Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Susan Anselm Jerome Lyimo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. SUSAN A.J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia fursa hii ili na mimi niweze kuchangia katika hoja muhimu sana ya elimu kwa sababu naamini wote humu ndani tunatekeleza majukumu yetu kwa sababu ya elimu. Hakuna Mbunge ambaye hajaingia darasa la kwanza awe yumo humu ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimesikitishwa sana, sana, sana na maneno aliyosema Mheshimiwa Salma Kikwete, ni mwanamke mwenzangu, lakini sishangai kwa sababu hata mume wake aliwahi kusema kwamba watoto wa shule wanaopata mimba ni viherehere vyao. Nimesikitishwa zaidi kwa sababu Waheshimiwa Mawaziri wote wawili ambao ni wanawake nao pia walikuwa wanapiga makofi. Jambo hili linasikitisha sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo sababu naamini kwamba Mheshimiwa Naibu Waziri alivyokuwa anajibu swali la Mheshimiwa Mama Sitta hapa Bungeni ilikuwa ni kiini macho tu, kwa sababu alisema by March angeleta mwongozo huo na hii ni Mei hajaleta na leo anampigia makofi Mheshimiwa Mama Salma Kikwete. Hii inaonesha ni jinsi gani humu ndani watu ni wanafiki, hawaishi/hawatembei katika maneno yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini kabisa hapa Tanzania tunataka tuwe na elimu jumuishi au elimu shirikishi kwamba kila mtoto asome.

TAARIFA...

MHE. SUSAN A. J LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza sipokei taarifa yake kwa sababu nilikuwa nam-refer Naibu Waziri aliyetoa majibu humu ndani na leo anamshabikia Mheshimiwa Mama Salma Kikwete ambaye anaenda kinyume na kitu ambacho alikisema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na suala la vitabu, nililianza juzi na bahati mbaya sikuwa na muda lakini nashukuru sana Mheshimiwa Doto Biteko ameliongea. Niseme ni wazi kwamba hapa ndani au katika Bunge lako baadhi ya Mawaziri wanaleta utani. Suala la vitabu ni zito sana. Wote tunatambua kwamba nchi hii ina ukosefu mkubwa wa Walimu na kwa maana hiyo vitabu vingekuwa vimetengenezwa vizuri watoto wangeweza kuvisoma na kuvielewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo ambalo linasikitisha Mheshimiwa Waziri anasema watawachukulia hatua, tunataka kujua toka mwaka jana wakati tumekuwa na tatizo hili, amewachukulia hatua watu kiasi gani? Jambo hili linasikitisha kwa sababu leo Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu ndiye aliyekuwa Mkurugenzi wa Taasisi ya Elimu. Kwa hiyo, ina maana hivi vitabu vibovu vimetengenezwa chini yake lakini leo amekuwa elevated kuwa Katibu Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaongea suala la Kiingereza nchi hii, tunajua watoto wadogo ni tabula rasa kile wanachokipata mwanzoni ndio kina-stick katika ubongo wao. Leo ukichukua kitabu hiki cha Kiingereza kwanza title yenyewe, ‘I learn English language’, this is not English. Hata hivyo, ukienda katikati ukurasa wa 127 kinasema, look at this insects lakini ua (flower) limewekwa kama ni insect (mdudu).

Sasa mtoto wa darasa la tatu unamwambia leo kwamba ua ni mdudu anakuwa anajua kwamba ua ni mdudu. Kuna huyu mtu anaitwa Dkt. Elia Y. Kibga ambaye ndiye Acting Director amesaini, ajue kwamba Mungu anamwona watoto wake hawasomi vitabu hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu ya msingi ni kwamba hivi vitabu sio tu vina matatizo ya kimaudhui bali pia vina matatizo makubwa ya kimantiki. Tunaomba vitabu hivi viondolewe mashuleni lakini kubwa zaidi tunaomba Tume au Kamati Maalum iundwe ipitie vitabu vyote kuanzia darasa la kwanza mpaka kidato cha sita kuona makosa makubwa yaliyopo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo vitabu hivi vimeshasambazwa takribani nakala milioni 16. Kama kila nakala ni Sh.5,000 bado usambazaji maana yake tuna zaidi ya shilingi bilioni 100 tumezipoteza, hela hizi zingeweza kabisa kujenga zaidi ya madarasa 500. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi niseme tu kwamba tunaomba kabisa Bunge lako Tukufu liunde Kamati/ Tume Maalum iende ikachunguze uchapishaji wa vitabu hivi. Pia isiruhusu Taasisi ya Elimu kuwa ndiyo inayotunga vitabu bali kuwe na chombo ambacho kitasimamia kuhakikisha kwamba vitabu hivi vinakuwa vizuri kwa ajili ya watoto wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikitoka kwenye suala la vitabu nije kwenye suala la ripoti ya CAG. Wote tunajua kwamba Mlimani City, nadhani kila Mbunge amepita pale, mkataba wa Mlimani City ni mbovu haijapata kutokea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa ya CAG ya 2005 inaonesha wazi kwamba ilikuwa inatakiwa pale Mlimani City pawe na hoteli ya three stars lakini mpaka leo hii tunaongea baada ya miaka 14 hakuna hoteli imejengwa pale. Mbaya zaidi mkataba huo unasema kwamba Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kinapaswa kupata 10% ya gross profit, lakini cha ajabu mpaka leo Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kinapata 10% ya net profit. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili linaleta hasara kubwa na ndiyo sababu leo tunazungumzia miundombinu ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kwa mfano, Bweni Namba Mbili (Hall Two) limefungwa toka mwaka jana hakuna mwanafunzi yeyote anayekaa pale kwa sababu ya uchakavu. Hizi fedha zingeweza kusaidia kufanya ukarabati wa jengo lile. Kwa hiyo, tunaomba sana hii ripoti ya CAG ifanyiwe kazi ili mapato ambayo yanaenda kwa mmiliki wa Mlimani City yawe yanaenda 10% ya gross profit na sio ya net profit. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala lingine ambalo nataka Wizara itusaidie na hii pia inatokana na CAG ripoti. CAG ripoti inasema 94% ya shule zilizoanzishwa nchini zinatoa huduma bila ya kusajiliwa. Hata hivyo, ni Wizara hiyo hiyo inapoenda kusimamia shule za private hata kama umeongeza darasani mwanafunzi mmoja tu shule inafungiwa. Mtuambie ni kwa nini 94% ya shule hazijafanyiwa usajili?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikitoka hapo sasa nije kwenye suala zima la ukaguzi, limezungumzwa sana na hata leo tumesema kwamba bila ukaguzi elimu yetu haiendi. Hata hivyo, fedha zinazotengwa kwa ajili ya ukaguzi ni kidogo sana..

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la hosteli za Chuo Kikuu cha Dar es Salaam maarufu kama Magufuli Hosteli. Pamoja na kwamba Waziri hajaeleza gharama halisi lakini inajulikana kwamba gharama za hostel zile ni shilingi billioni kumi, that means kila jengo moja ni shilingi milioni 500. Haiwezekani na haingii akilini na nimejaribu kuongea na wahandisi, haiwezekani jengo linachukua takribani wanafunzi 390 liwe lina gharama ya shilingi milioni 500.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba CAG akafanye special audit kuona ni kiasi gani kimetumika na kama ni kweli ni shilingi milioni 500 mimi niko tayari nitatoa shilingi milioni zangu 500 Serikali inijengee jengo kama hilo ili tuweze kuwaweka vijana wengine, kabisa. La sivyo labda naweza nikasema pia naweza nikaachia Ubunge kama kweli jengo moja la ghorofa tatu limejengwa kwa shilingi milioni 500. Mimi naamini hii ilikuwa ni siasa na kama ni hivyo basi tunaomba hata hizi hela za vitabu zijenge hosteli nyingine katika vyuo vingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la Mloganzila, mimi niseme kwa mara ya kwanza Tanzania imejenga hospitali kubwa ya Kimataifa na imekamilika toka mwaka jana mwishoni lakini mpaka leo haijafunguliwa rasmi kwa sababu tu haina watumishi. Naiomba Serikali na namwomba Mheshimiwa Rais, kama alivyotoa vibali kwa wale madaktari walioshindwa kwenda kuajiriwa Kenya, atoe vibali ili hospitali ile iweze kufanya kazi. Kwa sababu hospitali ile ni kubwa sana, ina vifaa vingi sana na wewe Mheshimiwa Mwenyekiti kama Mjumbe wa Kamati umeenda umeiona lakini imekaa pale kama white elephant.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sana hospitali ile ifanye kazi kwa sababu itaingizia Taifa kipato kikubwa kwa sababu wagonjwa wengi watatoka nje ya Tanzania watakuja kutibiwa pale, kwa hiyo vipatikane vibali kwa ajili hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ualimu. Najua mengi yamezungumzwa kutokana na matatizo ya walimu na mimi niseme kama mwalimu. Elimu ni mwalimu. Mwalimu akipata mazingira bora ataweza kufanya kazi yake vizuri lakini…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante.