Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nampongeza Waziri na Naibu Waziri kwa kazi nzuri wanayofanya pamoja na timu yake kwa ujumla na hotuba yenye mtazamo chanya na iliyojaa matumaini mazima katika sekta ya utalii, pamoja na matumaini makubwa ya Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishauri Serikali yangu Tukufu katika suala zima la upandaji miti katika maeneo yote yaliyozungukwa na misitu pamoja na watu binafsi. Sambamba na hayo, pia tuna misitu iliyoungua, kwa mfano, misitu ya Wilaya ya Lushoto, imeungua toka mwaka 1994, lakini mpaka sasa misitu ile haijaota tena. Kwa hiyo, naishauri Serikali ipande miti maeneo hayo ya misitu iliyoungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Wakala wa Mbegu yaani TTSA na TAFORI. Wakala hawa ni muhimu sana, kwani hawa ndiyo watakuwa wakombozi katika kurudisha uoto wetu wa asili uliotoweka, lakini Mawakala hawa hawana mafungu ya kutosha, pamoja na vifaa vyao wanavyotumia ni vya zamani.

Kwa hiyo, naisisitizia Serikali yangu kama kweli ina nia ya dhati ya kupata miche kwa ajili ya kupanda miti katika nchi hii, basi wawape mafungu ya kutosha mawakala hawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia hawa TFS wanafanya kazi yao nzuri sana ya kuhakikisha misitu yetu haihujumiwi hovyo. Kwa hiyo, naiomba Serikali yangu iwawezeshe kwa vifaa vya kutosha, kama magari pamoja na ma-grader kwa ajili ya kuchimba barabara za msituni ili kurahisisha kupitika kwa haraka wakati wa majanga ya moto yanapotokea kuliko ilivyo sasa, tunategemea wananchi kuzima moto, pamoja na vifaa vya kuzimia moto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wana mwamko wa kupanda miti, lakini wananchi wanapangiwa kuvuna miti yao waliyopanda wenyewe. Naiomba Serikali iitoe sheria hiyo, kwani inakandamiza wakulima wa miti. Hii imekuwa ni kero kubwa sana kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali iwawezeshe vijana waliojiunga kwenye vikundi hasa katika Wilaya ya Lushoto, kuna vijana wamejiunga kwenye vikundi vya upandaji wa miti, lakini hawana support yoyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala zima la utalii katika Wilaya ya Lushoto; kama unavyojua, Wilaya ya Lushoto ina vivutio vingi kama malikale, milima yenye vivutio, maporomoko (waterfalls). Pamoja na hayo, Wajerumani waliishi sana Lushoto. Kwa hiyo, Serikali ifuatilie na itambue vivutio hivi ili tusikose mapato, kama inavyofanyika sasa kienyeji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hayo, wapo vijana wengi pale Lushoto wanaotembeza watalii. Naiomba Serikali yangu iwajengee uwezo na kuwatambua ili wasifanye kazi kienyeji na kuhakikisha mapato yanapita katika Serikali yetu pamoja na kuwajengea uwezo wa kuwaendeleza kielimu na kama siyo kufungua Chuo cha Kitalii Lushoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama inavyojulikana, Lushoto ni eneo lililozungukwa na misitu ya asili na misitu ya kupandwa, lakini barabara ya kuingia Wilaya ya Lushoto ni moja tu. Kama ilivyo sasa hivi, mvua zinazoendelea kunyesha zimesababisha uharibifu wa miundombinu ya barabara pamoja na madaraja. Hii imepelekea uchumi wa Lushoto kurudi nyuma pamoja na Serikali kukosa mapato kwani magari yanayopitisha mbao hayapiti, watalii hawafiki Lushoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kuna kilio kikubwa sana cha barabara katika Wilaya ya Lushoto. Kwa hiyo, Serikali lazima ichukue hatua za haraka kujenga barabara nyingine na mchepuo, ambayo inatakiwa ijengwe eneo la kuanzia Dochi kupitia Ngulwi hadi Mombo. Kwani ikijengwa barabara hii ya mchepuo itakuwa barabara mbadala na kumaliza tatizo la maliasili zetu kupita kwa uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mgogoro wa Ngorongoro, naomba niishauri Serikali yangu kuwajengea wafugaji wale mabwawa, visima na malambo ili kunusuru uharibifu wa hifadhi zetu unaotaka kutokea. Pia naishauri Serikali yangu iunde WMA katika eneo la Loliondo na kuwa na sheria kali za kusimamia eneo lile, kwani kuna vyanzo vya maji vinaharibiwa siku hadi siku na mwisho wa siku wananchi na wanyama wetu wa porini watakosa maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, tulinde, tutunze hifadhi zetu ili na sisi tuweze kurithisha kama waliopita walivyoturithisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.