Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Felister Aloyce Bura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji

MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia, lakini pia namshukuru Mungu wangu kwa uzima na afya njema aliyonijalia.

Mheshimiwa Naibu Spika, naungana na Waheshimiwa Wabunge wote wanaosema kwamba bajeti ya Wizara ya Maji iongezwe, kwa sababu maji ni uhai. Nami kama mwanamke ambaye wenzangu wanahangaika usiku na mchana kutafuta maji, napata shida sana ninapowaona wenzangu hasa wa maeneo ya vijijini ninapofanya ziara; siku moja nililetewa maji ambayo sikujua kama ni majivu au ni maji, lakini yalikuwa maji ambayo wananchi wangu walikuwa wanayatumia.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali kwamba katika Mikoa ya Kanda ya Kati, Mikoa ya Singida na Dodoma Serikali itutazame kwa jicho la huruma sana kwa sababu hatuna mvua. Nimemsikia Mbunge wa Mkinga akisema kwamba kwake mvua inanyesha na imepitiliza, lakini hata kwa Mkoa wa Dar es Salaam mvua zinanyesha sana, Mikoa ya Kanda ya Kusini mvua zinanyesha, lakini sisi tulishasahau mvua; na mvua zinazonyesha sasa hivi haziwezi hata kujaza dimbwi. Kwa hiyo, wanawake wa Mkoa wa Dodoma wanateseka mno kwa kutafuta maji.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nami nahisi maeneo ya vijijini watu wameacha mambo ya dini wakaoa wanawake wengi hasa Wakristo, kwa sababu ukioa wanawake wengi mmoja akiwahi kwenda kisimani mwingine atabaki kulinda mji. Kwa hiyo, wanapata shida. Asubuhi saa kumi ndiyo wanatoka kwenda kutafuta maji na wanarudi saa tano mwanamke akiwa na ndoo moja na asubuhi wanaondoka na majembe na ndoo kichwani na jioni anarudi na ndoo na jembe begani. Naomba ufike wakati sasa Serikali ione namna ya kuisaidia hasa Mikoa hii ya Kanda ya Kati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mji wa Dodoma na viunga vyake, unakua kwa kasi kubwa sana, lakini miundombinu ya maji ni ile ile. DUWASA bajeti yake ni ile ile, vijiji vinavyozunguka Mji wa Dodoma wanategemea DUWASA kupata maji, DUWASA haina uwezo wa kusambaza maji kwa vijiji ambavyo viko eneo la mji huu. Mji huu wameshakuja wafanyakazi 2,800 kwa taarifa nilizopata hivi karibuni, lakini miundombinu ya maji iko pale pale. Maji yanatoka Mzakwe Kijiji cha Veyula hakina maji; UDOM hapa Ng’ong’ona hawana maji, Mkonze karibu tu na Kilimani hapa, hawana maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa Serikali iangalie kwa jicho la huruma Mji wa Dodoma kwa sababu unakua kwa kasi kubwa sana na miundombinu ya maji taka ndio hatuwezi kusema kwa sababu miundombinu ya majitaka DUWASA hawawezi peke yao bila mkono wa Serikali. Serikali iwasaidie DUWASA kuweka miundombinu ya maji taka lakini na maji ya kunywa kwa wananchi wa Dodoma Mjini pamoja na viunga vyake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali sasa, tumesema kuna maji, kuna mvua katika maeneo mengi, lakini shule zetu za sekondari na shule zetu za msingi hawana maji. Kwa nini Serikali isitafute namna ya kuvuna maji kwa shule zetu, Vituo vya Afya na Zahanati ili suala la maji katika Vituo vya Afya, Hospitali, Shule za Sekondari na Shule za Msingi sasa iwe ni hadithi?

Mheshimiwa Naibu Spika, ukizingatia kwamba sasa hivi wazazi hawatakiwi kuchangia; hawachangii ada, lakini ukiwaambia wachangie kulipa bili ya maji hawakubali, lakini tukivuna maji hatutahangaika kuwaambia kwamba wachangie bili ya maji. Kwa hiyo, Serikali ione namna sasa ya Vituo vyetu vya Afya na Shule za Sekondari na ikiwezekana Shule za Msingi pia wapate maji kwa kuvuna maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa vijiji kumi haujafanikiwa katika Mkoa wetu, maeneo mengi mradi wa vijiji kumi kupata maji haujafanikiwa sana na haujafanikiwa sana kwa sababu waliokuwa wana-monitor ni Wizara. Kwa hiyo, Halmashauri zetu hazikuwa na nafasi ya kusimamia ipasavyo. Wakandarasi ambao wamefanya kazi zao vizuri, walipwe ili wakamilishe kazi zao.

Pia tuna suala la Tanzania kuwa nchi ya viwanda, lakini viwanda, malighafi watapata wapi? Kwa sababu malighafi kwa sehemu kubwa ni mazao na mazao tunategemea mvua. Suala la umwagiliaji litiliwe mkazo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna bwawa la Kongogo lina miaka minane halijakamilika. Miaka minane hata skimu yenyewe haijaandaliwa. Wananchi wameshasubiri mpaka wamechoka, ile skimu ya Kongogo haijafanya kazi. Contractor aliyekuwepo, mpaka ameondoka skimu haijafanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Maji ya Maporomoko ya Ntomoko, tuliwahi kumpeleka Mheshimiwa Waziri Mkuu Mstaafu aliyepita, Mheshimiwa Pinda mwaka 2013/2014 na akatuahidi fedha na akapeleka, lakini hazikutosheleza na mradi ule una uwezo wa kusambaza maji vijiji kumi na nane. Sasa hivi nimeona vijiji vinane tu ambavyo vimewekwa kwenye bajeti.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana na suala la Farkwa. Farkwa litasaidia sana maji ya Mzakwe, Bahi, Chemba na Chamwino, lakini mradi ule tume….

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, lakini suala la Farkwa Ntomoko na Dodoma Mjini…