Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Felister Aloyce Bura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Waziri, Mheshimiwa Profesa Maghembe na timu yake kwa kazi nzuri ya usimamizi wa maliasili ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Watanzania walio wengi hawajui umuhimu wa uhifadhi, faida za uhifadhi na kuwa hakuna somo la uhifadhi katika mitaala yetu na hata kwetu sisi Wabunge ni wachache sana waliowahi kutembelea mbunga za wanyama, malikale na kadhalika. Nashauri somo la uhifadhi liingizwe kwenye mitaala ili mtoto wa Kitanzania akue akijua umuhimu wa uhifadhi, kutunza misitu, malikale na kadhalika. Vijana wakiwa mashuleni wajifunze kupanda miti, kufuga nyuki na wawapende wanyama, kwa jinsi hiyo tunaweza kupunguza malalamiko mengi kutoka kwa wananchi kuhusu uhifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la utalii wa ndani kwa vijana wetu litiliwe mkazo. Kwa kufanya utalii wa ndani vijana watajifunza mengi na kuacha uadui na wanyamapori na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna migogoro ya ardhi na hasa mipaka ya vijiji na Hifadhi za Taifa, Mapori ya Akiba na kadhalika. Migogoro mingi huchangiwa na Serikali kutokuwa makini, wananchi hawalimi kwa siku moja ndani ya mapori, wanalima kwa miaka kisha wanajenga nyumba bora za kuishi, zahanati na shule bila Serikali kuchukua hatua yoyote. Ni vizuri Serikali ikachukua hatua mapema wananchi wanapovunja sheria za uhifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mtazamo wangu sioni sababu ya kuwepo kwa TTB. TTB haina vyanzo vya mapato, kazi zinazofanywa na TTB zinafanywa na TANAPA na NCAA. Ni halali mashirika hayo kuichangia TTB? TTB haiwezi kufanya kazi ipasavyo. Hata hivyo, tulielezwa kwenye semina kuwa vivutio vya Tanzania havitangazwi ipasavyo hii ina maana kwamba TTB wameshindwa kazi. TTB ni hasara kwa Taifa, ivunjwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Balozi zetu katika nchi mbalimbali kuwepo na kitengo cha utalii kitakachofanya kazi ya kutangaza vivutio vya Tanzania. Kwa kuwa TTB hawawezi kwenda kila mahali kutangaza vivutio vya Tanzania, Kitengo cha Utalii kwenye Balozi zetu kinaweza kufanya kazi nzuri yenye manufaa kwa nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, askari wanyamapori wanafanya kazi kubwa na yenye hatari kubwa ya kupambana na majangili, lakini wanalipwa mishahara midogo sana sawa na askari wanaofanya kazi kwenye maeneo yasiyo hatarishi. Pamoja na hayo wanafanya kazi kwa masaa mengi kwa sababu ni wachache. Serikali ieleze ni lini askari wanyamapori wataajiriwa wa kutosha na kupewa motisha ipasavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, misitu ya Tanzania haina mwenyewe, mtu yeyote na kwa wakati wowote anaweza kufyeka miti atakavyo na asichukuliwe hatua yoyote. Nchi zingine duniani mtu haruhusiwi kukata miti bila kibali cha Serikali. Serikali inafanya nini kulinda misitu ya nchi hii?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.