habari njema sana kwa watu wenye ulemavu. Pia shukrani zangu zinaendelea ukurasa 29 aya ya 55 mpaka (56) na ukurasa wa 30 aya ya 57 mpaka 59.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia niipongeze sana Serikali, wakati Mheshimiwa Waziri akisoma hotuba yake siku ya Jumamosi alikiri kwamba kuna changamoto ya miundombinu na vifaa saidizi. Niiombe tu Serikali tunaongelea mambo ya elimu jumuishi lakini haiwezi kuwa kama miundombinu haitaboreshwa. Kwa hiyo, niiombe Serikali iiendelee kutoa kipaumbele kwa habari ya uboreshaji wa miundombinu ili elimu jumuishi iweze kuwezekana katika Taifa letu la Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sambamba na hili niombe Serikali kwamba katika vyuo vyetu vya ualimu, kwa sababu sasa hivi kuna uhaba mkubwa wa Walimu wa elimu maalum, kwa hiyo katika vyuo vyote vya ualimu nchini elimu hii ifundishwe. Kwa hiyo, Mwalimu anapotoka chuoni anakuwa ana ufahamu ama uelewa wa elimu maalum. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunapoongelea elimu jumuishi ni pamoja na Walimu, tusipokuwa na Walimu wa kutosha ambao wanafahamu elimu maalum hili halitawezekana. Kwa hiyo, niiombe Serikali iweke mkazo ama iweke msisitizo kwamba katika vyuo vyote vya ualimu elimu maalum ifundishwe ili mwalimu anapotoka pale anapokwenda shule yoyote ana uwezo wa kumfundisha mwanafunzi mwenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee Walimu wenye ulemavu. Inawezekana Serikali ikawa haina takwimu sahihi za Walimu wenye ulemavu lakini Walimu hao wapo. Kwa hiyo, niiombe Serikali iwe na takwimu sahihi za Walimu wenye ulemavu ili waweze kujua changamoto na mahitaji walionayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pPamoja na ugawaji wa hivi vifaa ambavyo vimegawiwa lakini Walimu hawa wasipoangaliwa itakuwa pia ni kazi bure. Kwa maana kwamba Serikali ikiwa na takwimu sahihi za hawa Walimu wenye ulemavu itawawezesha ili waweze kuwa na sifa, maarifa na weledi kama Walimu wengine. Walimu hao wanahitaji pia kujengewa uwezo kwa njia ya mafunzo. Kwa hiyo, niiombe Serikali pia itoe kipaumbele sana kwa ajili ya mafunzo ya hawa Walimu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee tena kwa mara nyingine kwa sababu nimeshawahi kuongea kwenye Bunge lako Tukufu, kwamba Serikali ione sasa umuhimu wa kuingiza lugha ya alama kwenye mitaala ya elimu ya Tanzania. Kwa nini nasema hivyo? Kila siku hapa tunalalamika kuhusu wakalimani wa lugha ya alama lakini kama hii lugha ya alama itafundishwa kwenye elimu yetu kuanzia darasa la kwanza mpaka form four, huyu mtu tunamuandaa kuwa Mwalimu, Mbunge, Daktari, Polisi, kiongozi wa madhehebu ya dini, kwa hiyo ataweza kuwasiliana na mtu ambaye ni kiziwi kwa urahisi. Kwa hiyo, niombe sana Serikali yangu sikivu ilione hili na kwa hapo baadaye tutengeneze kizazi ambacho kitakuwa kinaweza kuwasiliana na viziwi kwa urahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee pia takwimu za watahiniwa wenye ulemavu kuanzia darasa la saba, form four mpaka cha kidato cha sita. Kwa nini nasema hivi? Mheshimiwa Profesa Ndalichako atakuwa ni shahidi hapa katikati nilimsumbua sana kwa habari ya uhamisho wa mwanafunzi ambaye alikuwa na ulemavu. Hizi takwimu za watahiniwa zitasaidia wakati wa selection. Unapomalizika mtihani wa darasa la saba Serikali ikafahamu kwamba tuna wanafunzi wenye ulemavu wa aina hii kwa hiyo watawapangia shule kutokana na aina ya ulemavu walionayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niiombe sana Serikali kuwa na takwimu sahihi za watahiniwa wenye ulemavu, hii itasaidia kwa habari ya selection. Nitumie nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Profesa Ndalichako kwamba ule uhamisho ulifanikiwa na mtoto anaendelea na masomo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia niishukuru Serikali sana kwa sababu mimi ni mwakilishi wa watu wenye ulemavu kuhusiana na wale watoto mapacha walioungana kule Iringa, Consolata na Maria ambao kiukweli Serikali imesimamia elimu yao na watoto wanakiri kwamba hakukuwa na shida kwao kwa sababu hata wakiwa pale shuleni wakati wa kidato cha sita walijengewa kajumba ambako kalikuwa ni maalumu kwa ajili yao peke yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili niongeze, ulemavu wa jinsi hii, Mheshimiwa Profesa Ndalichako yule mtoto ambaye nilimwomba uhamisho kwa ajili yake, amepangiwa shule ya Jangwani, lakini bado kuna changamoto kwa sababu ulemavu wake unahitaji usaidizi, yaani anahitaji mtu wa kumsaidia hawezi kushika kijiko kula mwenyewe. Kwa hiyo, niiombe Serikali ione jinsi gani ya kuandaa wasaidizi kwenye hizi shule kwamba anakuwepo matroni maalum kwa ajili ya watoto wa jinsi hii. Matroni atamuogesha, atamsaidia kwenda chooni lakini pia atamsaidia hata chakula na kumfulia nguo. Kwa hiyo, niombe Serikali pia hili iliangalie kwa jicho la tofauti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho na si kwa umuhimu naomba niongelee Bodi ya Mikopo. Nimekuwa nikiomba na imekuwa ni kilio changu cha muda mrefu kwamba wanafunzi ama watoto ambao wanafanikiwa kufika kidato cha tano na sita mpaka kufika chuoni ni wachache sana. Kwa hiyo, hii elimu bure inayotolewa naomba Serikali itolewe bure kwa watu wenye ulemavu yaani mtoto mwenye ulemavu kama atafanikiwa kuingia kidato cha tano na mpaka kufika chuo, asomeshwe bure na Serikali kwa sababu wako wachache. Kwa hiyo, hata gharama ni ndogo haitakuwa kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ya kwangu kwa leo ni hayo, naomba kuwasilisha. Naunga mkono hoja ya Wizara hii. Ahsante.