Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii ya kuweza kuhitimisha hoja baada ya kuwa tumepata michango toka kwa Kamati, kutoka Kambi Rasmi ya Upinzani na kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote niwashukuru wote waliochangia, tukianza na maoni ya Kamati, maoni ya Kambi Rasmi ya Upinzani pamoja na Waheshimiwa Wabunge ambao ndiyo mmetoka kuchangia hivi punde. Wizara tumeyapokea maoni yenu, tutayafanyia kazi na tutayachambua yale ambayo yanahitaji ufafanuzi wa kina zaidi, tuweze kuyajibu kwa maandishi. Kwa yale ambayo mmetupa ushauri ambayo yanahitaji kufanyiwa kazi kwa ujumla wake kwa sababu hoja ni nyingi, niwaambie tu kwamba tumeyapokea na tutayafanyia kazi, kama ambavyo tumekuwa tukipokea ushauri kutoka kwenu mnapokuwa mmetimiza wajibu wenu wa kikanuni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza na hoja za jumla kabla sijaenda kwenye hoja mojamoja kati ya hoja ambazo zilijitokeza. Hoja ya kwanza ambayo imeongelewa kwa upana ni hii ambayo ilikuwa inahusisha mambo ya Vyama vya Siasa pamoja na Wabunge na ndugu yangu Mheshimiwa Lijualikali akasemea kwamba labda haya yanafanyika kwa Wabunge wa Upinzani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niweke kumbukumbu sawa; moja, vyama vingi vya siasa kwenye nchi yetu viko kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kwa sababu viko kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kila Mtanzania kuwa kwenye chama anachokitaka si kosa. Mtu anapokuwa kwenye Chama chake siyo kosa. Ikumbukwe tu kwamba wakati vyama vingi vya siasa vinaanzishwa kilikuwepo chama kimoja tu, Chama cha Mapinduzi na kwa aina ya watu waliokuwepo na maoni yaliyotolewa kulikuwepo na fursa pana zaidi ya kuwa na chama kimoja kuliko kuwa na vyama vingi, kwa maana hiyo Chama cha Mapinduzi kwa ridhaa yake ndiyo kilianzisha vyama vingi na kama Chama cha Mapinduzi kilianzisha vyama vingi na tangu vyama vingi vianzishwe Chama cha Mapinduzi hakijawahi kuyumba kuhusu ushindi wake, kuanzia ngazi ya vijiji mpaka ngazi ya Urais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo, niwaambie Waheshimiwa Wabunge, panatokea kamsukosuko kadogo mnaanza kutafuta mchawi, mara wanasema wanatumiwa mara wanasema wanatumwa na juzi nilimsikiliza Kiongozi wenu Mkuu akisema hao wanatumwa. Niwatoe hofu, Serikali pamoja na Chama haiwezi ikaanzisha yenyewe vyama vingi na yenyewe ikaanza kushiriki kuviondoa vyama hivyo, kwa sababu hata hivyo haijawahi kupata tishio lolote na uwepo wa vyama vingi bali imepata faida na uwepo wa vyama vingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, katika mazingira haya, niwashauri kitu kimoja, ndugu yangu Mheshimiwa Khatib Said Haji, ndugu yangu Mheshimiwa Katani walioongea, panapokuwepo na misukosuko ni wakati wa kutulia, huu nimewapa tu ushauri kwa kifupi ni wakati wa kutulia. Pia panapokuwepo na mizozo inayotishia usalama wa raia litakuwa jambo la kushangaza kama watu ambao wana jukumu la kusimamia usalama wa raia wasipoingilia kati, wakiingilia kati hilo ndilo jukumu lao, kwa sababu leo hii kukitokea jambo ambalo linatishia watu kupigana halafu Polisi kwa maana ya Wizara ya Mambo ya Ndani wakawa wameshapewa taarifa wasiende watakuwa hawajatimiza wajibu wa kulinda usalama wa raia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pande zozote zile, hata mechi tu za mchezo wa ndondo, wakiona pana tishio la usalama wanaita Polisi wanaenda kuwasaidia. Kwa hiyo, ndugu zangu pande zote zinazoona mnatofautiana mkiona mna shida toeni taarifa ili polisi iweze kuingilia kati. Sisi tusipoingilia kati tutakuwa hatujatenda haki ya kuwahakikishia raia wa Tanzania usalama wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mazingira kama hayo, mambo ya aina hii, niwaombe msitafute mchawi nje yenu, tumieni Katiba yenu, tumieni taratibu zenu ili muweze kulimaliza jambo hilo na nchi yetu inufaike na malengo yaliyokusudiwa kwa ajili ya uwepo wa vyama vingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu yangu, Mheshimiwa Katani ndiyo amenichekesha zaidi, anasema kulikuwepo na mkutano wa ndani kule kwao, mkutano wa ndani tu, halafu ndiyo anatolea mfano kwamba Waziri ulitamani mpaka Urais halafu hukuingilia kati ume-prove failure. Unajua kwa mtu anayetamani mpaka Urais kuingilia kitu ambacho OCD tu kinamtosha na yenyewe haijakaa sawa. Jambo ambalo lilikuwa la mkutano wa ndani la kibali cha mkutano wa ndani, hilo ni jambo ambalo Mkuu wa Polisi wa ngazi ya Kata ile anaweza kulimaliza na inapotokea limeshapita ngazi zote zile, basi utaratibu unaelekeza kukata rufaa kwa maandishi kwenda kwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sijawahi kupata rufaa hiyo ambayo inaelezea kwamba kuna jambo mahali fulani limeshindikana, mara zote inapotokea jambo limetokea la aina hiyo niwashauri kwamba tumieni taratibu, tumieni ofisi. Mara zote Polisi hawatungi sheria, Polisi wanasimamia sheria na pale ambapo sheria sisi wenyewe ndiyo tumepitisha, niwaombe Waheshimiwa Wabunge wala tusiwalaumu Polisi na kama tunaona zina kasoro basi tuzirekebishe ili wao wasimamie kwa urahisi bila kupata shaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi niwaambie tu Waheshimiwa Wabunge, baada ya kukaa kwenye Wizara hii nimekuja kuona kwamba lawama nyingi sana wanazopelekewa polisi hazitokani na polisi wenyewe. Kwa mfano, hata mambo haya yanayoongelewa sana ya kubambika kesi, mimi naweza nikawambia kwa kiwango kikubwa kesi za kubambikwa hazibambikwi na polisi ila wananchi wenyewe kwa kuhasimiana ndiyo wanaobambikiana kesi hizo. (Makofi)

Kuna Wilaya nilienda, tulijaribisha hata kufanya kura ya maoni, tulifanya kura ya maoni ya wazi ya kutafuta wahalifu; ili muweze kuona makundi yanayohasimiana yanavyoweza kubambikiana kesi. Baada ya kura ya maoni ile kupigwa kutafuta wahalifu wa CCM wote waliandika wahalifu ni wale wa CHADEMA, halafu wale wa CHADEMA waliandika wahalifu wote ni wale wa CCM. Leo hii ukienda Pemba ukiitisha kura ya maoni kutafuta wahalifu itakuja kwa muundo huo huo; na hata ukienda kwenye kesi nyingine kubwa, ndiyo maana wakati mwingine uchunguzi unachukua muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda ukakuta msikiti ambao hauna ugomvi, umetulia kabisa ibada zinaenda vizuri hamna kesi ya ugaidi, ukienda kwa wale waliogombana zinatokea kesi za ugaidi. Sasa polisi ambaye hasali pale amejuaje huyu ana kasoro hii na hii? Wengine ni wacha Mungu tu wanatumia muda mwingi sana kutimiza ibada zile lakini ndiyo hivyo kwa sababu ya maslahi mengine ya kiuongozi wala siyo ya kiibada yanatokea hivyo.

Kwa hiyo, ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge tunapokuwa tunaongelea mambo ya polisi tuweke akiba tukizingatia kwamba wao wanatimiza sheria, lakini pia taarifa nyingi wanazozitumia kuchukua hatua zinatoka kwa wananchi na tukishalijua hilo tutawasaidia waweze kutimiza wajibu vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipokutana na ma-RPC niliwaambia wasitumie taarifa za mahasimu wanaohasimiana kuwa ndiyo taarifa pekee za kujenga hoja katika kuandaa mashitaka hayo. (Makofi)

Tutaendelea kulifanyia kazi, lakini makundi yanayohasimiana hayajengi hoja ya kuweza kujitosheleza. Hatutapuuza kitu lakini ile siyo njia pekee ya kuweza kujengea hoja na kumtia mtu hatiani. Hata tu ukimuuliza Ndassa kwenye michezo ni nani wanaocheza rafu yeye atakutajia wale tu anaohasimiana nao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye hoja moja moja, nikianza na zile zilizotolewa kwenye Kamati. Serikali imepokea ushauri wa Kamati na utazingatiwa; na kama ambavyo tumekuwa tukifanyia kazi na tutaendelea kushauriana nanyi kuweza kuhakikisha kwamba yale yaliyotolewa na Kamati tunayafanyia kazi na majawabu yake mnayaona.

Kwa upande wa Zimamoto, hoja iliyotolea na Mheshimiwa Mkuchika tumeipokea, lakini si kwamba hatukuweka uzito, tuna mipango ambayo inaenda sambamba na hii ambayo imeonekena kwenye bajeti. Bajeti kubwa ya Serikali kuu itakapokuja itakuwa na dirisha ambalo Serikali inategemea kukopa fedha; na sisi tumeshafanya mazungumzo kama nilivyosema na wenzetu wa Ubelgiji pamoja na Australia ambapo tunategemea kupata zaidi ya Euro 22,000 kwa ajili ya manunuzi ya magari ya zimamoto na uokoaji. Kwa hiyo, pamoja na bajeti iliyotengwa, kuna njia zingine ambazo zinaenda sambamba ambazo ndizo tunategemea zituongezee nguvu za kupata magari hayo ambayo tunayahitaji.

Waheshimiwa Wabunge wengine waliochangia kwenye upande wa zimamoto, Mheshimiwa Juliana Shonza, Mheshimiwa Shabani Shekilindi, Mheshimiwa Sophia Mwakagenda pamoja na Mheshimiwa Japhet Hasunga tumepokea hoja zenu, hoja zenu ni za msingi na niwahakikishie kwamba Serikali inazifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa hoja zingine za mtu mmoja mmoja zilizotolewa, zimetoka hoja za masuala ya umeme aliyotoa Mheshimiwa Lucy, kuna hoja ilitolewa na Mheshimiwa Mtumwa kwa ajili ya kituo cha polisi, Mheshimiwa Raza na ndugu yangu Kangi Lugola; tumeyapokea na katika bajeti hii ni moja ya mambo ambayo tumeyazingatia sana haya yanayohusu maslahi ya askari wetu pamoja na haya ya vituo vya polisi na masuala ya umeme kama ambavyo Mheshimiwa Kiwelu aliulizia pamoja na Mheshimiwa Kangi Lugola.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumetolea ufafanuzi zaidi na tutawapa kwa maandishi kwa namba na kwa maelezo jinsi mafunzo ambavyo yameweza kufanyika kwa vikosi vyetu vyote ambavyo viko ndani ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

Jambo lingine ambalo liliongelewa ni lile linalohusu package kwa vikosi vingine vilivyosalia. Ameisema kwa kirefu Mheshimiwa Gekul na mara kwa mara amekuwa akiisemea Mheshimiwa Esther Matiko pamoja na ndugu yangu Mheshimiwa Mchengerwa.

Niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba ilikuwa ni utaratibu wa utoaji wa fedha kwa vipaumbele, haikuwa kuweka madaraja, ilikuwa ni utaratibu wa utoaji wa fedha kufuatana na upatikanaji wa fedha na mahitaji kwa sekta nzima kwa maeneo yote katika nchi yetu. Kwa mfano, fedha zinapopatikana kipaumbele cha kwanza kinakuwa ni mishahara ya watumishi wote kwa ujumla wao, ukishatoka hapo kunakuwepo na suala la Deni la Taifa na ukishatoka hapo kunakuwepo na mafungu madogo madogo kulingana na bakaa inayosalia.

Kwa hiyo, kwa utaratibu ule, ili na shughuli zingine ziweze kuendelea ilionekana ni vyema tuanze na kikosi kimoja kimoja kwa maana ya taasisi moja moja zilizoko kwenye vikosi, hivyo ndivyo ilivyotokea wakapata wa kwanza wakaja wakapata Polisi na kwa sasa tunavyoongea mwezi huu watapata Magereza na baada ya hapo watapata na wengine. Niwatoe hofu jambo hili kila askari ana fedha yake; kwa hiyo hakuna wa kusema huyu aliyechelewa labda atakuwa amekosa, watapata kama wenzao waliokuwa wamepata na watapata arrears zao kama ambavyo ilitakiwa waweze kupata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hili la Magereza alilisemea nadhani na mmoja wa wachangiaji kwamba nitembelee Magereza. Mimi nimeshatembelea Magereza mengi sana, yamebaki machache sana ambako sijaenda, na kote nilikopita nimeziona hizo hali zote. Ndiyo maana tunapotengeneza utaratibu wa utekelezaji wa mpango wetu tunazingatia yale ambayo tumeyakuta katika hali halisi za Magereza yale. Hata lile la Hanang nilifika na nimeona ujenzi ambao ulishaendelea lakini halijaanza kutumika kwa sababu sehemu ya jengo la utawala lilikuwa bado halijakamilika, na hicho ndicho ambacho tunaweka uzito.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunaitambua hiyo hoja ya kwamba mahabusu wanakuwa hawaendi kusikiliza kesi zao kwa sababu kwanza, panakosekana magari, lakini pili wakati mwingine mafuta yanakosekana; pia na ule umbali unasababisha hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mary Nagu amelisema sana na amelililia sana na hata alishachangia sehemu ya ukamilishaji wa jengo hilo na mimi niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge tunatoa vipaumbele kwenye maeneo hayo. Hoja yako tumeipokea, kwamba watu hawa wanakosa haki zao, lakini niseme kwamba ni jambo ambalo tulishalipokea na mimi nilishafika katika ene hilo, na hiyo hoja ya kutokutumia angalau yale majengo ambayo yalishajengwa nilishaiona na niwahakikishie kwamba tutalipa uzito unaostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye maoni ya Taarifa ya Kambi Rasmi ya Upinzani; Mheshimiwa Lema ameulizia kwa nini Jeshi la Polisi linazuia mikusanyiko ya kisiasa kwa sababu za kiintelijensia. Jeshi la Polisi halizuii mikutano ya kisiasa iwapo muhusika atafuata taratibu na kwa upande wa Waheshimiwa Wabunge nilishalielezea kwenye briefing na nilishaelezea siku nilipokuwa najibu maswali hapa.

Waheshimiwa Wabunge, baadhi yenu mmoja mmoja tulishaongea, kwenye hili la mikutano ya hadhara hatujataka utaratibu ambao uko duniani kote ila tumetaka utaratibu wa kimazoea na kwa sababu tunabeba utaratibu wa kimazoea tunasababisha jambo zima lionekane liko tofauti. Utaratibu uliopo kama taasisi zile za vyama vya siasa zingekuwa zinaangalia hata mataifa mengine yanafanyaje kile ambacho kingekuwa kinadaiwa hakikupaswa kiwe hiki ambacho kinadaiwa kwa sasa hivi. Kwa sababu hiki ambacho kinatokea ndiyo common practice katika mataifa yote ambako tunajifunza demokrasia ya vyama vingi. Naiunga mkono hiyo kwa sehemu hiyo ya kuhakikisha kwamba kila mtu kwenye anuani yake aende akafanye shughuli zake za kazi za watu wake ambako wanaweza wakamhoji na akafanya kazi za kwake za kisiasa.

Kwa maana hiyo kama jambo hili lingekuwa linajadiliwa kwa sehemu ya wale ambao jukumu lake si sehemu ile aliyochaguliwa ile ingekuwa ni mada nyingine, lakini ule utaratibu uliokuwa unatumika wa kiholela hata Watanzania wenyewe walikuwa hawaridhiki nao na ni utaratibu ambao umewagharimu sana Watanzania katika baadhi ya maeneo na ninyi ni mashahidi. Hata hivyo utaratibu huu ambao umekuwa ukitumika katika maeneo mengine umesababisha mpaka vifo. Kwa maana hiyo hili ni jambo ambalo Mheshimiwa Rais alilitolea dira, ndio utaratibu ambao na maeneo mengine unatumika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, Mheshimiwa Lema alisema kwa nini Jeshi la Polisi linafanya kazi ya kukusanya mapato na tozo wakati hiyo ni kazi ya TRA. Tuna mapato ambayo yanakusanywa na TRA, lakini vile vile kuna sehemu ya mapato ya Serikali yanayojulikana kama maduhuli yanakusanywa na taasisi mbalimbali za Kiserikali kufuatana na convenience ya kuweza kukusanya mapato hayo. kwa

mfano mapato kidogo yanayoweza kukusanywa na Jeshi la Polisi ni convenience kwamba hawa watu wametapakaa maeneo mengi wanaweza wakaifanya kazi hiyo kwa ufanisi kuliko kutumia TRA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ameelezea suala la Wakili Mwale ambalo amesema kwamba kesi yake imechukua muda mrefu. Niseme tu kwamba nimelipokea na kwa sababu ni eneo ambalo na mimi napanga kuzungukia, ni maeneo ambayo tumekuwa tukizungukia kwa kushirikiana na wenzetu wa Wizara ya Katiba na Sheria, ni jambo ambalo tunalipokea, tutafuatilia undani wake tujue imefika wapi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka hata DPP amezunguka maeneo tofauti tofauti akiwa na Dkt. Mwakyembe, na wakati mwingine tumezunguka tukiwa wote watatu kama Wizara, kuna baadhi ya maeneo ambayo tuliyatolea ufafanuzi na kuna baadhi ya maeneo ambayo tulichukua hatua kwa watu ambao walikuwa na matatizo ya aina hiyo..

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni hoja ambayo tumeipokea, tutakaa na kaka yangu tulione na tufuatilie, tujue undani wake umefikia wapi; lakini na kile ulichosema kwa huyu tuweze kuangalia na wengine ambao wanaangukia kwenye mkumbo huo ili waweze kupata haki zao na waweze kuendelea na maisha yao, tumeipokea na tutaifanyia kazi. Kwa Wabunge wengine ambao mmepokea hoja za aina hiyo, tunaweza tukapenyezeana lakini na sisi tutazungukia katika maeneo tofauti tofauti ili tuweze kuchukua hatua na watu hawa waweze kupata haki zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili la askari wa usalama barabarani (traffic) kupata mafunzo na wengine elimu ya usalama barabarani tumeshalisema na kuna hatua ambazo tumesema tutazichukua ili kuweza kuhakikisha kwamba watu wetu wanaendelea kuwa na mafunzo na wanafanya kazi kwa weledi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine lilisemwa na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kwamba Jeshi la Polisi nchini litahakikisha kwamba amani na utulivu vinakuwepo. Hili ni jambo la kipaumbele kwa Wizara yetu na tumesema hata katika haya maeneo ambayo katika siku za hivi karibuni kumetokea na rabsha za hapa na pale, niwahakikishie kwamba kazi inaendelea kwa ufanisi mkubwa sana, kazi inayoendelea ni kubwa sana na kwa sababu ya mazingira ya kiusalama hatusemi mipango tunayoifanya na hatusemi hatua tunazochukua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo miwahakikishie Waheshimiwa Wabunge mnaotokea katika maeneo hayo na maeneo mengine kuweni na uhakika kwamba Serikali iko kazini, Wizara ya Mambo ya Ndani iko kazini, Jeshi la Polisi liko kazini na niwahakikishie kwamba ni suala la muda tu. Wale ambao wameamua kujipima kwenye hilo, mimi niwatangazie kwamba wameshindwa kabla hata hawajaanza na tutashughulika na mmoja mmoja mpaka tutampata wa mwisho anayeshughulika na mambo hayo. Mpaka sasa zoezi hilo linaendelea vizuri na watakuwa wanajihesabu na wengine wanawaona wakiwa huko magerezani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatutamvumilia hata mmoja asababishe maisha ya wananchi wetu yawe ya hekaheka. Kwa hiyo, tutashughulika na mmoja mmoja lakini na yoyote yule ambaye atashirikiana na wahalifu na yeye tutamuunganisha na wahalifu. Hatutaruhusu watu wetu washindwe kufanya shughuli za uzalishaji kwa sababu ya watu ambao hawataki amani katika suala la aina hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa hoja za maandishi, Mheshimiwa Mwikabe alisema askari wana madai mengi ya likizo, safari na kuistaafu. Nilielezea kwenye hotuba, kazi kubwa sana imefanyika ya malipo, na ukiangalia malipo ya madai ndiyo utaona kwamba Magereza hatuwabagui, kwenye madai yale tuliyolipa, Magereza tumewalipa fedha nyingi kulikoa hizi taasisi nyingine ambazo ziko Wizara ya Mambo ya Ndani. Kwa hiyo, tunatoa tu vipaumbele vinavyolingana lakini panapotokea pana mtiririko wa fedha ambao hautoshi kuwalipa wote kwa pamoja tunafanya kwa namna hiyo.

Ndugu yangu Mheshimiwa Njalu alisemea kuhusu malalamikoa ya askari kuhusu nyongeza ya mishahara na posho; tumeweka yale mapendekezo niliyoyasoma wakati nawasilisha bajeti leo hii mapema.

Waheshimiwa Wabunge wengine wameelezea kwa kirefu, Mheshimiwa Mponda, Mheshimiwa Mtulia, mama yangu wa Iringa, ndugu yangu Mheshimiwa Kakoso wa Mpanda na ndugu yangu Mheshimiwa Shangazi tumepokea hoja zenu. Hii aliyoisemea Mheshimiwa Kakoso aliisema pia Mheshimiwa Kadutu, ameisema pia ndugu yangu Mheshimiwa Mbogo wa Nsimbo, jambo hilo kwa ngazi ya Serikali tumelipokea kuhusu uamuzi uliofanyika siku zilizopita wa kuwapa uraia ndugu zetu wapendwa wa kutoka Burundi na nchi nyingine, lakini baada ya kuwapa wakaendelea kukaa wamoja katika eneo lao moja ambalo baadhi yao wasiojua vizuri misingi ya nchi yetu, wanatengeneza kanchi ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumelipokea, tunaendelea kujadili kwa ngazi ya Serikali kuangalia utaratibu ni upi mzuri ambao utawafanya baada ya kuwa wameshakuwa Watanzania wasichukue hata kimoja kilicho kibaya kutoka katika Mataifa yao yaliyosababisha hata wakatoka kule walikokuwa.

Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge tumelipokea na baada ya kuwa tumeshamaliza bajeti kwa ngazi ya Serikali tutajadiliana na ninyi tutawahusisha na Kamati tutaihusisha kwa sababu ilishatembelea hata hayo maeneo ili tuweze kuona njia muafaka na ya kudumu ya watu hawa ambao walipata uraia. Kwa sababu hawatakuwa watu wa makazi yenye taswira ya kiukimbizi lakini wakiwa ndani ya nchi. Hivi ilivyo sasa, sheria wanazozitumia wanazitumia ambazo ni za makazi ilhali walishakuwa raia kwa kupewa uraia. Kwa hiyo, hilo tumelipokea na niwahakikishie kwamba tutalifanyia kazi. (Makofi)

Ndugu yangu Mnyika ameongelea kuhusu vituo vya polisi katika Wilaya yake; nilisemee tu kwamba tayari tuna hatua ambazo tunazichukua. Maeneo yale ya mji ni moja ya maeneo ambayo tunaweka vipaumbele kwa sababu uhalifu unapotokea katikati ya Jiji unahamia pembeni. Kwa hiyo, hivi tunavyoongea pale Madale kuna kituo kimekamilishwa cha Daraja B, Kiluvya pana kituo kimekamilishwa na Mburahati ambacho ni cha Class A.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya aina hiyo pia ameisemea Mheshimiwa Bonnah kwa upande wa Segerea; tumeipokea na yenyewe tutaipa uzito unaostahili na baada ya Bunge kuwa limeisha tunategemea kufanya tathmini kujua hayo maeneo ambayo yameshauwa na watu wengi yanastahili kuwa na vituo lakini kwa mazingira yalivyo yanaendelea kutokuwa na vituo na hivyo kusababisha matatizo.

Ndugu yangu Mheshimiwa Dau ametoa hoja yake na ndugu yetu Mheshimiwa Mwenyekiti wa Kamati ametoa na yeye maoni yake kwa maandishi. Mheshimiwa Adadi nikuhakikishie tu kwa kuwa wewe ni dictionary inayotusaidia kwenye taasisi hii na kumbukumbu nzuri kwenye taasisi hii, hoja yako ambayo umeitoa tumeipokea. Tunawapongeza sana wananchi wa Muheza kwa kukuchangua kwa kweli umekuwa dictionary inayotusaidia katika Wizara yetu, tutaifanyia kazi hoja yako kwa uzito unaostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Faida Bakar ulipewa dakika chache sana lakini mambo uliyoyaongea yamekuwa na msingi sana na yatatusaidia sana, tumeyapokea. Ni kweli Jeshi la Polisi katika maeneo ya Pemba wanafanya kazi kwa mazingira magumu sana na mimi nilishafika huko, tumeyazingatia yote uliyasema, tunayapa uzito. Juu ya hoja yako uliyotoa katika eneo lake itatupa fursa ya kuifanyia kazi na kuwapa faida na maeneo mengine. Kwa sababu kuna maeneo mengine yanayofanana na huko ulikotolea mfano na mimi nilijionea nilipofika katika eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa uhamiaji hoja zilizotolewa zilikuwa ni Serikali iendelee kutekeleza mpango wa kuwarudisha makwao wahamiaji haramu walioko magerezani ili kupunguza gharama za kuwahudumia na kupunguza msongamano. Jambo hili lina matatizo lakini tumeendelea kulijadili. Waheshimiwa Wabunge hata ninyi mtakubaliana nami kwamba lina matatizo. Moja wengi wa wahamiaji haramu tulionao kwenye magereza yetu kimsingi ni wapitaji haramu, kwa sababu wengi wao nia yao huwa si kukaa Tanzania; ndiyo maana unakuta wengine walishapita, wanakaribia kupita wanakamatwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo tatizo lake ni kwamba tumeingia kwenye mikataba ya kimataifa ya kutokufanya biashara ya usafirishaji wa binadamu. Kwa hiyo, hilo ambalo linatokea, linatupa shida ya namna ya ku- facilitate upitaji wao kwa sababu ya mikataba hiyo kwamba tupo kwenye mstari mwembamba sana wa kuonekana tumewasaidia wapite kwa sababu hawakai kwetu, lakini vilevile kwa wakati ule ule iwe hatujavunja hilo sharti la kuwa tumeshiriki kurahisisha usafirishaji wa binadamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kwa mazingira kama hayo tunajadiliana tuone ipi ni njia muafaka na hili litajadiliwa kwa ngazi ya nchi wanakotoka hawa watu ili kuweze kuonekana ni namna gani ambavyo tunaweza tukalifanya. Lakini sasa hivi Serikali inaendelea na juhudi za kuwaondosha nchini kwa taratibu zilizopo. Zoezi hili limekuwa likitekelezwa punde fedha zinapopatikana kwa sababu linahitaji fedha kuweza kuwasafirisha watu hawa. Kwa hiyo, juhudi hizo za kuwaondoa kwa utaratibu huu ambao hautatufanya tuonekane tumevunja mikataba hiyo na tuonekane ni sehemu ya nchi inayofanya biashara za kusafirisha wanadamu tuwe tumelikwepa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ilikuwa kwamba Serikali iwezeshe bajeti ya Fungu 93 kwa kufanya makisio ya doria ili kubaini na kuwaondosha wahamiaji haramu, jambo hilo limezingatiwa na bajeti imeongezewa. Lingine ilikuwa kuhusu hati za kusafiria; Serikali ipo katika mpango wa kutoa passport mpya za kielektroniki ambapo kwa mujibu wa makubaliano ya Wakuu wa Nchi wa Jumuiya za Afrika Mashariki, passport za ki-diplomasia zitakuwa na rangi nyekundu kwa nchi zote za Afrika ya Mashariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ndugu yangu Mheshimiwa Hamidu na ndugu yangu Mheshimiwa Zainab waliongelea kuhusu masuala ya Msumbiji na Mtwara. Raia wa Msumbiji wanaoishi katika Mkoa wa Lindi na Mtwara ni wahamiaji walowezi na hivyo kisheria hawana haki ya kupiga kura. Aidha, katika Katiba yetu pamoja na sheria haviruhusu uraia wa nchi mbili, kwa maana hiyo ili kuondoa utata walowezi wote hao wanaoishi bila vibali hawatambuliki. Hata hivyo Serikali inaendelea na zoezi la kuwatambua ili kuweza kuwapatia kibali kinachoitwa Settled Migrants Spars ambapo kitawawezesha kisheria kwa mujibu wa marekebisho ya Kanuni za Sheria ya Uhamiaji ya mwaka 2015.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukirudi kwa upande wa NIDA, alisema kwa kuandika Mheshimiwa Upendo Peneza pamoja na ndugu yangu Mheshimiwa Pondeza. NIDA anasema iliandaliwa shilingi bilioni 172 kwa upande wa JKU Zanzibar na Serikali ielezee hili deni litalipwa lini, nimelipokea.

Mheshimwia Mwenyekiti, jambo lingine alilolisema ndugu yangu Jaku, nimuombe wala asishike shilingi, jambo lake tulishalipokea, tumelifanyia kazi kwa kiwango kikubwa. Isipokuwa ni kwamba kiserikali kuna procedure ambazo ni lazima zifuatwe hasa mambo yanapokuwa ya kimalipo. Lazima uhakiki ufanyike na uhakiki ukishafanyika kuna taratibu za kuweza kuanza kulipa. Kwa maana hiyo taratibu ambazo zinahusisha fedha pamoja na kuielewa vizuri hoja yake, lakini lazima taratibu zingine za uhakiki ilikuwa ni lazima zifanyike ndipo taratibu hizo za malipo ziweze kufanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nimuhakikishie kwamba baada ya kuwa taratibu za uhakiki wa malipo, uhalali wa deni zitakapokuywa zimeshafanyika malipo yatafanyika. Yeye nimpongeze kwa kufuatilia kwa umakini na kwa ukaribu hoja zinazohusu wapiga kura wake; na siku akiwa na uchaguzi aniambie tu nitawasemea wapiga kura wake kwamba Jaku anapokuwa Bungeni hana mchezo na akipewa hoja za wapiga kura wake huhakikisha kwamba anazifanyia kazi kwa uzito unaostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wengi kama nilivyosema wameandika hoja zao kwa maandishi na hapa tulipo tunazo nyingi sana ambapo ni wengi sana. Kwa mujibu wa kanuni zetu nisingeweza kuwataja mmoja mmoja, lakini niwahakikishie kwamba hoja zenu kwa ujumla wake tumezipokea, tunawashukuru na tunazifanyia kazi na nyingine tutazitolea ufafanuzi kwa maandishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepokea pia hoja alizotoa Janet Mbene, tutazifanyia kazi na kuhakikisha kwamba tunatoa majibu. Amesemea ndugu yangu Ritta Kabati suala la gereza nililielezea na wakati ule wala asishike shilingi. Huo ndio uamuzi wa Serikali, mapendekezo hayo aliyoyatoa ndicho tutakachofanya na ameyasema. Ameandika ndugu yangu Oliver tutayafanyia kazi yale yote na wengine wote ambao sijataja ambao wako kwenye orodha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kutoa ufafanuzi wa hoja hizi, naomba kutoa hoja, ahsante sana kwa kunipa fursa.