Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Awali ya yote namshukuru sana Mwenyezi Mungu kama wasemavyo wahenga kwamba kila kiongozi basi anakuwa na baraka za Mwenyezi Mungu. Kwa kusema hivyo, naomba nimpongeze sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye mimi nasema wazi kwamba ni chaguo la Mwenyezi Mungu na ni chaguo la Mwenyezi Mungu kutokana na uthubutu wake hasa kwa tukio kubwa leo hii ambalo amelithibitishia Taifa la Watanzania ni kwa jinsi gani kwa muda mrefu tumekuwa tukiibiwa madini yetu na sisi Watanzania tukiendelea kuwepo katika limbwi kubwa la umaskini. Kweli huyu ni chaguo la Mwenyezi Mungu, nampongeza sana kwa uthubutu wake, kwa kile ambacho amedhihirisha leo hii, basi yale aliyokuwa akiyafikiria, kwamba ni kweli, kwa hili tuzidi kumuombea Mwenyezi Mungu ampe maisha marefu ili aweze kuyabaini mengi na hatimaye Watanzania wafurahie rasilimali zilizopo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nichukue pia nafasi hii kuipongeza Wizara, nampongeza Waziri, nampongeza pia na Naibu Waziri, niwapongeze pia na Wakurugenzi wa TANAPA, lakini pia Mhifadhi Mkuu wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro, pamoja na changamoto zote hizo na lawama nyingi lakini kazi wanayofanya ni kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba kwa nini naipongeza Serikali na naipongeza pia Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro, kwanza kwa hatua yake ya mfumo mpya wa kielektroniki wa kukusanya maduhuli, ambao unaitwa NCAA Safari Porto ambao umeonyesha ni kwa jinsi gani wameweza kukusanya shilingi bilioni 81 hii ni faraja kwetu, kwa maana kwamba endapo katika maeneo mengi kuhakikisha kwamba mfumo huu unafanya kazi pesa zitakazo ingia katika sekta ya utalii zitakuwa ni nyingi na zitaweza kusaidia kutatua changamoto mbalimbali zilizopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niishauri Serikali na niseme tu kwamba uzuri wa Bonde la Ngorongoro na sababu ya Ngorongoro kuingia katika maajabu saba ya dunia ni kutokana na upekee kwamba wanyama pamoja na binadamu wanaishi pamoja na kwa maana hiyo basi pamoja na changamoto mbalimbali zilizopo mimi naishauri tu kwamba Wizara itekeleze maagizo ya Waziri Mkuu ya kuhakikisha kwamba katika Bonde la Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro wanatenga maeneo ili mifugo isiingie katika bonde lile na badala yake waende kunywesha maji katika maeneo hayo ambayo yatakuwa yametengwa tofauti na hivi sasa kwamba ndio tunataka kuwaondoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiwaondoa pasipokuwa na mbadala, je, tumewasaidia kweli hawa wananchi? Kwa hiyo tutimize tu hili agizo la Waziri Mkuu kuhakikisha kwamba tunatenga maeneo na hayo maeneo basi hao wafugaji watakwenda kunywesha mifugo yao na badala yake hakutakuwa na mifugo itakayoingia katika Bonde la Hifadhi ya Ngorongoro kwa sababu uzuri wa Ngorongoro ni ile Crater yenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine pia ambalo napenda niishauri Wizara, kwa mfano siku ya Jumapili hapa kulikuwa na semina na tulielezwa ni kwa jinsi gani ambavyo baadhi ya wanyama wapo hatarini kupotea, na hii ni kutokana na muingiliano kati ya binadamu na hao wanyama. Ni kweli nakumbuka siku za nyuma ukiingia tu eneo la Monduli ulikuwa unakutana na wanyama wengi katika maeneo hayo, lakini hivi sasa hakuna na hii inaonyesha kwamba ni kweli ni kutokana na muingiliano baina ya binadamu na wanyama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sasa pamoja na yote hayo kama kweli katika hifadhi zetu, kama kweli katika mfano Bonde la Ngorongoro tunataka kweli wale wanyama waendelee kuwepo kule tuhakikishe kwamba hata haya magari yenyewe mfano, msimu wa utalii kwa siku zinaingia mpaka gari 200. Sasa Serikali iangalie jinsi gani itaweza kupunguza hayo magari na hata ikiwezekana pamoja na kwamba tozo la kodi lipo basi tuone uwezekano wa kuweka tozo kubwa ili magari yasiingie kwa wingi kule na badala yake tuendelee kuhifadhi mazingira tofauti na hivi sasa ambapo magari ni mengi sana katika Crater ya Ngorongoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine pia tunafahamu kwamba Serengeti, hifadhi zilizopo Kaskazini ndizo ambazo hasa kwa kiasi kikubwa zinasaidia hata kuendesha hizi hifadhi nyingine, lakini ni pengine ni kutokana na miundombinu ambayo ipo katika maeneo hayo. Katika hizi hifadhi nyingine ambazo zipo naishauri Serikali kuhakikisha kwamba inaboresha miundombinu ili basi hifadhi hizi ziweze kufikika kwa urahisi na watalii waweze kwenda kule, lakini pia kuhakikisha kwamba inatangaza vivutio vingi ili watalii waweze kufahamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano ukienda Kigoma kuna hifadhi ya Gombe na Mahale na kwa bahati nzuri hifadhi hii ina chimpanzee ambao katika hifadhi nyingine ni vigumu sana kuwapata. Sasa watalii wengi wanashindwa kufika kule kutokana na miundombinu ambayo sio rafiki. Kwa maana hiyo endapo tutaboresha miundombinu na kuhakikisha kwamba wanafika kule kwa urahisi na kwa bahati nzuri hivi sasa tunayo bombardier ambayo inakwenda kule, lakini je, katika kwenda huko Gombe na Mahale miundombinu ikoje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunawahamasishaje watalii ili waweze kufika huko hii ikiwa ni pamoja na kutangaza zaidi na hata kwa kutumia vyombo vyetu vya humu ndani lakini pia vyombo vya nje kama ambavyo kwenye ripoti yenu mmeonyesha. Kwa kufanya hivyo tutaweza katika hifadhi zetu kupata watalii wengi zaidi na kuingiza pato kubwa kwa Serikali yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia utalii sio kwamba ni hifadhi tu, utalii hata majengo ndio maana Zanzibar wanakwenda kule kwa sababu ya Mji Mkongwe wa Zanzibar. Ukienda katika Jiji la Dar es Salaam mfano Posta ni eneo ambalo lingefaa sana ule mji badala ya kuubomoa yale majengo ya zamani, majengo yale tungeyaacha ili uwe ni mji ambao utakuwa ni kumbukumbu. Tofauti na hivi sasa tunabomoa majengo yale ya zamani na kujenga majengo mapya, tupanue kwa kwenda katika maeneo mengine ambayo yatatengwa ili basi tuweze kujenga zaidi na hata kuwekeza vivutio zaidi ambavyo vitawavutia wawekezaji na sio kubomoa tu yale majengo ambayo ni majengo yamekuwepo kwa muda mrefu na majengo hayo tunayapoteza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Zanzibar wangeweza kufanya hivyo leo hii kusingekuwa na watalii wengi ambao wanakwenda, umebaki kuwa ni mji wa kihistoria, Mji Mkongwe wa Zanzibar. Kwa hiyo, mimi naishauri sana Serikali kuhakikisha kwamba inazingatia haya lakini kubwa zaidi ni kuhakikisha kwamba miundombinu inawezesha watalii wengi kuweza kufika kule. Lakini pia katika huu mfumo unaotumika na Ngorongoro tuhakikishe kwamba tunaongeza mashine katika lile eneo la geti pale ili kuepuka ule mrundikano wa watalii wanapofika pale kwa wingi, kwa sababu wakati mwingine mtalii anapokuja yeyeanataka afike pale amalize zile taratibu mara moja aweze kuingia, lakini matokeo yake anafika pale anapanga foleni kwa kweli inakuwa ni usumbufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tuangalie ni jinsi gani mzee wetu Maghembe pale kwamba tunaboresha vipi kwa kuweka kama ni hiyo mifumo ya kielektroniki inakuwepo ya kutosha ili wanapofika pale kusiwepo na huu usumbufu, lakini kwa wale ambao wanasema kwamba tozo hizi za kodi kwamba zimesababisha watalii...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante.