Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Spika, pongezi kwa kuweka mikakati mizuri na endelevu ya kuinua vipaji katika michezo kuanzia vijana wa miaka 13. Hii itatuhakikishia kupata wanamichezo mahiri wa kitaifa na kimataifa.

Mheshimiwa Spika, rai yangu; michezo hii iwe ya aina mbalimbali sio soka na netball peke yake bali izingatie riadha na michezo mingine. Timu hizi zizingatie jinsia ili kupata vijana wa kike na wa kiume katika michezo. Timu zizingatie watu wanaoishi na ulemavu na kuwawezesha. Suala la michezo ya wanawake halijapata kushughulikiwa ipasavyo na Serikali.

Mheshimiwa Spika, michezo mingi ni ile ya netball lakini wanawake wana uwezo wa kushiriki katika kila mchezo lakini hawawezeshwi. Kwa mfano, sasa hivi Timu ya Mpira ya Wanawake ya Chalinze ndio mabingwa wa Taifa lakini hawana uwezeshwaji na wamekwama kuendelea na mazoezi na hivyo kuhujumu fursa zilizopo mbele yao. Tunaiomba Serikali iwahudumie hawa wachezaji wa Timu hii ya Wanawake ya Chalinze badala ya kumuachia Mheshimiwa Salma Rashid Kikwete peke yake. Serikali iweke mkakati wa kujumuisha wanawake katika maendeleo ya michezo.

Mheshimiwa Spika, utamaduni; Serikali izingatie tamaduni zilizopo Tanzania na kuzifanyia kazi zile ambazo zinajenga heshima na maadili mema na kuzidumisha kwa kuzifundisha shuleni na kwenye sherehe mbalimbali, wakati huo huo wakiwaasa wananchi dhidi ya mila na tamaduni zinazodhalilisha watu kijinsia, kidini na kikabila.

Mheshimiwa Spika, ngoma zetu zidumishwe lakini wachezaji wavae nguo za heshima wakati wa kucheza, sio lazima watu wawe nusu uchi. Wizara ifanye kazi na Wizara ya Elimu na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto.

Mheshimiwa Spika, kuunganisha juhudi za Wabunge na Serikali; Wabunge wengi wamekuwa wakitoa jezi na vifaa vingine vya kuwezesha michezo majimboni lakini wamekuwa wakifanya hivyo katika mazingira magumu maana majimbo yetu hayana viwanja vizuri vya michezo na hata baada ya kupata timu nzuri au wachezaji wazuri, hakuna mwendelezo maana hatuna Maafisa Michezo kwa hiyo usimamizi ni mgumu. Tunaomba Wizara itupatie utaratibu mzuri wa kuibua vipaji kwenye majimbo yetu.

Mheshimiwa Spika, majimbo yaliyopo kwenye maeneo ya milima yana uwezekano mkubwa ya kuzalisha wanariadha. Tunaomba maafisa michezo na vifaa vya kusaidia hilo.

Mheshimiwa Spika, kushirikisha Sekta Binafsi; michezo ni biashara kwa hiyo Serikali ifanye tathmini ya namna ya kushirikisha Sekta Binafsi, sio kufadhili timu ili kujitangaza bali kuwa na timu kikamilifu, kuajiri makocha, kufadhili viwanja vya michezo na kuziendesha ili Serikali ibaki kuweka mazingira mazuri kisheria na kisera. Serikali iwezeshe kutafuta wenye vipaji watakaochukuliwa na Sekta Binafsi kwenye timu za michezo mbalimbali, kwa mfano, Serikali itenge fedha ya kusomesha Maafisa Michezo vyuo vikuu, Makocha, Walimu wa Michezo, Waongoza Filamu, wataalam wa sanaa na utamaduni na filamu.

Mheshimiwa Spika, kwa kutumia maliasili zetu katika uwekezaji katika filamu, watengenezwe maeneo ya mbuga zetu, miji yetu, vijiji vyetu, milima yetu, maziwa yetu, mito na bahari na kutoa leseni/ vibali, hatimiliki kwa ajili ya kuja kutengenezea filamu. Hii itauza nchi yetu na kuviweka kwenye ramani ya medani za filamu nchini, vilevile inawezesha Watanzania kuajiriwa kwenye filamu na documentary hizi, wakati huo huo wakilipatia Taifa kipato kikubwa.

Mheshimiwa Spika, Wizara ishirikiane na Wizara ya Maliasili na Utalii pamoja na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kuona jinsi hili litakavyofanywa. Nchi yetu ilishawahi kutumika kutengeneza filamu lakini ilikuwa kabla ya uhuru lakini sasa mazingira ni mazuri zaidi, kwa hiyo Wizara itumie fursa hii kikamilifu.

Mheshimiwa Spika, magazeti na TV; Tanzania ina uhuru uliopitiliza wa habari kwa maoni yangu na kwa kweli kuwa na magazeti mengi sio tu kueleza lakini ni chanzo cha matatizo mengi yanayotokana na tasnia hii ya uandishi maana uandishi wa vyombo vyetu vingi hauridhishi hata kidogo. Kwanza ni lugha inayotumika, utafiti mdogo ungefanywa kwenye mambo mengi ya kiuchumi, kisayansi, kiteknolojia na kijamii. Wote wanaandika taarifa za kuambiwa, hakuna anayefanya utafiti na kutoa ripoti inayofundisha wananchi.

Mheshimiwa Spika, waandishi wetu wengi hawana ujuzi wa kutosha kwenye uandishi wa taaluma kiasi kwamba wawe wamebobea katika fani maalum. Suala la kuandika makala yasiyofanyiwa utafiti linaleta usumbufu, udhalilishaji na maumivu kwa wananchi wengi na hii haikubaliki. Tunaitaka Serikali ichukue hatua kali za kisheria kukomesha hili huko tunakokwenda.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.