Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze mchango wangu kwanza kwa kumshukuru Mwenyenzi Mungu kwa kuniwezesha kushika kalamu na kutoa mchango wangu kwa njia ya maandishi.

Kwanza kabisa naomba kuchangia juu ya Wakala wa Uhifadhi na Uvunaji wa Mazao ya Misitu (TFS). Taasisi hii imekuwa ni mzigo kwenye Halmashauri zetu, badala ya kuwa taasisi ya uhifadhi yenyewe inaongoza kwa kuharibu misitu vilevile mahusiano ya taasisi hii na jamii au Halmashauri zetu siyo mzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, taasisi hii imekuwa haitoi elimu ya kutosha kwa jamii juu ya uvunaji endelevu wa misitu badala yake imekuwa ikiwalinda wavunaji haramu kwa faida ya watendaji wa taasisi. Mfano mzuri ni katika Halmashauri yangu ya Liwale katika Wilaya ya Liwale kuna hifadhi mbili za misitu, kuna msitu wa Angai ambao unahifadhiwa na vijiji 24, na msitu wa Nyera-Kipelele, huu ni msitu wa kitaifa lakini hadi leo msitu wa Nyera - Kipelele bado uvunaji haujafanyika. TFS wanasema mwongozo wa uvunaji haujakamilika lakini wavunaji haramu wanavuna kila kukicha bila ya wahusika kuchukua hatua za kuzuia ujangili huu. Kwa ule msitu wa vijiji bado vijiji havina elimu ya kutosha juu ya uvunaji endelevu jambo linalochangia kwa kiasi kikubwa upotevu wa mapato katika vijiji husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kukosekana kwa uwakilishi wa Mbunge na Madiwani katika Kamati ya Uvunaji wa Rasilimali za Misitu kunaongeza mwanya wa wizi wa mali za misitu. Kamati hii huongozwa na Wakuu wa Mikoa. Je, kuna siri gani inayofanya Meya na Wabunge washindwe kualikwa kwenye Kamati hizi ikiwa wao ni wawakilisi wa wananchi? Vilevile makato ya asilimia tano yanayotengwa kwenye Halmashauri zetu ni kidogo mno kulinganisha na uharibifu wa misitu hiyo, Halmashauri zetu hutegemea misitu katika kukuza uchumi wake, hivyo naishauri Serikali kuangalia upya viwango hivyo ili kuviboresha na kuziongezea uwezo Halmshauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee Pori la Akiba la Selous. Hifadhi hii ni kubwa sana hapa Barani Afrika na duniani kwa ujumla na sehemu kubwa ya hifadhi hii iko Wilayani Liwale, cha kusikitisha hakuna miundombinu yoyote iliyojengwa Liwale katika kuhudumia hifadhi hii. Hata barabara ya kuingia katika hifadhi hakuna, lango la kuingia kwenye hifadhi hii kwa watalii liko Mikumi Mkoani Morogoro jambo linalowanyima fursa za ajira kwa wakazi wa Wilaya ya Liwale na Mkoa wa Lindi kwa ujumla. Hivyo, naiomba Serikali kufikiri kufanya uwekezaji wa kutosha ili wale wanaozungukwa na hifadhi hii waone faida ya kuwa na hifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Mamlaka ya Wanyamapori, pamoja na nia nzuri ya Serikali ya kuanzisha mamlaka hii, utendaji wake bado siyo wa kuridhisha, bado kuna usiri mkubwa na ushirikiano na jamii zinazozungukwa na hifadhi siyo nzuri. Mfano katika Halmshauri yangu ya Liwale hadi leo hatujui hatma ya mgao wetu wa asilimia 25 ya mapato yatokanayo na uwindaji wa kitalii. Hatujui tunayapataje, ukiwauliza wahusika hawana majibu ya kuridhisha zaidi ya kukatisha tamaa. Kitendo cha kuficha taarifa za mapato na kuacha kuweka wazi stahiki za Halmashauri zetu hakioneshi au kinapingana na malengo ya kuundwa kwa taasisi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa sekta ya utalii kwa Kanda ya Kusini bado vivutio vingi havijatangazwa vema au vimesahaulika kabisa. Ukanda wa Pwani ya Bahari ya Hindi katika Mikoa ya Pwani, Lindi na Mtwara kuna vivutio vingi havijatangazwa. Mfano, Boma la Mjerumani lililoko Liwale, Kaburi ya Mzungu (Mfaransa) lililoko Mikukuyumbu- Liwale. Kaburi la Bibi aliyesadikiwa kuwa ni Sharifu katika uhai wake lililopo katika kijiji cha Ndapata - Liwale. Vilevile kuna viboko wanaowasiliana na wazee wa kimila walioko Kilwa, pamoja na maji moto yaliyopo katika Mto Rufiji. Hivi vyote ni vivutio vya utalii vilivyosahaulika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu migogoro ya mipaka, kuna mgogoro wa muda mrefu wa mpaka wa kijiji cha Kikulyungu na Hifadhi ya Selous, mgogoro huu umeshachukua roho za watu wanne, ni bora sasa mgogoro huu ukapatiwa ufumbuzi ili amani na usalama vikarejea baina ya jamii na wahifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fidia kwa ndugu Abilahi Njonjo, huyu ni mwananchi aliyejeruhiwa na Askari wa wanyamapori kwa kupigwa risasi kusababisha akatwe mkono. Taarifa zake ziko Ofisi ya Katibu Mkuu wa Wizara akilalamikia namna ya kupata hicho kinachoitwa kifuta machozi ni miaka miwili sasa tangu amekatwa mkono.