Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nitoe mchango wangu kwenye Wizara hii ya Elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwanza kabisa nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri anayofanya kwenye Wizara hii, mapinduzi makubwa yamefanyika kwa muda huu wa mwaka mmoja ambao amekaa hapo. Tumeona kwenye hotuba yake hapa vitu vingi
vimefanyika vikubwa vikubwa ambavyo siku za nyuma vingechukua labda miaka mingi sana lakini kwa muda mfupi amejitahidi. Nichukue nafasi hii kwa kweli kumpongeza sana kwa juhudi anazoendelea nazo. Naamini kwa muda atakaokuwepo kwenye Wizara hii mabadiliko makubwa yatakwenda kutokea kwa sababu ni mama anayejitahidi sana; ni mama anayejali na ni mama kwa kuongea anamaanisha, lakini pia vitendo vyake tunaviona. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa sababu mwaka jana nilipeleka maombi ili kunisaidia kwenye shule yangu mojawapo ili iweze kupata kibali hatimaye iwe A-Level. Alinisaidia akanipa kama shilingi milioni 100 na zaidi, tukajenga bwalo na mabweni ya wanafunzi tayari yamekamilika na mwaka huu tumepata kibali cha kuingiza watoto wa kidato cha tano. Ahsante sana Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nianze kutoa mchango wangu kuhusiana na ukaguzi wa shule kwenye maeneo yetu. Ukaguzi wa shule ni muhimu sana kwenye nchi yetu na kwenye shule zetu kwa sababu kwa huo ndio tunaelewa ubora wa elimu yetu inayotolewa huko mashuleni. Hata hivyo, Kitengo cha Ukaguzi kuanzia huko Taifa mpaka huku chini Wilayani kina hali sio nzuri sana. Nichukue mfano wa kitengo hiki kwenye Wilaya yangu ya Maswa. Wilaya yangu ya Maswa kitengo hiki hakina miundombinu inayotakiwa ili kiweze kufanya kazi yake vizuri. Kwanza wako kwenye kaofisi kamoja ambapo wamejibana, lakini pia vifaa hawana, wana gari moja ambalo limezeeka sana na ni gharama kubwa kulifanyia maintenance.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukichukua hali iliyoko kwenye kitengo hiki, vifungu au mafungu ya fedha yanayopelekwa kwenye ukaguzi wa elimu ni kidogo sana kiasi kwamba hawawezi kwenda field na kukikuta gari bovu kama ilivyo kwenye Wilaya yangu ndiyo hali inakuwa ngumu kabisa. Hawawezi kufanya maintenance, hawawezi kununua mafuta, hawana posho ya kujilipa wanapokwenda kukagua kwa hiyo, ubora wa elimu kwenye maeneo yetu unakuwa ni wa mashaka mashaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe Kitengo cha Ukaguzi kwa shule zetu, shule za msingi hata shule za sekondari kiboreshewe mazingira yake. Wapewe usafiri unaowezekana kusafiri kwenda kwenye shule kukagua, wapewe vifaa vinavyohitajika, wapewe posho yao, wapewe mafuta, kama hawapewi watafanyaje kazi hizi, itakuwa ni ngumu sana. Gari lililopo pale kwenye Wilaya yangu halina matairi, halifanyiwi maintenance, hawa watu wapo tu pale ofisini. Pamoja na kwamba wako wachache lakini wangeweza kujitahidi angalau basi kuzitembelea baadhi ya shule ili waangalie ubora wa elimu inayotolewa pale, hilo ni jambo la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo nataka nizungumzie ni hii Tume ya Walimu, sijui kama iko sehemu ngapi, kama iko kwenye Wizara yake, Wizara ya Utumishi au Wizara ya TAMISEMI. Hii Tume ya Walimu na yenyewe ina matatizo lukuki. Hawa Tume inatakiwa akituhumiwa mwalimu waende kwenye eneo la kazi la yule mwalimu, lakini hawaendi kwa sababu pia wanapokea pesa kidogo. Wakienda pia wanatakiwa baada ya kubaini mashtaka aliyonayo warudi waje wafanye kikao ofisini (kikao cha Tume), lakini hawawezi kufanya vikao vyao vya Tume kwa sababu pia hawana fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo yake unakuta mwalimu ametuhumiwa, ameandikiwa mashtaka wamemtembelea lakini hawawezi kumwita kuja kufanya naye kikao kwa sababu fedha hazipo kwenye Tume hii ya Walimu na kwa hiyo, mwalimu huyo anakaa analipwa nusu mshahara kwa sababu anapotuhumiwa anasimamishwa analipwa nusu mshahara muda mrefu. Kwenye Wilaya yangu ya Maswa kuna walimu kama wawili, watatu hivi, wamekaa sasa kama mwaka nzima hawajasikilizwa, wanaendelea kulipwa nusu mshahara. Kwa kweli naomba sasa Wizara hii ya Elimu iweke mpango madhubuti ya kuimarisha Tume hii ya Utumishi ya Walimu ili iweze kuwasaidia walimu hasa wale

wanaopata matatizo na kama mtu kesi yake haieleweki basi imalizwe mapema halafu aendelee kufanya kazi yake vinginevyo kwa mafungu wanayopewa hawawezi kufanya kazi yao vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni majibu wanayosubiri walimu ambao Tume imekwishapeleka hoja zao huko Makao Makuu wanasuburi muda mrefu sana. Wengine wanaposubiri hata barua zinaporudi ili aje arudishwe kazini inachukua muda mrefu mno, lakini ana barua ambayo iname-clear mashtaka yake lakini bado kurudishwa kazini inakuwa ni ngumu sijui utaratibu huu unakuwaje. Maana inakuwa pale kwa Afisa Utumishi anaambiwa subiri, subiri, subiri. Nashauri utaratibu huu uangaliwe upya ili tuwarahisishie walimu hawa wanapopata matatizo lakini pia matatizo yao yapogundulika hayapo basi warudishwe kazini haraka iwezekanavyo na stahili zao waweze kupewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande mwingine nataka nizungumzie kuhusiana na FDC. FDC kuanzia mwaka jana Mheshimiwa Waziri alituambia zimerudi kwenye Wizara yake. Hivi FDC (Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi) huko kwenye maeneo yetu vina hali siyo nzuri sana. Nichukue mfano wa Chuo cha Maendeleo ya Wanachi cha Malampaka kule kwenye jimbo langu kina miundombinu ambayo imezeeka sana. Mheshimiwa Waziri hiki Chuo cha Maendeleo ya Jamii kimetoka kilipokuwa middle school kikageuzwa kikawa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi. Kwa hiyo, majengo yake ni ya zamani sana, yamechakaa lakini haya hajakarabatiwa na samani zilizoko pale na zenyewe ni za zamani sana zingine zimevunjika, hazina thamani kama jina lake lilivyo. Hivi vyuo kwa sababu vimerudishwa kwake Mheshimiwa Waziri basi naomba aviangalie kwa maana ya kuvipatia vitanda na samani. (Makofi)

Mwenzangu ananikumbusha hapa, Chuo cha Maendeleo ya Wananchi cha Malya pia kina matatizo yale yale. Hiki chuo nachokizungumza cha Malampaka kina walimu wawili tu na kinatakiwa kiwe na walimu 26; hakuna usafiri na vifaa vya kujifunzia.

Sasa naomba Mheshimiwa Waziri anapojumuisha ajaribu kuviangalia hivi vyuo pia kwa sababu vimerudi kwake basi viweze kuwasaidia wananchi wetu huko tuliko. Maana vyuo hivi ndiyo mkombozi sasa kwa watoto wetu wale wanaomaliza form four wale wanaomaliza darasa la saba ili wajifunze elimu ya kiufundi na elimu mbalimbali iweze kuwasaidia kwenye maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimazilie kwa kusema ahsante sana kwa kunipa nafasi lakini pia naendelea kumshukuru pia Mheshimiwa Waziri kwa sababu amefanya juhudi kubwa sana kwa kweli hasa kwenye shule yangu ya sekondari ya Malampaka, tuna hali nzuri sasa hivi na tunaanza A-level, lakini kama alivyomtuma Katibu wake Mkuu alipofika pale aliahidi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante.