Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii kwa hotuba nzuri. Hongera Mheshimiwa Waziri kwa hotuba madhubuti. Wizara hii ni miongoni mwa sekta kiongozi katika ukuaji wa uchumi wa Taifa la Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninampongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa namna ya pekee na kwa namna anavyofanya kazi na kuonesha ushirikiano mkubwa kwetu sisi watu wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe, hasa kuhusiana na hatua mbalimbali za uendelezaji wa Mapori ya Akiba ya Kigosi Moyowosi. Pori la Akiba la Kigosi Moyowosi ni pori zuri sana, hata hivyo liliachwa bila uangalizi madhubuti, matokeo yake pori hili likavamiwa na makundi makubwa ya ng’ombe wa ndani na wengine kutoka nchi jirani, hasa nchi ya Rwanda na Burundi.

Mheshimiwa Spika, kutelekezwa kwa Pori hili la Akiba la Kigosi Moyowosi kulisababisha miundombinu yake kukosekana, barabara katika pori hili ndio uti wa mgongo wa ulinzi na usalama kwa pori lenyewe na wanyama wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokuwepo kwa barabara za kudumu ndani ya pori hili kumedumaza maendeleo ndani ya pori hili, matokeo yake mwanya unapatikana kwa majangili kuua wanyama, uvamizi wa wakulima na wafugaji na wahamiaji haramu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwanja wa ndege ndani ya Pori la Akiba la Kigosi Moyowosi ni chachu ya ukuzaji wa utalii ndani ya pori hili. Kiwanja cha ndege kifufuliwe, ili kiwe kiungo muhimu na Hifadhi za Taifa za Mahale na Gombe, pia Rubondo National Park. Hongera Mheshimiwa Waziri kwa uamuzi wako wa busara wa kuonesha nia ya kulipatia Pori la Akiba la Kigosi Moyowosi magari mawili kwa ajili ya uendelezaji wa shughuli za utawala na ulinzi wa pori lenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ameonesha nia ya kulikarabati grader lililopo Kifura ili lifufuliwe na kuanza kutumika kufungua barabara ndani ya pori hili. Nakuunga mkono Mheshimiwa Waziri, songa mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuanzishwa kwa Mamlaka ya Wanyamapori (Tanzania Wildlife Authority – TAWA), ni hatua muhimu sana katika kuyaunganisha na kuyasimamia mapori yote ya akiba nchini. Ninaamini hatua hii itaongeza ufanisi kiutendaji kama ilivyo kwa TANAPA na Ngorongoro Conservation Area Authority na kwa mantiki hiyo, mchango wa mapori ya akiba nchini, chini ya TAWA kuongezeka katika Pato la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu wa mwisho ni kuhusu uanzishwaji wa Game Rangers ndani ya Pori la Akiba la Kigosi Moyowosi na kufungua barabara ndani ya pori hili. Mungu ibariki sana Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.