Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Saed Ahmed Kubenea

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Ubungo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nakushukuru kwa kunipa nafasi nami nichangie mjadala huu.

Kwanza kwa niaba ya Waandishi wa Habari wenzangu, wamiliki wa vyombo vya habari, Wahariri na wadau wote wa habari, natoa pole kwa msiba mkubwa uliolikumba Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, napenda nizungumzie suala la uwanja wa Taifa wa Dar es Salaam. Uwanja wa Taifa umekabidhiwa ndani ya kipindi cha miaka mitano. Uwanja ule umejengwa kwa dola za Kimarekani milioni 50. Ni uwanja wa tatu kwa ukubwa katika Bara la Afrika, lakini uwanja wa Taifa umekabidhiwa ukiwa haujakamilika. Kwenye eneo la jukwaa kuu ambalo linaitwa VIP, ikinyesha mvua watu wote waliokuwepo pale wanaloa kana kwamba umesimama kwenye mnazi. Ushahidi ni mvua hii inayonyesha Dar es Salaam sasa hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa zilizopo ni kwamba mkandarasi alitakiwa ajenge ule uwanja kwa kuweka paa maalum ambalo litakuwa linafunga na kufungua ili wakati wa mvua lile paa liweze kutumika kuzuia mvua isinyeshee. Sasa uwanja umekabidhiwa, sherehe zimefanyika bila eneo hilo kukamilika.

Mheshimiwa Spika, pia katika eneo hilo, ulikuwepo mfumo wa ukusanyaji mapato na uwanja ulikabidhiwa bila mfumo huo kukamilika, lakini Serikali hii ya sasa hivi ikafuatilia utaratibu huo na ikaona kwamba ule mfumo unaweza ukawekwa na wajenzi na umewekwa na tumeokoa zaidi ya shilingi milioni 900 bila fedha za Serikali.

Mheshimiwa Spika, kwa nini usifanyike utaratibu mzuri, waliojenga uwanja ule wakaukamilisha tukaendelea na shughuli zetu bila mgogoro? Inawezekana kwamba ama waliopewa mamlaka ya kusimamia uwanja hawakuwa na uwezo wa kusimamia uwanja ule vizuri wakati wa ujenzi ama walihongwa ili uwanja ule usikamilike vizuri.

Mheshimiwa Spika, sasa hatuna sababu ya kufukua makaburi, lakini ni muhimu Uwanja wa Taifa ukaangaliwa vizuri kwa sababu watazamaji au watu wanaofika uwanja wa Taifa wanaloa mvua na ushahidi wa mechi ya juzi kati ya Simba na Azam watu wote waliokuwepo pale uwanjani waliloa kama vile wamesimama kwenye mnazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna suala hapa ambalo Mheshimiwa Waziri wakati anazungumza sikuwepo, lakini nimesoma vyombo vya habari. Gazeti la Habari Leo limesema Mheshimiwa Waziri amesema Waandishi wa Habari asilimia 90 hawana sifa. Sasa najiuliza, sijui utafiti gani ambao Mheshimiwa Waziri ameufanya kwamba asilimia 90 ya Waandishi wa Habari waliopo hawana sifa na sijui sifa ambayo Mheshimiwa Waziri anaizungumzia ni ipi? Kwa sababu wapo Waandishi wa Habari ambao wamepata mafunzo mazuri kwenye vyombo vya habari na wao leo wamekuwa Waandishi wa Habari, wanafanya kazi na wanaongoza vyombo vya habari.

Mheshimwa Spika, Mheshimiwa Waziri Dkt. Mwakyembe, Mwandishi wa Habari, anafahamu hili. Alipomaliza masomo yake ya Kidato cha Sita alikwenda kufanya kazi kwenye chombo cha habari. Wakati huo au mpaka sasa sina hakika, ila nahisi mpaka sasa Mheshimiwa Dkt. Mwakyembe hajawahi kusomea Uandishi wa Habari. Kama nakosea, Waziri wangu, kaka yangu atanikosoa, lakini ndivyo ninavyofahamu mimi.

Mheshimiwa Spika, elimu peke yake haitoshi kuwa na Waandishi wa Habari wazuri na mzungumzaji aliyepita hapa alizungumzia mambo ya ukocha kwamba kuwa na vyeti tu hakumfanyi mtu awe kocha mzuri. Kwa hiyo, ni vizuri kauli kama hiziā€¦

SPIKA: Mheshimiwa Kubenea, sikukatishi lakini nia yangu ni kukupongeza tu. Hii habari ya vyeti tu halafu mkija hapa, ooh Bashite, Bashite!

Mheshimiwa Kubenea endelea tu. (Makofi)

MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Ninachotaka kusema ni kwamba tunaweza tukazungumzia vyeti na hatukatai vyeti, lakini tunachozungumzia, misingi, uadilifu, uaminifu mzuri wa mtu, elimu peke yake haitoshi. Ni lazima tujenge Waandishi wa Habari. Sasa kauli hizi zinaweza zikachukuliwa na Waandishi wa Habari na zimetolewa na Waziri mwenye dhamana ya tasnia ya habari ambaye anapaswa kwa vyovyote vile kulinda Waandishi wa Habari kwa gharama yoyote ile, sio kuwakatisha tamaa.

Mheshimiwa Spika, kuna suala hapa la Waandishi wa Habari kufanya kazi katika mazingira magumu sana. Waandishi wa Habari wanatishwa, hawako huru, wanaminywa na sheria nyingi mbaya ambazo zinaminya uhuru na haki ya Waandishi wa Habari kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mfano hai ni huo ambao wewe umeuchukulia wa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam ambaye aliingia kwenye chumba cha habari akalazimisha habari itoke. Ripoti imeandaliwa na Mheshimiwa Nape, Kamati ya Mheshimiwa Nape iliyoundwa na Mheshimiwa Nape inaongozwa na Mkurugenzi wa Idara ya Habari, Maelezo, ni Doctor, ni Mwanasheria, ni Mhariri, amefanya kazi Mashirika ya Kimataifa. Haiwezekani mtu wa namna hii akafanya kazi bila weledi kama ambavyo Mheshimiwa Waziri amesema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Kamati imeongozwa na Jesse Kwayu, Mhariri wa magazeti mengi nchi hii amepitia. Amekuwa kwenye media zaidi ya miaka 20; kizazi kingi hapa cha Uandishi wa Habari amekifundisha. Haiwezekani Jesse Kwayu akafanya kazi chafu isiyo na weledi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa aliitwa kwenye Kamati; akakataa, Kamati ilitaka kutoa ripoti kesho yake, ikasitisha ili imhoji Mkuu wa Mkoa. Mkuu wa Mkoa akakimbia Kamati. Uandishi wa Habari unaelekeza, tafuta source, akikosekana unasema. Huwezi kuua story kwa sababu mtu amekosekana. Makonda ameikimbia mwenyewe Kamati. Mheshimiwa Waziri anasema hawezi kutumia Ripoti ya Kamati ambayo haina weledi.

Mheshimiwa Spika, mimi sina ugomvi na Dkt. Mwakyembe, akikataa kutumia ripoti, huo ni utashi wake, lakini nina ugomvi naye anapochanachana na kuikosoa hii ripoti. Akatae kutumia, aseme sitaki, basi! Asibeze kazi ya kitume iliyofanywa na Kamati hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Kamati hii imefanya kazi ya kitume. Serikali hii ambayo Mheshimiwa Dkt. Mwakyembe anaongoza, haikuhoji watu ambao walikuwa na vyeti feki. Wanalalamika, lakini ripoti ya vyeti feki imetolewa hadharani. Magazeti yameagizwa yaandike hiyo ripoti na magazeti hayo yamechapisha hadharani. Waziri wa Habari anayekataa ripoti ambayo haikusikiliza watu, ameruhusu magazeti anayoyaongoza yachapishe ripoti ambayo upande wa pili haukusikilizwa. Hii ni double standard. Kama tunataka kuongoza Taifa hili, ni vizuri tukafanya kazi bila kuonea watu.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru na nime-note ulichoongea. Nasisitiza kwamba nchi inaendeshwa kwa misingi ya haki. Hatuwezi kuwa upande huu, jambo tunalikubali tunalifuata, upande huu...

TAARIFA...

MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Spika, nimeipokea taarifa hiyo na kwamba gazeti kwa mujibu wa mhariri alifuata kuchapisha kwa sababu Rais aliagiza majina yale yachapishwe kwenye magazeti. Kwa hiyo, asingeonekana mzalendo kama angekataa kufanya kazi hiyo, naye amekuwa mzalendo amechapa, lakini haituzuii sisi kukosoa utaratibu uliotumika. Nami sio Mhariri wa hilo gazeti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna suala la Mkataba wa TBC na Kampuni ya Kichina. Jambo hili limezungumzwa hapa Bungeni mara kadhaa, tumeliandika kwenye vyombo vya habari kwamba mkataba kati ya TBC na Kampuni ya Kichina ni wa kinyonyaji. Mheshimiwa Waziri wa habari aliyetangulia kabla ya Mheshimiwa Dkt. Mwakyembe, aliahidi mbele ya Bunge hili kwenye mkutano uliopita kwamba ripoti ile itakuwa hadharani na Serikali itaiangalia upya suala zima la mkataba wa TBC na Kampuni ile ya Kichina. Nataka Mheshimiwa Waziri wakati anajibu atueleze mkataba kati ya TBC na Kampuni ya Kichina umefikia wapi?

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.