Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii jioni ya leo na mimi nichangie Wizara hii ya Maji. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uhai na kuniwezesha jioni hii kusimama hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijielekeze moja kwa moja kwenye Mfuko wa Maji. Wachangiaji walio wengi hapa wameongelea kuhusu Mfuko wa Maji uongezewe fedha kutoka shilingi 50 kwenda shilingi 100 na mimi naunga mkono. Hata hivyo, naunga mkono lakini kwa upande mwingine nasikitika. Nasikitika kwa sababu nimeangalia kwenye hiki kitabu cha Mheshimiwa Waziri kwenye huu Mfuko wa Maji kwangu mimi sijatengewa pesa hata shilingi. Kwa hiyo, pamoja na kuomba kwamba uongezewe fedha lakini kwangu mimi ni majanga. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukifungua ukurasa wa 159 - 164 pale pameorodheshwa watu waliotengewa fedha zinazotokana na mradi wa maji katika Miji Midogo lakini Liwale haijatajwa. Kwa bahati mbaya zaidi ikaja ikatajwa ukurasa wa 164, namba 32 pale pametajwa Halmashauri 14 ambazo zimetengewa shilingi bilioni 3.5. Hivi mimi kama mwakilishi wa wananchi wa Liwale pesa hizi zisipofika nazifuatilia wapi? Huoni uwezekano nitakavyokwenda kufuatilia pesa hizi naweza nikaambiwa zimeenda Chato, Mkuranga ama sehemu fulani kwa sababu pale
zimerundikwa Halmashauri zaidi ya 14, nashindwa kuelewa.
(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile katika Halmashauri yangu ya Wilaya ya Liwale nimeshakwenda kwa Waziri mara kumi kidogo. Nimemwambia kuna mradi wa kutafuta chanzo cha maji mbadala kwa Mji wa Liwale, umeshakula shilingi milioni 200 lakini mpaka leo mradi ule umekufa na maji Liwale hatuna. Namwomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha hapa atuambie hatua gani imefikia mpaka mradi ule umekufa?(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwenye Mradi wa Maji Vijijini ambao unafadhiliwa na World Bank, awamu ya kwanza ilikuwa ni vijiji kumi lakini kwenye Halmashauri yangu nina vijiji saba tu lakini bado mpaka leo hii Vijiji vya Kipule, Mihumo na Ngongowele visima vile vimeachwa, vimeishia ardhini hakuna maji mpaka leo. Mheshimiwa Waziri atakaporudi hapa kuhitimisha hoja hii naomba atueleze ni nini hatima ya mradi ule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sio hivyo tu, nashukuru, Alhamdulilah, Kijiji cha Mpigamiti mpaka sasa hivi kimepata maji lakini kuna Vijiji vya Ngolongopa, Naujombo, Kitogolo, Mtawambo, Mkutano, Makata, Mikunya, Ngunja, Mkundi na Nandimba havina maji kabisa. Kwa hiyo, kwa heshima na taadhima namwomba Mheshimiwa Waziri awahurumie watu wa Liwale. Kama takwimu zinaonyesha kwamba Liwale tuko watu wachache kama ambavyo nimewahi kusema hatustahili kupata maji hayo niyasikie leo. Kama tuko wachache basi watuwekee koki moja moja kila kijiji kuliko kutunyima maji kabisa.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naingia kwenye skimu ya umwagiliaji.Nimeshaongea naMheshimiwa Waziri mara nyingi, kuna miradi mitatu ya skimu ya umwagiliaji Wilaya ya Liwale imegharimu nchi hii zaidi ya shilingi bilioni nne lakini mpaka leo hii ni mwaka wa saba hakuna senti hata moja iliyorudi kutoka kwenye miradi ile. Kwa maana kwamba hakuna mkulima aliyenufaika na miradi ile hasa hasa mradi wa Ngongowele. Niameangalia kwenye kitabu chake ametaja mradi mmoja tu wa Mtawango, mradi wa Ngongowele hautajwi kabisa na huu mradi wa Ngongowele ukienda pale ni ardhi tupu mpaka leo. Nafikiri nimeshakwenda kwake zaidi ya mara tatu. Kama Liwale hawaithamini basi hata hizi pesa za Serikali nazo hawazithamini, shilingi bilioni nne zimeteketea pale hakuna chochote kilichozalishwa nchi hii, tunafikiria kufanya kitu gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, usimamizi wa miradi hasa ya umwagiliaji, nashindwa kuelewa, tukienda kwenye Halmashauri tunaambiwa miradi hii inasimamiwa na Kanda kwamba sisi watu wa Halmashauri hatutakiwi kuhoji chochote. Sasa inapofikia miradi ile haikamiliki nani wa kumfuata? Mheshimiwa Waziri nimeshakwenda kwake zaidi ya mara tatu naulizia, atupe ufafanuzi hii miradi nani afuatwe, watu wa Kanda au watu wa Halmashauri lakini hakuna majibu yoyote ambayo ameweza kunipatia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo basi, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa kuhitimisha anieleze tatizo la maji linatokana na nini hasa Mkoa wa Lindi. Hata kwenye bajeti mkoa ambao umepata bajeti ndogo zaidi ni Mkoa wa Lindi, tatizo liko wapi? Au ile dhana ya Kusini bado mnaiendeleza?Mnataka ile hadithi niliyowapa hapa iwe ya kweli?Jamani naomba tuiangalie Kusini, tuiangalie Lindi. Lindi tunahitaji maji hata kama tuko wachache hao wachache wanahitaji maji, maji hayana wingi wala uchache wa mtu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maana kama upande wa hospitali unaweza kusema kwa sababu tunahudumia watu wachache Madaktari wawili wanatosha, lakini maji nayo je? Tunaomba Mheshimiwa Waziri pamoja na kwamba Wabunge wengi wamesema kwamba Wizara hii ya Maji iongezewe bajeti, naomba atakapoongezewa bajeti kama hili litakubalika basi autazame Mkoa wa Lindi maana bajeti yetu ni ndogo sana. Tena hizo fedha kidogo tulizotengewa ni za wafadhili na siyo za ndani. Kama fedha za ndani hatuna tunategemea fedha za wafadhili itakuwa shida wasipoleta. Mkoa wa Lindi bajeti yetu asilimia kubwa ni ya wafadhili maana yake wafadhili wasipotoa pesa Mkoa wa Lindi tumeambulia patupu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijagongewa kengele ya pili, nilikuwa na hayo machache ya kumweleza Mheshimiwa Waziri. Tena kwa bahati mbaya zaidi kwa sababu ya matatizo ya usafiri nimekosa Mawaziri watatu mwezi wa Kwanza na wa Pili kuja Liwale kutembelea ile Wilaya, Naibu Waziri na Waziri wa Miundombinu ni wamojawapo, walipanga kuja Liwale lakini wameshindwa kuja kwa sababu ya usafiri, barabara chafu na mbaya. Nataka niseme kama Mawaziri hawatakuja nitaendelea kupiga kelele hapa na Mungu anawaona.