Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Dr. Shukuru Jumanne Kawambwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bagamoyo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, natanguliza pongezi kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba nzuri na kwa kazi nzuri. Pia, nawapongeza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Katibu Mkuu, viongozi na watumishi wote wa Ofisi ya Waziri Mkuu kwa utendaji mzuri na maandalizi mazuri ya bajeti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kushukuru mema mengi tunayofanyiwa na Serikali yetu, Jimbo langu la Bagamoyo linakabiliwa na changamoto kadhaa ambazo zinahitaji ufumbuzi:-
(i) Kuhusu kuwalipa fidia wananchi wa Zinga, Kerege na Kiromo wanaopisha mradi wa EPZ. Mazingira wezeshi ya uwekezaji ni pamoja na kuwalipa wananchi fidia ya ardhi na mali zao kupisha wawekezaji. Ni miaka tisa sasa wananchi hao bado wanasubiri kulipwa fidia zao. Serikali yetu Tukufu iwalipe fidia wananchi hawa mapema iwezekanavyo.
(ii) Ukosefu wa ajira kwa vijana wengi Jimboni Bagamoyo. Naiomba Serikali kujielekeza zaidi katika kuongeza fursa za mikopo na elimu ya ufundi na ujasiriamali kwa vijana katika JImbo la Bagamoyo. Serikali iharakishe mchakato wa ujenzi wa Chuo cha VETA, Wilaya ya Bagamoyo. Kwa mustakabali wa Taifa, naunga mkono uamuzi wa kukabidhi Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi kwa Wizara ya Elimu kwa ajili ya kutoa mafunzo ya ufundi.
(iii) Azma ya Serikali kupanua na kuimarisha kilimo cha umwagiliaji ni jambo jema sana. Naiomba Serikali yetu Tukufu itutengee Bagamoyo fedha za kutosha kutuwezesha kupanua miradi ya umwagiliaji hususan kujenga miundombinu katika miradi ya umwagiliaji ya JICA - Bagamoyo na Chauru na Kidogozero kule Chalinze. Serikali itutengee pia ruzuku kwa ajili ya pembejeo, msimu huu wa kilimo pembejeo zimekuwa tatizo sana.
(iv) Mtandao wa barabara zinazopitika vijijini ni nyenzo kubwa kwa ajili ya maendeleo ya uchumi na afya kwa wananchi wetu. Kasi ya ujenzi na ukarabati barabara za Bagamoyo Vijijini ni ndogo sana.
Barabara nyingi za Bagamoyo Vijijini ni mbovu na zinawagharimu wananchi kiuchumi na maisha yao. Barabara katika Kata za Fukayosi, Yombo, Kiromo, Zinga na Mapinga na barabara ya Mjini Bagamoyo ni mbovu sana. Serikali iongeze mafungu katika barabara na iangalie uwezekano wa kuunda Wakala wa Barabara Vijijini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utalii una fursa kubwa ya kuchangia pato la Taifa letu na utalii wa Tanzania ni wa namna mbalimbali ikiwemo utalii wa fukwe za bahari, utalii wa wanyamapori, utalii wa utamaduni, kihistoria na malikale. Bagamoyo ina fursa kubwa ya utalii wa kihistoria na malikale. Serikali ituwezeshe kuhifadhi magofu ambayo yanazidi kumalizika mwaka hadi mwaka. Serikali itenge mafungu kwa ajili ya kazi hii. Pia, Wilaya iwezeshwe kufundisha vijana katika fani za kumhudumia mtalii mfano, kuongoza watalii na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.