Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja asilimia mia moja. Sababu ya kuunga mkono hoja ni kutokana na mipango mizuri ya Serikali kwa wananchi wake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo la uwajibikaji na maadili ndani ya Serikali, naipongeza Serikali kwa jinsi inavyorejesha nidhamu ya utumishi wa umma. Mheshimiwa Rais na Waziri Mkuu wameonesha kipaumbele chao cha kupambana na mafisadi kwa kuwatoa kazini na kufanyiwa uchunguzi ambao umewezesha wengine kufikishwa Mahakamani, naipongeza sana hatua hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la ukuzaji wa uchumi kupitia mpango wa kufanya mapinduzi ya viwanda, naiomba Serikali pamoja na kuanzisha viwanda vipya, tuangalie na viwanda vyetu vilivyokuwepo zamani, viwanda vifuatavyo tuviangalie kwa umuhimu wake katika Jiji la Dar es Salaam:-
(i) Kiwanda cha Kubangua Korosho cha Mbagala - TANITA
(ii) Bora Shoes
(iii) UFI
(iv) Tanzania Cables
(v) Aluminium Africa
(vi) Metal Box
(vii) Metal Product
(viii) Urafiki Textile
(ix) Banda la Ngozi na viwanda vingine vingi ambavyo kwa sasa hakuna uzalishaji unaoendelea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu huduma za afya, naiomba Serikali iondoe dhana ya wagonjwa au majeruhi wanaopata ajali kupitia katika Hospitali ya Mkoa badala ya kupelekwa moja kwa moja Muhimbili. Nasema hivyo kutokana na ukosefu wa vifaatiba katika Hospitali za Temeke, Amana na Mwananyamala. Wagonjwa wanaopata ajali mara zote wanapoteza fahamu katika Hospitali za Mikoa na wanafika Muhimbili wakiwa mahututi au wamekufa kabisa. Naiomba Serikali yangu sikivu ibadili utaratibu huu usiwe wa lazima sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mazingira wezeshi; nashukuru Serikali kwa kuwaandalia vijana na akinamama, naipongeza Serikali kwa kuweka bajeti ya shilingi milioni 50 kwa kila Mtaa na Kijiji. Naiomba Serikali iweke mkazo wa kupeleka fedha maeneo yenye ujasiriamali. Maeneo yenye wingi wa vijana na wanawake ni pamoja na Mbagala, Mtoni, Tandika, Gongo la Mboto, Buguruni, Kariakoo, Ilala, Manzese, Mwenge, Kijitonyama, Tegeta, Ubungo, Bunju na Kibamba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo hayo yana wingi wa wananchi ambao wanahitaji kupata mitaji, naiomba Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kuangalia maeneo hayo kwa jicho la upekee.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kazi na hifadhi ya jamii, napongeza Wizara na Mheshimiwa Waziri wa Kazi, Mheshimiwa Jenista Mhagama, kwa jinsi alivyoendesha zoezi la kuwatoa wageni walioajiriwa nchini bila vibali, jambo alilolifanya ni kubwa na limesaidia sana. Naomba zoezi hili liwe endelevu kwa maslahi ya wananchi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti,naunga mkono hoja.