Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Mohamed Omary Mchengerwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Rufiji

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi nikushukuru kwa kunipa fursa. Awali ya yote nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia afya njema, nawashukuru sana wananchi wangu wa Jimbo la Rufiji kwa kuendelea kuniombea dua hususani katika kipindi hiki ambacho ni kipindi kigumu kabisa kupata kutokea kwa wananchi wa Mkoa wa Pwani hususani wakazi wa Kibiti, Rufiji na Mkuranga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii kwa kufanya kazi nzuri kabisa katika Wizara hii ambayo ni moja ya Wizara ngumu kabisa katika nchi yetu hii. Mheshimiwa Waziri yeye pamoja na timu yake wamefanya kazi nzuri na mimi nawapongeza sana, sisi wananchi wa Rufiji wametusaidia kwa mambo kadhaa ambayo nitayazungumza hapo mbele lakini pia nimpongeze Mkurugenzi yule wa Misitu Ndugu Mohamed, nimpongeze Meneje wetu wa TFS kutoka kule Rufiji ambae marazote amekuwa akitatua kero za wananchi wangu na mimi namfananisha Profesa Maghembe na kanuni ya kwanza ya uongozi iliyowahi kutolewa na Dkt. John Maxwell ambae aliwahi kuandika kitabu chake The Laws of the Leadership akisema kwamba; “Personal and organizational effectiveness is proportional to the strength of a leadership” na mimi namuona yeye kama ni kiongozi ambaye ameweza kuimiliki Wizara hii na ninaamini Rais Dkt. John Pombe Magufuli wakati anakuteua aliamini wewe ni muadilifu na umechapa kazi. Wizara hii ina madudu mengi sana na kama ungekuwa umeyumba kidogo basi Wizara hii kwa kweli ingekushinda mapema sana.

Lakini nikupongeze kwa kusimamia Ibara ya 26 ya Katiba na kumtaka kila Mtanzania kusimamia na kufuata sheria za nchi yetu na hii nimeiona kwasababu wakati wa mijadala ya Wizara hii ya Maliasili na Utalii tumeona hoja nyingi zinazoibuka ni hoja zilizopo kwenye Wizara ya Kilimo na Mifugo na ni wewe sasa umekuwa kama Waziri wa Kilimo na Mifugo lakini pia umekuwa kama Waziri wa Ardhi na umeendelea kuchapa kazi na mimi naomba niwakukmbushe Wabunge wote wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakumbuke kwamba Ibara ya 26(2) inatupa mamlaka sisi Wabunge iwapo tunaona sheria yoyote ambayo inasimamiwa na Profesa Maghembe sheria ile inakinzana na matakwa ya nchi yetu tuliyonayo sasa basi ni vyema Wabunge sasa tukaleta sheria ile ndani ya Bunge lako hili tukufu kupitia Ibara ya 64 ya Katiba ili tuweze kubadilidha sheria ile na tusimlaumu Profesa Maghembe kwa kuwa anasimamia Ibara ya 26 ya Katiba ya kusimamia na kufuata sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, magazeti mengi ya wiki hii yameandika mambo mengi kuhusu Rufiji, Kibiti na Mkuranga. Gazeti la leo la Citizen limeandika taarifa kwamba; “Why Rufiji residents are reluctant to cooperate over murders” lakini gazeti la jana ninalo hapa limeandika taarifa kwamba; “Rufiji families pain after losing their lovely ones.”

Jana mmoja wa wahanga aliyepigwa risasi siku tatu zilizopita amefariki jana alipigwa yeye na baba yake, yeye lipigwa risasi ya tumbo na jana amefariki na tunamshukuru Mbunge wa Kibiti kwa kufanya kazi nzuri ya kuhakikisha kwamba mwili ule unafika Kibiti na shughuli za maziko zinaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nikuhakikishie katika Bunge lako hili tukufu, unao Wabunge watatu ambao wanaishi katika maisha magumu sana kupata kutokea katika nchi hii; Mbunge wa Mkuranga, Mbunge wa Kibiti pamoja na Mbunge wa Rufiji. Tunaishi katika maisha magumu sana na siyo sisi tu hata katika familia zetu, lakini pia hata wapiga kura wetu wanaishi katika maisha magumu sana. Wananchi wamekonda sana hawawezi hata kushiriki katika shughuli za maendeleo hali ni mbaya sana na tunaiomba Serikali jambo hili kulifanyia kazi haraka kwasababu jambo hili linaendelea kutanuka na jambo hili siyo dogo kama ambavyo Wabunge wengine wanaweza kufikiria hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wengi wamekuwa wakihoji maswali ni kwa nini Wabunge hawazungumzi ndani ya Bunge? Tunafanya hivi kwa makusudi kabisa lakini tunataka wananchi wetu wajue tunafanya kazi kubwa kuhusiana na jambo hili lakini yapo mambo sisi hatuwezi kuyazungumza kwenye Bunge hili.

Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani wananchi wangu wa Ikwiriri wanakushukuru sana kwa kufika, kujionea familia ambazo ziliathirika ambazo waume zao wamepigwa risasi na kufariki, wananchi wangu wanakushukuru sana. Lakini nataka niseme Serikali isikie na Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli ajue kwamba mambo haya yanayotokea hayatokei kwa bahati mbaya, mambo haya yana root cause, mambo haya yamepangwa, tunataka Serikali ijue hilo. Yapo mambo mengi, zipo chuki nyingi ambazo zimejengwa kwa wananchi, zipo chuki nyingi, yako mambo mengi ambayo yalifanyika yanatoa kero kubwa kwa wananchi ndiyo maana hata gazeti la leo lilipoandika taarifa hizi mimi siashangaa sana kwasababu ninajua kwamba yako mambo ambayo Serikali sasa inapaswa kuyafanya na inatakiwa iyafanye sasa wala isisubiri kwa sababu jambo hili ni kubwa na linaendelea kutanuka kutoka sehemu moja kwenda sehemu nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo mimi naomba katika miongoni mwa mambo ambayo sisi tunaendelea kumpongeza Rais wetu ni terehe 31.03.2017 Rais Dkt. John Pombe Magufuli baada ya kufanya kikao chake na Waziri Mkuu wa Ethiopia alikubali kuwasaidia Watanzania kwa kuonyesha dhamira ya kujenga Stigler’s gauge iliyopo kule Rufiji ili wananchi wetu waweze kupata umeme wa uhakika kwani tunaamini kabisa miongoni mwa kero kubwa za wananchi wangu ni kutokuwa na umeme kwa takribani miaka miwili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu ni mwaka wa pili sasa wananchi hawana umeme wa uhakika sasaa hizi ni miongoni mwa kero kubwa ambazo wananchi wangu wanazo na leo nazungumza kwa uchungu kabisa, kero hizi muunganiko wa umeme ni kilometa nane tu lakini Waziri wa Nishati na Madini ameshindwa kutuunganishia umeme kwenye Gridi ya Taifa kwa miaka mwili wananchi wa Kibiti, wananchi wa Rufiji na wananchi wa kutoka kule Kilwa hawapati umeme wa uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunampongeza Mheshimiwa Rais kwa kuliona hili na tunaamini kabisa kwamba uzalishaji wa umeme upo kwenye Stigler’s gauge utasaidia upatikanaji wa umeme katika maeneo mengine hiyo ni miongoni mwa kero kubwa tulizonazo kwasababu tatizo hili ni kero kama nilivyosema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lipo tatizo la barabara ambalo Mheshimiwa Rais amekubali kutujengea barabara yetu ya Nyamwage kwenda Utete na mimi naomba nimpongeze na ninaomba wananchi watambue kwamba kero hii ya barabara imepatiwa ufumbuzi nasema haya kwa sababu ya kiini cha tatizo tulilonalo, wananchi wanalalamika sana na hatuna sababu ya kwa kweli kwa nini tuendelee kukaa kimya.

Nikuombe sasa Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii nirejee kwako, zipo kero katika maeneo yetu. Kwa mfano, katika Kata ya Kipugira watu wako wanaweka GPS kwenye nyumba za wananchi wetu, lakini naomba niikumbusghe Wizara yako kwa kusimamia Katiba; Ibara ya 16 ya Katiba inatoa uhuru wa faragha, lakini swali hili nilimuuliza Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii ni kwa nini Wizara yako inaweka GPS kwenye nyumba za wananchi wangu? Wanavunja ibara ya 16 ya Katiba ambayo inatoa haki ya faragha ambayo kila mwananchi anayo haki ya ku- enjoy haki ya faragha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimuombe Mheshimiwa Waziri ukisimama hapa unipe majibu kuhusiana na jambo hili ni kwa nini Wizara yako sasa inakiuka Ibara ya 16 ya Katiba lakini pia nimuombe Mheshimiwa Waziri akisimama hapa atuelezee tarehe 9 Septemba Waziri Mkuu alifika Rufiji na katika maeneo aliyokwenda ni pale Utete na alijionea wananchi walikuwa na malalamiko mengi sana. Upo msitu wa Kale ambao wananchi wa Utete pamoja na Chemchem wamekuwa wakiutumia kwa kilimo kwa miaka mingi sana.

Mheshimiwa Waziri naomba nikukumbushe nafahamu kuna tamko la Waziri Mkuu la upimaji upya wa maeneo yetu, lakini tukumbuke kwamba michoro ya awali ambayo Wizara yako inatumia ni michoro iliyochorwa na wakoloni mwaka 1936. Nikuombe Mheshimiwa Waziri utambue dhamira ya wakoloni ya kuchora michoro ile ni kwa sababu population ya Tanzania ilikuwa bado ni ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati ule wa mkoloni tulikuwa tunazungumzia population ya watu milioni nane mpaka milioni 10. Lakini leo hii Mheshimiwa Waziri tuna watu zaidi ya milioni 55 na Rufiji wakati ule tulikuwa kuna watu ambao walikuwa hawazidi hata 20,000; 30,000, lakini leo hii tunapozungumza tuna wananchi zaidi ya 200,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe ulisimamie hili, lakini hii ni pamoja na Kata yangu ya Mbwala katika vijiji vya Nambunju pamoja na Kitapi, maeneo haya yote Wizara yako imeanza kuyapima upya na Wizara sasa inachukua maeneo yote ambayo wananchi walikuwa wakiishi na kutaka kuyafanya maeneo yale ya misitu. Nikuombe Mheshimiwa Waziri uzingatie hili kwani ukichukua maeneo haya wananchi hawatakuwa na pa kwenda kabisa. Nikuombe ulisimamie hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo lingine kuhusiana na hotel levy; kodi hii ya hotel levy ambayo imekuwa ikitolewa kwenye nyumba za kulala wageni, kodi hii ni kero kubwa sana. Tukuombe sasa Wizara yako iweze kulingalia kulipitia kwani wananchi wanaomiliki nyumba hizi za wageni wanalipa shilingi 100,000 ya leseni kwenye Halmashauri, lakini pia wanalipa hii hotel levy. Wakati huo huo wanalipa tena kodi ya mapato TRA shilingi 560,000, wakati huo huo wanalipa hotel levy, wanalipa tena leseni, wanalipa gharama kubwa sana. Wananchi wangu kuanzia Jaribu Mpakani kwenda moja kwa moja Kibiti mpaka kule Mkuranga na Rufiji wanalalamika sana kuhusiana na kodi hii. Na nikuombe Mheshimiwa Waziri basi muweze kuingalia na kuweza kuona namna gani mtaweza kuitatua suala hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija pia katika suala zima la mahusiano kati ya Wizara yako na wananchi wetu wanaozunguka vijiji, nikuomba Mheshimiwa Waziri sasa ukija kujibu hapa ueleze mkakati wako wa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Naunga mkono hoja.