Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Jerome Dismas Bwanausi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lulindi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. JEROME D. BWANAUSI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kukushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika hotuba ya Waziri wa Maliasii na Utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze tu kwa kumpongeza sana Profesa Maghembe; Naibu Waziri, Injinia Makani; Katibu Mkuu na Watendaji wa Wizara kwa kuanza kuonesha sura mpya ya Wizara na kuanza kuleta matumaini mapya kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuishauri Wizara, Mheshimiwa Waziri Profesa Maghembe na wenzake kwamba juhudi zinazoendelea hivi sasa za kutatua migogoro walioyoikuta ziongezwe kasi ili kuwe na mahusiano mema kati ya Wizara na wananchi katika maeneo mbalimbali hapa nchini. Pia niitahadharishe Wizara siyo vema kuanza kutafuta migogoro mipya kwenye maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakala wanaoshughulika na mambo ya misitu wamepewa jukumu la kwenda kutathmini mipaka ya hifadhi za misitu, lakini nimwombe na kumkumbusha tu Mheshimiwa Waziri kwamba zoezi hili halikuwa limefanyika kwa zaidi ya takribani miaka 20 iliyopita,
kinachotokea hivi sasa ni baadhi ya maeneo kuanza kuzalisha migogoro kutokana na zoezi hili. Mheshimiwa Waziri nitolee mfano tu kwenye Jimbo langu la Lulindi tunayo hifadhi ya msitu ya Njawala, lakini tunavyo vijiji vinavyozunguka katika eneo hili, ambavyo Vijiji hivi vya Njawala, Mchoti na Mtona ni vijiji ambavyo vipo tangu miaka 20 iliyopita, katika zoezi hili vijiji vile vinaambiwa vimo ndani ya msitu, sasa inaleta kero kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anahitimisha basi ni vizuri kueleza wataalam wetu wasiende kuanzisha migogoro mipya. Nilipokuja katika Bunge hili nimemletea Mheshimiwa Waziri barua na wamenituma nimwombe Mheshimiwa Waziri baada ya Bunge atembelee maeneo ya Jimbo la Lulindi ili akajionee hali halisi katika maeneo haya, naamini atanikubalia ili tukayasikilize na kuyatatua matatizo haya tukiwa kule site. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo ningependa kulichangia ni tatizo kubwa sana la wanyama hatarishi na wanyama ambao wanawadhuru wananchi. Tangu niingie katika Bunge hili 2010 nimekuwa nikilalamika sana juu ya Wizara kutotilia maanani matatizo yanayotokana na mamba wanaoshambulia wananchi katika Jimbo langu la Lulindi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuliwahi kufanyika utafiti kama miaka minne iliyopita na utafiti ulifanywa na wenzetu wa Wizara ya Maliasili, wakabaini kwamba katika Mto Ruvuma hasa eneo langu la Jimbo la Lulindi, mamba ni wengi zaidi ya 300 wapo katika eneo lile. Kulitolewa ahadi, ya kuwapunguza mamba wale lakini kwa masikitiko makubwa katika miaka minne tu wananchi wa Jimbo langu na Watanzania 35 wameshapoteza maisha na zaidi ya watu 50 wamekwishajeruhiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua tunayo Taasisi ya Utafiti ya Wanyamapori (TAWIRI), nichukue fursa hii kuilalamikia sana TAWIRI, najiuliza labda makao makuu yapo mbali sana na Mtwara yako Arusha, katika kipindi chote cha Ubunge wangu sijawahi kuwaona TAWIRI wakija kutembelea maeneo yaliyoathirika katika Majimbo yetu. Kikubwa ambacho wanakatisha tamaa ni kwamba sisi tunasikiliza maelekezo yanayotolewa na Shirika la Wanyama Duniani kwamba lazima tuwalinde wanyama wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimwombe Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anahitimisha hebu awape matumaini wananchi wale ambao wanaishi kandokando ya Mto Ruvuma, vijiji hivi ni vijiji vya ulinzi, kuna Vijiji vya Mapili, Mduhe, Maparawe, Mkoo, Sindano na Mgwagule wananchi hawa katika kipindi chote hiki wameishi kwa maisha ya shida mno. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeshafika ofisini kwa Mheshimiwa Waziri mara nyingi na tumezungumza, kwamba moja ya suluhisho la kuwasaidia wananchi wale ili wasiathirike na tatizo la mamba ni kupunguza idadi ya wananchi wanaokwenda kuchota maji na huduma zote za maji kutoka kwenye mto ule. Tunao mfuko hapa unaoshughulika na wanyama pori, tunayo mifuko mingi inayoshughulika na wanyama pori, inazo fedha, kwa nini Wizara isihakikishe kwamba inasaidia vijiji vile kupata maji ili tupunguze idadi ya watu wanaokwenda kutumia maji kutoka Mto Ruvuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namfahamu Mheshimiwa Profesa Maghembe, Naibu Waziri Engineer Makani na Katibu Mkuu kwamba ni wasikivu sana, naamini atakapokuwa anahitimisha kwenye hotuba yake atawaambia ndugu zangu wale Lulindi ni jinsi gani Wizara yake itakavyolichukulia suala hili kwa uzito mkubwa na kuhakikisha katika bajeti hii ya 2017/2018, tunatenga fedha kwa ajili yakuchimba visima vinane kwenye vijiji hivi ili kuwasaidia wananchi wale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sitaacha kusema aliyosema aliyetangulia kutoa maoni yake. Mheshimiwa Waziri hili tamko tunalotaka kuendelea kupewa msisitizo la kuzuia mkaa kutoka eneo moja kwenda lingine ni lazima litazamwe upya. Bado hatujafika wakati ambapo nishati mbadala zinaweza kutosheleza badala ya mkaa. Namwomba sana hili jambo la kuhifadhi misitu ni jambo muhimu sana, nakubaliana nalo sana kwa asilimia mia moja, lakini twende taratibu, kuagiza tu mamlaka zote zianze kuzuia mikaa kuingia mijini kwenda wapi, wakati mitandao ya gesi hatujaikamilisha, ni jambo ambalo hapana, hili jambo tutaonekana tunakurupuka na litaleta athari kubwa sana kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba sana kwa sababu hili jambo linagusa maisha ya wananchi wetu wengi wa vijijini na maisha ya wengi wa mijini, jambo hili lisitishwe mpaka pale ambapo tayari tutakuwa na nishati nyingine ambayo wananchi hawa wanaweza wakatumia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwa sina tabia ya kupenda kugongewa kengele, naamini haya ambayo nimeiambia Wizara, nimeiambia Serikali na hasa kwa wananchi wale ambao wanapoteza maisha, yatazamwe sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipindi hiki cha mvua huwa hakuna matukio makubwa ya mamba kuwavamia wananchi, kwa sababu maji yamejaa, wako katikati ya maji marefu, lakini kuanzia Julai hadi Desemba kila siku tunapokea taarifa ya vifo vya wananchi. Mheshimiwa Waziri wale ni Watanzania sasa nimwombe sana Mheshimiwa Waziri na Naibu wake kuwaambia Watendaji kwamba, wakiwa wanang’ang’ania taarifa zinazotolewa na jumuiya ya Kimataifa… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante.