Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. INNOCENT S. BILAKATWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba ulinde muda wangu. Nakushukuru kunipa nafasi hii kuchangia. Kwanza nampongeza sana Waziri Mkuu kwa hotuba nzuri ambayo ameiwasilisha mahali hapa. Ni hotuba nzuri ambayo inaongelea kila kitu; hakuna mahali ambapo hakugusa. Kabla sijafika huko, kwanza naipongeza Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kutumbua majipu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema ni Serikali ya Chama cha Mapinduzi ndiyo inayotumbua majipu. Kwanza majibu yalianza kutumbuliwa pale walipoanza kukata jina la fisadi namba moja. Hili nalisema kwa sababu hao hao ndio waliosema ni fisadi, hatukuanzisha sisi.
MBUNGE FULANI: Kweli!
MHE. JOHN H. WEGESA: Kwa hiyo, naipongeza Serikali ya Chama cha Mapinduzi na nawapongeza Mawaziri, songeni mbele. Tuko nyuma yenu, tutapigana usiku na mchana mpaka kitaeleweka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Rais wetu kwa ujasiri mkubwa kwa kazi nzuri anayoifanya na Serikali nzima kwa ujumla. Niwaambie Waheshimiwa Mawaziri na Waziri wetu Mkuu, msiogope. Siku zote unapokwenda kwenye kituo cha mabasi au cha daladala, kuna watu wanaitwa wapiga debe. Siku zote wapiga debe huwa sio wasafiri. Waacheni wapiga debe wakapige debe, wanaosafiri wanajua wanakoenda. Sisi tunajua tunakoipeleka nchi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nijikite kwenye michango yangu. Naipongeza Serikali kwa jinsi ambavyo inajitahidi kukusanya mapato. Naiomba Serikali yetu, bado Watanzania wanahitaji elimu kuhusu kutumia hizi mashine za electronic. Ukienda maeneo mengi ya vijijini, hizi mashine hakuna. Tunapoteza mapato mengi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini kwa muda mfupi huu tuliotoka kwenye shilingi bilioni mia nane na kitu, kwenda kwenye shilingi trilioni 1.3 tunaweza kuvuka hata tukaelekea kwenye trilioni mbili.
Naomba tuongeze juhudi za kuwaelimisha Watanzania, kila tunachokinunua tupate risiti. Naiomba sana Serikali hasa katika suala la umeme, kuna maeneo mengine ambayo hawataweza kutumia mashine hizi; hakuna mitandao, hakuna umeme. Kwa mfano, kama kule kwetu Kyerwa, kuna maeneo mengi hakuna mitandao na hizi mashine hazitafika. Naomba Serikali ipeleke mitandao mahali ambapo hakuna mitandao ili tuweze kukusanya mapato mengi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nijikite kuipongeza Serikali; inasema tunaenda kwenye nchi ya viwanda; ili tuweze kufika kwenye nchi ya viwanda, kuna vitu ambavyo tunahitaji kwanza tuviangalie.
Kwanza, tuongeze nguvu kwenye umeme. Tunataka huu umeme wetu unaokwenda vijijini uweze kuwasaidia vijana wetu. Tunayo makundi mbalimbali, uzalishaji mkubwa uko vijijini; kilimo, kila kitu kinapatikana huko vijijini. Tukiweka umeme wa kutosha, tutaweza kufungua viwanda vidogo vidogo na vijana wetu ambao ndio nguvukazi wataweza kupata ajira. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali izingatie hayo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hilo tu. Tunayo mitambo mikubwa, tuna viwanda vikubwa, hivi viwanda vinahitaji kutumia umeme. Serikali ijikite kuongeza nguvu kwenye kuzalisha umeme, tunataka mitambo inayochimba madini iunganishwe kwenye grid ya Taifa. Itakapounganishwa kwenye grid ya Taifa, mapato yetu yataongezeka kwa sababu uzalishaji ambao wanatumia sasa hivi generator utapungua na mapato yataongezeka. Kwa hiyo, naiomba sana Serikali, tunao uwezo wa kuongeza umeme kwa sababu tayari tunayo gesi nyingi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine, tunaposema tunaenda kwenye uchumi wa kati, uchumi wa viwanda, ni lazima tuboreshe miundombinu yetu iwe mizuri. Huwezi ukasema utajenga viwanda wakati miundombinu haiko vizuri. Kwa mfano, kama kule kwetu Kyerwa tunazalisha kila kitu lakini barabara ni mbovu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba sana Serikali na Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, hili mliangalie. Kuna barabara inayotoka Murushaka kwenda Nkwenda mpaka Mulongo mpakani na Uganda. Hii barabara imesuswa kwa muda mrefu, lakini unapoongelea uchumi wa Kyerwa ni pamoja na barabara hii. Hii ndiyo namba moja Kyerwa. Naiomba sana Serikali iliangalie. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine, kuna hao wananchi ambao wanazalisha, kwa mfano, kama kule kwetu, kuna masoko ambayo yameanza kujengwa pale Nkwenda na Mulongo; haya masoko yamesahaulika. Serikali iliyajenga, yamefikia nusu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba sana Serikali, haya masoko yaendelezwe ili wananchi wawe na soko la uhakika. Siyo wanalima halafu wakishalima mazao yanaozea mashambani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba sana Serikali ijitahidi sana kuboresha miundombinu ili mazao haya yaweze kuuzwa mahali panapohusika. Mwananchi anapolima ajue nina uhakika wa kupeleka mazao yangu sokoni na kupata pesa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia maiomba Serikali hii ihakikishe inawakumbuka vijana wetu wa bodaboda. Hawa ni vijana wanaojiajiri, lakini hawa vijana wamekuwa kwenye mazingira ambayo siyo mazuri; vijana hawa wakati mwingine wanapata mateso mengi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti naiomba sana Serikali, kuwapa elimu hawa vijana na sisi wanasiasa ambao tuko humu Bungeni, tuwape elimu hawa vijana waweze kuwa na Bima ya Afya wapate matibabu. Vijana wengi wanapata ajali, wengine wanakatika miguu na mikono lakini hakuna Bima ya Afya. Mwingine hana pa kutibiwa!
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaweza tukaanzisha Mfuko hawa vijana wakawa na kitu kidogo ambacho wanaweka ili hata inapotokea, wanapopata ajali, anakuwa na pesa sehemu fulani ameiweka; siyo wanatumia tu. Wanahitaji elimu na nawaomba Wanasiasa wenzangu tuhakikishe hawa vijana wetu tunawapa elimu ili wajue ile ni ajira kama sisi wengine ambavyo tunajiwekea akiba na hawa vijana waweze kujiwekea akiba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo nilizungumzie, ili tuweze kufanikiwa haya yote ambayo tunayasema, tunahitaji kuboresha maslahi ya Watumishi wetu. Kuna watumishi wengine wanafanya kazi kwenye mazingira magumu. Mazingira yanakatisha tamaa. (Makofi)
Kwa mfano, kama kule kwetu Kyerwa kwenye Halmashauri, kuna gari moja tu. Hiyo gari ya Mkurugenzi, mara wanakwenda kwenye miradi; hawawezi wakafanya kazi vizuri. Kwa hiyo, naomba tuboreshe mazingira yawe mazuri waweze kufanya kazi vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, ili tuweze kwenda kwenye uchumi mzuri na maisha yawe mazuri, lazima Watanzania wapate maji safi na salama. Katika maeneo mengi hakuna maji. Tunaposema tunataka uchumi wa Mtanzania upande, ni pamoja na kuondoa hivi vitu ambavyo mnamfanya Mtanzania; kwa mfano, kuna mahali pengine mtu anakwenda kuchota maji masaa matano. Huyu mtu atafanyaje shughuli za maendeleo aweze kujipatia kipato?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, haya tuyaangalie. Naiomba sana Serikali, tunapofanya haya, tusiangalie sehemu moja tu, hawa ni Watanzania, wote wafaidi kile kidogo tunachokipata. Unakuta miradi inaelekezwa eneo moja tu. Tuelekeze maeneo yote, tugawane kidogo, mwisho wa siku wote tufanikiwe maana wote ni Watanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba sana Serikali, suala la afya ni muhimu. Namwomba Waziri Afya, Kyerwa hatuna Hospitali ya Wilaya, lakini hata vile Vituo vya Afya vilivyopo havina madawa, naamini hii ni Serikali sikivu; na majipu haya ambayo wenzetu wa upande wa pili waliyapandikiza, tumewagundua, tunayatumbua kila siku; yanaondoka. Tunaamini wao ndio wanayapandikiza kwa sababu tunapoanza kuyatumbua, tunaona wanalalamika, maana wale ni wenzao. Kwa hiyo, tutaendelea kuyatumbua na Serikali imejipanga vizuri tutapata Watumishi waaminifu ambao hawakupandikizwa. Serikai hii itapaa sana!
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naishukuru Serikali yangu na naamini ni sikivu. Kwa hayo machache, naunga mkono hoja.