Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Dr. Harrison George Mwakyembe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyela

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuishukuruKamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa ushauri na mapendekezo yake yanayolenga kuimarisha utendaji wa Wizara yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, aidha, namshukuru Waziri Kivuli na Msemaji Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni kwa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mheshimiwa Joseph Osmond Mbilinyi na Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia katika hotuba yangu kwa kauli na maandishi. Natambua kuwa Waziri Kivuli tuliyenaye safari hii ni mdau mkubwa wa sekta ya sanaa nchini hususani tasnia ya muziki, hivyo, maendeleo ya sekta hii yanamgusa moja kwa moja kiasi ambacho hata jina la Wizara yangu ameligeuza kwenye hotuba yake yote, badala ya kuita Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo anaiita Wizara ya Habari, Utamaduni, Wasanii na Michezo, nafikiri anajifikiria mwenyewe. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kusema kuwa Wizara yangu inaupokea ushauri wote uliotolewa hapa na itauzingatia katika utekelezaji wa bajeti yake ya mwaka 2017/ 2018. Hotuba yangu imechangiwa na jumla ya Waheshimiwa Wabunge 67 ambapo waliochangia kwa maandishi ni 30 na kwa kauli ni 37.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kazi nzuri sana aliyofanya Naibu Waziri, Mheshimiwa Anastazia Wambura ya kuzitolea ufafanuzi baadhi ya hoja zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge bado naamini kuwa muda nilionao ni mfupi sana sitaweza kuzitolea ufafanuzi hoja zote. Hivyo, naahidi kuzitolea ufafanuzi kwa maandishi na nitahakikisha kila Mheshimiwa Mbunge anapata nakala yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze na baadhi ya hoja za Kambi Rasmi ya Upinzani. Kwanza Msemaji Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani ukurasa wa tatu na wa nne wa hotuba yake anaeleza kuwa katika suaa la ulinzi wa uhuru wa habari, Tanzania tumepoteza sifa kabisa katika medani za Kimataifa na hivyo tuko kwenye orodha ya nchi zinazokandamiza uhuru wa habari duniani. Ushahidi wake ni utafii uliofanywa na Reporters Without Borders ambao amedai Mheshimiwa Waziri Kivuli kuwa umeiweka Tanzania nafasi ya 122 kati ya nchi 198 duniani zilizofanyiwa utafiti kuhusu uhuru wa habari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeisoma taarifa hiyo ya utafiti kwa makini (Press Freedom Index) inayoandaliwa kila mwaka, lakini mimi nimepata picha tofauti kidogo kwamba Tanzania tuko nafasi ya 83 badala ya 122 kati ya nchi 180 zilizofanyiwa utafiti huo. Kama ilivyo kila mwaka, Tanzania inaongoza katika Jumuiya ya Afrika Mashariki katika nafasi hiyo ya 83 maana Kenya inatufuatia nafasi ya 95 pamoja na kwamba waandishi wengi wa habari wanaotuma taarifa kuhusu ukandamizwaji Tanzania wengi wako Nairobi, lakini wao ni 95, Uganda wako 112, Sudan ya Kusini wenzetu wako 145 wamejitahidi sana nchi mpya ile imepata uhuru hivi karibuni, Rwanda 159, Burundi 160, nchi nyingi tunazoziheshimu nazo tumeziacha kwa mbali, Brazil ni 103, Nigeria ya 122, India 136, Malaysia 144, Urusi 148, Singapore
151, Uturuki 155 na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisemi kushika nafasi ya 83 basi tumefanikiwa sana, hapana hata kama tumezipita nchi 107 duniani. Ninachosema na naomba Waheshimiwa Wabunge mnielewe, laiti hawa Reporters Without Borders wangekuwa wanafanya utafiti wao kisayansi nina uhakika Tanzania tungekuwa tumeshika nafasi bora zaidi, nasema hivyo kwa sababu kuu tatu.

Kwanza, utafiti wanaoufanya hauangalii quality of journalism (ubora, weledi katika uandishi wa habari) ni kama wanaendekeza matumizi ya watu ambao hawajasomea uandishi wa habari (makanjanja) ambao hawajui maadili ya taaluma. Matokeo yake tunapata uandishi ambao hauna accuracy na nasema hili kwa masikitiko sana maana mimi ndiyo mwenzao katika Wizara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi nilikwenda kwenye sherehe za uhuru wa vyombo vya habari Mwanza. Amini usiamini nimetoa hotuba tena kwa pole pole, kwa kuzingatia hali ya magazeti yetu sasa hivi, magazeti yote sasa hivi yanashindwa kuuza hata asilimia 50 ya kile wanachozalisha ni kutokana na vyombo vya elektroniki kusoma magazeti hayo kwa undani mno, sasa kuna haja gani ya kununua magazeti? Kwa hiyo, nikaeleza jamani hebu tufuate kama nchi zingine zilivyo, tusome vichwa vya habari. Baada ya dakika 30 tu kutoka hapo taarifa ya chombo cha habari cha siku nyingi inasema Mwakyembe kapiga marufuku usomaji wa magazeti. Sasa niko mimi pale, tunaongelea uhuru wa vyombo vya habari na uhuru ndiyo huo inaccuracies.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu, wiki iliyopita ilikuwa siku ya Ijumaa, gazeti kubwa kabisa hapa ukurasa wa 30, sitalitaja wataona kama nawaonea lakini mliosoma mmeona. Ipo taarifa inasema, mke wa Malkia wa Uingereza astaafu. Hivi Malkia wa Uingereza ana mke? Unajua inaweza kutuletea matatizo makubwa hata ya kidiplomasia, gazeti linaandika hivi? Unajua katika uandishi wa habari tunahitaji sana sana uangalifu, mnafanya kazi muhimu ambayo watu wote wanategemea na Watanzania na dunia inawaamini, sasa mkifanya vikosa vidogo vidogo kama hivyo heshima itakuwa wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wewe angalia tu leo hii tuna msiba mkubwa katika Taifa letu, tena niwape pole sana Watanzania wote na wazazi waliopoteza watoto na ndugu zetu wote ambao leo wapo huko wakiomboleza, lakini mwandishi yeyote ambaye amesomea taaluma ya habari hawezi akatoa mbele mapicha tu ya watoto wamezagaa pale wameumia, wamelazwa, majani yamefunikwa unakuwa insensitive.

Mheshimiwa Spika, katika uandishi wa habari tunasema you have to minimize harm. Huo ndiyo uandishi wa Tanzania, ukiwaita kesho kuwahoji oooh uhuru wa habari unaingiliwa, wewe kasome brother ndiyo hicho tu utaelewa. Sasa hivi tuna mitandao ya jamii ambayo kila mtu tu ni mwandishi, jana alikuwa anauza sijui mikate kesho na yeye ni mwandishi, ni matatizo makubwa. Kwa hiyo, tuna kazi ya kudhibiti sekta hiyo lakini wenzetu hawa Reporters Without Borders hawaangalii haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, utafiti huu haurutubishwi na ushahidi wa kimazingira (circumstantial evidence) kwamba inakuwaje kwa mfano nchi ina ukandamizaji mkubwa wa uhuru wa vyombo vya habari kama Tanzania inavyosemekana bado ni moja ya nchi bora katika Bara la Afrika ambayo inavutia uanzishwaji mkubwa wa vyombo vya habari, ni moja ya nchi inayoongoza katika Bara la Afrika hata duniani tupo katika orodha. Leo hii Tanzania ina majarida 428, ina redio 148, vituo vya television 32, watumiaji wa mitandao wako takribani milioni 20 na line za simu milioni 41, ni nchi gani yenye ukandamizaji unaweza ukakuta rutuba ya namna hiyo ya vyombo vya habari? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu, freedom index inaangalia vigezo vitatu vikuu; cha kwanza wanaangalia uhuru wa vyombo vya habari; pili, wanaangalia ulinzi na usalama wa waandishi wa habari, lakini kwa kuangalia kwanza sheria zilizopo nchini na kuongea na wadau mbalimbali. Kigezo cha tatu wanakiita level of pluralism hata kwa kiswahili kutafsiri vizuri, ni uhuru pengine wa ujumla katika jamii (diversity). Katika hicho kigezo Watanzania muelewe mtapoteza point kila siku. Mimi nitatoa mfano kwa sababu tunawaudhi wakubwa, Watanzania shida yetu ambayo mimi nasema lazima tujivunie ni kwamba hatuwezi kukubali kuyumbishwa tukaua utu, uhuru na utamaduni wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano, mwaka jana Tanzania iliitwa Geneva mbele ya Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa kutetea rekodi yake ya Haki za Binadamu, tulikuwa tunakabiliwa na masuala 227. Naomba nichukue fursa hii kumpongeza sana Mwamasheria Mkuu wa Serikali, Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Katiba na Sheria, Profesa Mchome na wataalam wote wa sheria walioko pale kwa sababu ilibidi kukaa chini kuangalia je, tukubali kuyumbishwa ama tusimamie misimamo ya nchi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kifupi tulikubali kutekeleza masuala 131 ambayo yamo kwenye programu ya utekelezaji wa nchi yetu, ni mengi tu kwa mfano, kuondoa tozo kwa ajili ya vyeti vya watoto, kushughulikia kwa mfano suala la Sheria ya Ndoa ambalo na sisi wenyewe it is a problem, sisi tuko tu kwenye mchakato lakini masuala mawili tulikubali kidogo tukasema tuyaangalie lakini masuala 94 tuliyakataa katakata ili kulinda utu, uhuru na utamaduni wetu. Nitawatolea mifano ya baadhi ya mashinikizo kama ifuatavyo:-

(i) Kuhalalisha utoaji mimba, tukasema msitushinikize sasa hivi. (Makofi)

(ii) Kufuta ndoa za wake wengi, tukasema hapo mnaingilia utamaduni wetu, mnaingilia imani zetu, hatukubali. Hata kama mnaondoa sijui hiyo misaada iondoke. (Makofi)

(iii) Tukubali ndoa za jinsia moja, tukasema hilo over our dead bodies pengine tufe wote kizazi hiki waingie hao ambao watakubali upuuzi wa aina hiyo, tumekataa Tanzania lakini ukikataa wakubwa wapo. Lobbying ya masuala hayo ni kubwa katika dunia. (Makofi)

(iv) Tukubali haki za mashoga na tuutambue ushoga kama ni haki ya binadamu, tukasema hapana. (Makofi)

(v) Tuliondoe suala la ushoga kwenye Sheria zetu za Adhabu, tukakataa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuwambia Watanzania, the gay and lesbian lobby in the world is very strong, wana pesa hao. Ukiwafanyia fujo wanakuyumbisha kila sehemu. Mimi nilijua tutapunguziwa marks ndiyo wanaotoa pesa kwenye mashirika mengi yanayotufanyia assessment. Kwa hiyo, Watanzania tuwe macho, mara nyingine hizi statistics lazima tuziangalie kwa macho mwili kama Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikimbile suala lingine muhimu ambalo Msemaji Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani amenukuu ukurasa wa tano wa hotuba yake akisema Ibara ya 19(2) ya Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kiraia na Kisiasa na kuonyesha jinsi ibara hiyo inavyotoa haki ya kujieleza, ya kutafuta, kupata na kusambaza taarifa kwamba haina vikwazo vyovyote na kwamba maudhui yake yamerudiwa katika Ibara ya 18 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mimi nimekubaliana naye kabisa Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani kuhusu ile Ibara ya 18. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja hii aliisisitiza zaidi Mheshimiwa Tundu Lissu kwa kusema Ibara ya 18 haina clawback clause yaani kipengele kinachobana au kudhibiti haki hiyo. Picha hii ya kwamba vipengele hivi vinabeba haki na uhuru usio na mipaka inatokana na mdogo wangu Mbilinyi, Waziri Kivuli kusoma Ibara moja tu yaani Ibara ya 19(2) ya huo mkataba hakwenda Ibara ndogo ya (3). Angeenda Ibara ndogo ya (3) angekuta kuna masharti ya kutekelezwa, masharti hayo yanasema, kwanza, haki hii utaitekeleza lakini kwa kuheshimu haki na heshima ya watu wengine na pili kwa kulinda usalama wa Taifa, afya na maadili. Kwa hiyo, hakuna haki isiyo na mipaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 18 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, vilevile katika kutafsiri Katiba, najua Mheshimiwa Tundu Lissu amefanya makusudi tu, anaelewa, huwezi ukatafsiri Katiba kwa kipengele kimoja kimoja. Kila kipengele cha Katiba ni sehemu ya tungo moja ambapo vipengele vyote lazima uviweke juu ya meza, uvisome kwa pamoja kuelewa maana ya kila kipengele. Any constitutional provision is but a component in an ensemble of interacting provisions which must be quote or brought into play as part of a larger composition. Hii ni principle wanasheria wote wa constitutional law wanajua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 18 lazima isomwe na Ibara ya 30 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayosema, katika kufurahia haki na uhuru wako hakikisha huathiri haki na uhuru wa wengine, huathiri maslahi ya umma na huathiri usalama wa Taifa lako. Kwa hiyo, hiyo ndiyo mipaka nilitaka tu kusisitiza hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwakumbushe Waheshimiwa Wabunge wote hapa kwamba mwaka 2004, nchi za Kiafrika ziliamua kuunda Mahakama ya Haki za Binadamu ya Afrika. Nchi zilikuwa 30 na mojawapo ilikuwa Tanzania. Tungekuwa nchi ya ukandamizaji wa haki za binadamu tusingeweza kukubali kuanzisha mahakama hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini siyo hivyo tu, kuna kipengele kinachosema, nchi lazima ikubali ili raia wake wanapokuwa wamekwazwa wataleta mashauri yao kwenye mahakama hii. Ni nchi saba tu toka mwaka 2004 zimesaini kuweza kushtakiwa na watu wake Tanzania nayo imo. Sasa jamani nchi ambayo inajiona kwamba iko notorious katika ku-abuse human rights inaweza kweli ikakubali kuingia kwenye kifungu hicho?(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ukiangalia yote haya unaweza hata kushangaa kwamba hii ndiyo Serikali ya kuteka waandishi wa habari? Nafikiri tunabangaiza tu hoja mpaka jana nimeshangaa tu kusikia hata eti Katibu Mkuu wa CCM ametekwa? Yaani imekuwa sasa utani nchi hii ukiitwa na polisi umetekwa, mtu amefumaniwa huko ametekwa, tunafanya mzaha kwenye kitu muhimu sana katika jamii yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kusema kwamba Edward Snowden ambaye amekimbia nchi yake 2013 kujificha Urusi hakimbizwi na Serikali ya Tanzania, anakimbia Marekani kwa kuvuka mipaka, unavuka mipaka. Siyo hivyo tu, tuna Julian Assange ambaye toka mwaka 2012 nafikiri anakaa kwenye kachumba kamoja tu kwenye Ubalozi wa Equador, anakimbia wakubwa, kote kuna mipaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi nilipokuwa Mwanza tumekaa kidogo na kijana wangu mmoja mwandishi nikamwambia nakupa swali. Je, ni nchi gani ambayo watu 230 pamoja na waandishi sita walikamatwa kwa kufanya maandamano wakati wa kuapishwa kwa Rais wa nchi yao? Akasema Tanzania.Nikamuuliza lini? Akafikiri sana. Baadaye nikamwambia hapana, huyo Rais ameapishwa mwaka huu, akashindwa. Nikamwambia ilikuwa ni Marekani. Alisema haiwezekani.

Mheshimiwa Spika, ndiyo tatizo tulilonalo Waafrika tunaamini kwamba chochote cha nje ni bora cha kwetu siyo bora. Watu 230 walikamatwa na wakiwa waandishi wa habari sita na wakafunguliwa mashtaka. Hayo tunafikiri yanafanyika Tanzania tu, yanafanyika nchi za Kiafrika lakini sisi kwa kweli tuko katika nchi inayojitahidi sana katika kuheshimu haki za binadamu za wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii vilevile imebaini kuwa Kanuni za Urushaji wa Matangazo ya Dijitali na Kanuni za Leseni zitazuia uwepo wa channel za umma yaani public broadcaster katika vifurushi vya matangazo ya Direct To Home (DTH). Jambo hili hili limeongelewa na baadhi ya Waheshimiwa Wabunge ambao kwa kweli kwenye majibu yangu ya maandishi nitawataja wote.

Mheshimiwa Spika, naona kama tumewahi kidogo lakini naomba niseme kwamba kanuni mpya ambazo zinapendekezwa hapa hazitaawaathiri watumiaji wa channel za umma kwa kuwa wataendelea kuwa na haki ya kupata matangazo ya televisheni za umma hata baada ya vifurushi vya kawaida vya kulipia kumalizika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipindi kilichopita Waheshimiwa Wabunge kilikuwa cha mpito, kwa hiyo, kilikuwa na matatizo mbalimbali ambayo lazima tuyavumilie. La msingi hapa ni kuwa hizo zinazoitwa kanuni ni mapendekezo ya kanuni ambayo wamepelekewa wadau wayaangalie halafu wayarudishe Serikalini, halafu kinaendeshwa kikao cha pamoja cha kujadiliana. Nafikiri tumewahi mno, tumeleta wasiwasi mapema sana kabla ya kufika tunakotakiwa kufika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwepo na suala la upungufu kwenye Sheria ya Haki Miliki. Wizara yangu imeona umuhimu wa kufanya marekebisho ya sheria, sio tu ya Haki Miliki lakini sheria zote katika sekta hizi kwa mfano sheria inayogusa tasnia ya filamu na sanaa ikiwemo Sheria ya Filamu na Michezo ya Kuigiza Namba 4 ya mwaka 1976 na Sheria ya Baraza la Sanaa la Taifa Namba 23 ya mwaka 1984. Tayari Wizara imeshaanza kuchukua hatua kwa kuanza uandaaji wa marekebisho ya sera ili kukidhi matakwa ya sasa. Kwa upande wa Sheria ya Haki Miliki tunashirikiana na Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji tuweze kuifanyia marekebisho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwepo na suala la Serikali iwezeshe timu za Taifa ili ziweze kufanya vizuri katika mashindano mbalimbali, hayo ni mawazo ya Kamati. Sisi tunaikubali hiyo changamoto na tayari tunafanya hivyo. Serikali imeendelea kutenga bajeti kila mwaka hata kama sio toshelezi. Mfano mdogo tu ni kwamba mwaka 2016/2017 tuliweza kugharamia wanamichezo wote saba walioshiriki katika Olympic nchini Brazil.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka kesho mwezi Aprili tuna mashindano ya Jumuiya ya Madola yatafanyika Australia. Tayari Serikali ipo kwenye mazungumzo ya mwisho na nchi za Ethiopia kwa ajili ya kupeleka wakimbiaji wetu (wanariadha wetu); Cuba kwa ajili ya kupeleka timu yetu ya ngumi na vilevile China kwa ajili ya wachezaji wetu wa mpira wa meza. Hizo zote ni juhudi za Serikali na mwaka 2019 nilishalisema hili kwamba sisi ni wenyeji wa mashindano ya AFCOM kwa vijana wa chini ya miaka 17. Tayari timu yetu ya vijana wa miaka 13 – 14 ipo kambini. Ikifika mwaka 2019 watakuwa tayari wana miaka 16 - 17. Kwa hiyo, Serikali inafanya juhudi na tumelizingatia hilo vilevile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna suala la Kambi ya Upinzani na Mheshimiwa vilevile Mheshimiwa Devotha Minja alilisema hili kwamba kuyumba kwa uchumi kunakotokana na sera za Serikali za Awamu ya Tano, kumeiathiri sekta binafsi ya habari na vyombo vya habari sasa hivi vinapunguza wafanyakazi.

Mheshimiwa Spika, naomba niseme tu mnielewe, si kweli hatua za kimageuzi zinazochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Tano kwamba zimeleta matokeo hasi. Mageuzi haya yameleta matokeo mengi chanya ikiwemo kuongezeka mapato ya Serikali na kutekeleza miradi mingi tena mikubwa ya maendeleo ambayo wote tunaijua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, madai kwamba ni sera za Serikali ya Awamu ya Tano zinafanya vyombo vya habari kuanza kupunguza wafanyakazi, kwa kweli kama nilivyosema si kweli. Naomba niulize kama wote mnafuatilia vizuri mitandao na vyombo vya habari, mwezi Julai, 2015 Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC) lilitangaza kupunguza wafanyakazi 1000, Serikali ya Awamu ya Tano ya Tanzania haikuhusika.

Mheshimiwa Spika, Machi 2017, Shirika la Habari la ESPN lilipunguza wafanyakazi 100, mtandao wa Twitter ulipunguza asilimia tisa ya wafanyakazi wake wote, tena ilikuwa ni Oktoba, 2016. Kati ya mwaka 2010 hadi 2016 CNN yenyewe imeshapunguza zaidi ya wafanyakazi 100 wakiwemo wahariri na wachambuzi waandamizi. Yote haya ni matokeo tu ya uchumi wa dunia hayahusiani kabisa na Serikali ya Awamu ya Tano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la Bunge live ambalo tumelijibu, tumelijibu, tumelijibu imefika mahali naomba sasa nilielekeze kwa Bunge, after all nina taarifa kwamba tayari TCRA imewakabidhi Bunge leseni sasa hivi wana uwezo wa kufanya chochote wanachotaka. Kwa hiyo, naomba hili nilielekeze huko badala ya mimi kujibu baadaye mtasema ulisema, ulisema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kambi Rasmi ya Upinzani inasema Serikali iache kuangalia mtandao wa kijamii kwa jicho hasi bali ionekane kama sehemu ya ajira ili kukuza kipato. Hivyo ndivyo tunavyofanya, tumejenga mazingira mazuri ya mitandao na Watanzania ambao wapo kwenye mitandao kwa sasa ni mamilioni. Tunachosema hapa ni matumizi mabaya ya mitandao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwanasiasa maarufu wa Marekani nafikiri Hillary Clinton alisema mwezi Desemba, 2016 kuwa matumizi mabaya ya mitandao ni ugonjwa hatari unaoweza kuteketeza dunia. Alisema hivyo kwa sababu mwezi Desemba 2016 kulikuwepo taarifa kwenye mitandao kwamba Serikali ya Israel inasema itaipiga Pakistan ikipeleka askari Syria. Pakistan wakajibu jaribu na sisi tutakushughulikia, kuja kugundua ni maneno wala hayajatoka Israel. Kwa hiyo, kwa kweli mitandao ya jamii kama hatujaidhibiti inaweza kutuingiza katika matatizo makubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wengi mtakumbuka kisa cha kijana wa kiingereza aitwaye Liam Stacey aliyetumia vibaya uhuru wake wa habari na mnajua kwamba hivi karibuni tu amemaliza kifungo chake baada ya Mahakama ya Mjini Swansea kumkuta na hatia ya kumkashifu mchezaji wa zamani wa Bolton Wanderers mwenye asili ya Afrika Fabrice Muamba aliyekuwa ameanguka uwanjani baada ya kupata shambulizi la ghafla la ugonjwa wa moyo. Kwa hiyo, sio sisi tu ambao kwa kweli tunahangaika namna ya kudhibiti hata wenzetu wanafunga lakini tunaambiwa sisi tu Tanzania ambao tumewapeleka watu mahakamani, lazima tufanye hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kambi Rasmi ya Upinzani na Mheshimiwa Profesa Jay (Mheshimiwa Joseph Haule) na Waheshimiwa Wabunge wengi wamesema Serikali inawapuuza wadau wa masuala ya sanaa hasa baada ya kuwatumia kwenye chaguzi mbalimbali. Serikali haijawahi kuwapuuza wasanii nchini na kama nilivyosema kwenye hotuba yangu kwa kweli tumechukua hatua mbalimbali ya kuwajengea weledi, kwa kuwatambulisha na kuwakutanisha na wadau wa maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe wito tu kwa baadhi ya vyama vya siasa ambavyo kwa kweli wanasiasa wao wanawachochea hawa vijana kuimba nyimbo za kisiasa, hii ni entertainment industry. Mimi naomba vijana wangu wanisikilize, nimewaambia wanipe mfano wa mwanamuziki yeyote duniani aliyefanikiwa kwa kutukana viongozi, nimewaambia hivyo.

Mheshimiwa Spika, mimi nimeenda Nigeria, wasikilize P-Square, Tiwa Savage, Davido, Don Jazzy, ni vijana ambao wengine wamenunua mpaka ndege, very successful lakini nimewaambia hebu niambie umewahi kusikia wanasema ooh Mr. President your wrong. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimewaambia wewe imba nyimbo ambazo zitakuletea mafanikio mwenyewe. Kama unataka siasa nenda kagombee Udiwani huko au kagombee nafasi yoyote huko, hii nientertainment industry siyo political industry na wengi wamenilewa. Angalia Afrika Mashariki akina Chameleon kuna wimbo wowote Chameleon anaongelea Serikali ya Uganda? Nani successful musician hapa anafanya hivyo, namfahamu mmoja tu, alijitia mwanasiasa Fela Ramsome Kuti lakini aliishia pabaya sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tuna vijana wanang’ara hapa kina Diamond, Ally Kiba, sikiliza nyimbo zao hakuna hata moja wanaongea mambo ya kipuuzi sijui anajifanya mwanasiasa, utakuwa mwanasiasa wewe? Mimi naomba kazaneni kuboresha vipaji vyenu, let me tell you vijana wangu the sky is the limit. Mimi nimewahakikishia nitawasaidia kwa kila hali muweze kufika anga ya juu kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoja hapa ambayo imeongelewa na Mheshimiwa Sakaya, Kambi ya Upinzani, Mheshimiwa Shekilindi, Mheshimiwa Sixtus Mapunda kwamba Serikali iwekeze katika michezo kwani haiwezi kutegemea mafanikio bila kuwekeza fedha. Nafikiri hili suala nimeshaliongelea, kwa kweli uwekezaji ni suala ambalo tunaliona ni muhimu sana tena sana na tunalifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kitu kimoja tu, nilikuwa naongelea kuhusu vijana wangu wa muziki tunapenda mno kulalamika. Nichukue fursa hii kuwapongeza vijana wawili wasanii, Ndugu Hamis Mwinjuma (Mwana FA) na mwenzake Ndugu Ambwene Yessaya (AY) ambao badala ya kulalamika wameibeba Kampuni kubwa ya Tigo kuipeleka mahakamani kwa sababu imekuwa ikitumia miziki yao kama ringtones kwa muda mrefu na Mahakama ya Ilala ikaiamuru Kampuni ya Tigo kuwalipa wale vijana zaidi ya shilingi bilioni 2.185, wame-appeal iko High Court. Mimi nasema vijana wa Tanzania tukiwa namna hiyo (pro-active) siyo kukaa tu kutunga ngonjera za kulalamika, tutafika mbali sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imetunga sheria kandamizi za uhuru wa habari mfano Cyber Crime Act, Sheria za Huduma za Habari hivyo zibadilishwe. Mheshimiwa Tundu Lissu, Mheshimiwa Joseph Mbilinyi, Mheshimiwa Devotha Minja, Mheshimiwa Godbless Lema, Mheshimiwa John Mnyika na wengine ambao nitakuwa nimeruka majina yao wameliongelea suala hili. Tofauti na mtizamo wa watu wachache sheria hizi zinalinda uhuru wa wanahabari na wananchi na kwa sasa zimethibitishwa hata na Mahakama Kuu kuwa ni sheria nzuri na hazikiuki Katiba ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mwanza katika uamuzi wake nimeona niupitie huu wa Machi 9, 2017 kuhusu Shauri la Madai Na. 2 la mwaka 2017, Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania na Hali Halisi Publishers Ltd. dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mheshimiwa Jaji De-Melo alitupilia mbali shauri la kupinga Sheria za Huduma za Habari kwa kuwa walalamikaji hawakuwa na hoja za msingi na taratibu za kisheria kupinga sheria hiyo.

Mheshimiwa Spika, vilevile Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam katika Shauri la Kikatiba Na. 6 la mwaka 2016 kati ya Jamii Media Company Ltd. dhidi ya Attornery General na IGP, kwa kweli uamuzi uliotolewa na Majaji Kitusi, Koroso na Khalfani ulikuwa ni mzuri. Uamuzi huo ulisema licha ya kasoro ndogo ya utoaji wa dhamana walifikia hitimisho kuwa Sheria ya Makosa ya Mitandaoni ya mwaka 2015 haikiuki misingi ya Katiba wala haki za watu kujieleza. Hukumu hii imezima rasmi hisia na mawazo ya kuwa sheria hizi ni mbaya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesikia kengele imegonga sipendi sana uniambie mara ya pili. Mambo mliyoyasema ni mengi, naomba nizungumzie lugha ya kiswahili. Tumempongeza Mheshimiwa Rais kwa kutumia lugha ya kiswahili mara kwa mara na naomba viongozi wote tuige na tuongee kiswahili sanifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kwa upande wetu Baraza la Kiswahili la Kitaifa nalo linafanya juhudi kubwa, limetoa kamusi nyingi na sasa wametoa Kamusi standard, hii hapa, ningetamani kila Mheshimiwa Mbunge apate. Ni kamusi ya kisasa, ni kubwa na imekubalika na nchi nyingi za Kenya, Uganda na nchi zingine. Naomba Mwenyekiti ufikishe ombi langu kwa Mheshimiwa Spika ukimkata Mheshimiwa Mbunge hela kidogo tu shilingi 25,000 kila mmoja atakuwa kwenye pigeon hole ana kamusi hii, naomba sana iwe hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna suala moja ambalo ameliongelea mdogo wangu Kubenea, mwandishi wa habari wa siku nyingi, analalamika kwamba nimewakatisha tamaa wanahabari kwa kusema asilimia 90 hawana weledi. Sio mimi, ndiyo shida hiyo, sasa huyu anayeongea ni mwandishi wa habari wa siku nyingi lakini amekaa na hiki kitabu siku tatu hata kuelewa hajaelewa, ananishangaza sana Mheshimiwa Kubenea.

Mheshimiwa Spika, naomba nisome, wala siongelei magazeti hapa, yeye anasema nimewasema watu wa magazeti. Nimesema kwamba Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania inaendelea kusimamia ubora wa huduma za utangazaji (broadcasting quality of service) na ndiyo waliofanya utafiti kwa vituo vyote vya redio na television, yeye anamfikiria Mwanahalisi hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania wanasema katika ukaguzi uliofanywa asilimia 90 ya wafanyakazi wamebainika hawana sifa stahiki katika taaluma ya uandishi wa habari na utangazaji katika vituo vya redio na television. Vilevile nimkumbushe Mheshimiwa Kubenea hiyo inakuja pia kwa waandishi wa habari, tumewapa miaka mitano nendeni shule ndugu zangu, dunia imebadilika sasa hivi. Haiwezekani umetoka darasa la saba tu unakuwa mwandishi wa habari eti nawe unatafsiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku moja niliona clip moja kijana mmoja anatafsiri alikuwa anaongea na Mmarekani mmoja mtalii, yule mtalii anasema waambie Watanzania nchi yao ni nzuri, yeye anasema ninyi Watanzania mnapenda kuomba chakula tafuteni ninyi wenyewe chakula. Kwa hiyo, mimi naomba tuwe na weledi katika tasnia hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie tu kwa kusema hoja zenu zote sisi tutazifanyia kazi na kuzigawa kwa kila Mbunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja.