Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha wa 2017/2018 - Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha wa 2017/2018 - Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye Wizara hii nyeti iliyopo mbele yetu. Kabla ya kuanza niwape pole sana Watanzania wenzangu wa Jiji la Arusha na Watanzania wote kwa ujumla kwa msiba huu mkubwa. Wananchi wa Mikumi tupo pamoja nanyi na tunaendelea kuwaombea marehemu walale mahali pema peponi. Amina.

Mheshimiwa Spika, kabla sijaanza kuchangia na- declare interest mimi ni Mwanamuziki, ni mwanamuziki bora kabisa wa hip hop Afrika Mashariki na kati na kusini mwa Jangwa la Sahara, kwa hiyo hii Wizara inanihusu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, historia ya nchi yetu inaonesha tangu waasisi wa nchi hii walipokuwa wakifanya harakati kadha wa kadha walikuwa wakitumia sana sanaa. Nakumbuka Mwalimu Nyerere alikuwa akatumia wasanii mbalimbali akina Mzee Mwinamila, akina Mzee Moris Nyunyisa ambao mpaka leo midundo yao inatumika kwenye taarifa za habari huko TBC wakati anafanya harakati za ku-promote vijiji vya ujamaa.

Mheshimiwa Spika, lakini pia akina Mzee Mkapa walikuwa wakitumia sana wanamuziki wa mashairi kama akina Mzee Tambalizeni na watu wengine kama hao. Inaonesha ni jinsi gani ambavyo sanaa ni kitu muhimu na ni nyenzo muhimu sana katika Taifa kuonesha utamaduni, kuonesha mila lakini pia kufikisha ujumbe kadha wa kadha. Tunajua kwamba sanaa inatumia sana mafundisho lakini pia inakanya, inaonya na inasifia inapobidi; lakini kwa sasa kwa siku za usoni imeonekana wasanii kadha wa kadha wameonekana kuwa wakibanwa kutoa yale mawazo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wengi wamependa kuwa wakisifiwa tu na wasanii wanapotoa mawazo mbadala wamekuwa wakipata rabsha kama ilivyotokea kwa msanii Roma ambaye ametekwa na akaja kuachiwa katika mazingira ya kutatanisha, lakini pia Msanii Ney wa Mitego ambaye alishikwa na baadaye akaja kutolewa kwa msamaha wa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii inawapa hofu sana wasanii kuweza kutoa kile walichokuwa wanakifikiria kwa sababu tunaamini msanii yupo huru na anatakiwa kutoa mawazo huru katika kulisaidia Taifa letu. Hata sisi tulipokuwa tukifanya muziki tulikuwa tunaimba nyimbo kama ‘Ndiyo Mzee”, “Siyo Mzee” na vitu vingine wengi mnavijua, Mheshimiwa Waziri ulisema wewe ni shabiki wangu mkubwa, kwa hiyo, tunaamini kabisa kwamba mlikuwa mnajua jinsi ambavyo tumetumia sanaa hii kufundisha, kukanya, kuonya na kuburudisha pia.

Mheshimiwa Spika, wasanii wa Tanzania wamekuwa kwenye mazingira magumu sana na wamekuwa kwenye umasikini mkubwa. Mara nyingi tumekuwa tukiwatumia wasanii katika kampeni mbalimbali; tumekuwa tukiwatumia katika kampeni za malaria na hata katika chaguzi zilizopita
mmeona jinsi wasanii walivyokuwa wakitumika na baadaye mmewatumia kama Makarai na kuyaweka uvunguni.

Mheshimiwa Spika, tunajua Makarai yanatumika kwenye kujenga maghorofa na vitu vingine kama hivyo lakini tayari nyumba ikishakamilika yanawekwa uvunguni hayatakiwi hata kuonekana kwa wageni. Wasanii wa Tanzania wamekuwa wakitumika kwa style hiyo na wengi wamekuwa wakiwa maskini sana na hali yao ya uchumi imekuwa ngumu kwa sababu wamekuwa hawathaminiwi tena. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimesimama hapa nikipiga kelele na kupaza sauti ya wasanii kwa sababu nataka niwaambie, katika nchi zilizoendelea kama Marekani, Uingereza Taifa lao linapata mapato makubwa sana kupitia sanaa zao. Takwimu iliyofanywa hapa Tanzania na Rulu Art Promoters inaonesha kwamba muziki peke yake unachangia takribani asilimia moja na zaidi ya pato la Taifa la Tanzania. Kwa hiyo, tunaona kabisa muziki umekuwa katika hali mbaya lakini bado inachangia asilimia moja. Naamini Wizara ikitumia umakini na ikijaribu kuwekeza zaidi katika Wizara hii, wasanii wa Tanzania wataweza kuchangia pato kubwa sana katika Taifa. Pia imesaidia sana kwenye kutoa ajira, wasanii wamejiajiri na kuajiri vijana wengi zaidi katika sekta hii ya sanaa.

Mheshimiwa Spika, bajeti ya mwaka 2016/2017, Serikali ilitenga pesa kidogo sana ambayo ni bilioni tatu tu na katika hali ya kustaajabisha ni bilioni 1.19 ambayo ilikwenda kwenye nyanja hii na sasa hivi tunaweza tukaona katika bajeti hii imetengwa pesa ndogo ambayo kiukweli kabisa tunaona kama utani shilingi bilioni sita kwa sekta nzima ya Habari, Utamaduni na Michezo.

Mheshimiwa Spika, naamini kabisa kama kweli tuko makini kwenye kusaidia sanaa ya Tanzania ambayo imekuwa ikitoa ajira kubwa sana kwa wasanii na vijana wa Kitanzania, ilitakiwa tuweke pesa nyingi na hiyo pesa iweze kufika kwenye maeneo yanayohusika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni kumekuwa na malalamiko sana ya wasanii mfano wa filamu. Wasanii wa filamu wameandamana juzi wakiwa wanapaza sauti zao wakiwa wanataka haki zao za msingi. Hata hivyo niwaulize tu wasanii wenzangu wa filamu, huyu Bashite ameonekana kuwa na matatizo mengi na vyombo vya habari, amekuwa na matatizo mengi na Watanzania wengi wameonekana ambao wameonekana kuwa wanampinga, inawezaje mkamuweka akawa front line katika kutetea haki zenu za msingi? Tunaamini movement yoyote ambayo inatakiwa ifanyike kwenye kutetea haki inahitaji muungano wa watu wengi.

Mheshimiwa Spika, iwapo mngetaka kufanikiwa kwenye hili jambo mngemtumia kama Waziri wa habari kama alivyofanya press conference yake na Roma, tuliona vyombo vyote vikionesha mshikamano na umoja wao lakini sasa hivi tumeona mnamtumia Bashite ambaye anataka kujiosha kupitia ninyi na matokeo yake sasa Watanzania hawajawaelewa na ninyi wenyewe mmemeguka kwa sababu amekuwa na matatizo mengi na watu tofauti tofauti.

Mheshimiwa Spika, tunafahamu, sanaa ya filamu ya Tanzana inatoa ajira na sisi tuko hapa kwa ajili ya kuitetea na tunajua kwamba mna shida nyingi. Kwa mfano mdogo tu; kabla ya kufanya filamu, inabidi utoe shilimgi 500,000 kwenye Bodi ya Filamu kwa sababu tu ya kupeleka script yako, lakini ukishatoa script yako inabidi utoe tena shilingi 300,000= kwa ajili ya kupewa kibali cha ku-shoot. Ukishamaliza kutoa shilingi 300,000 na ukisha-shoot unapeleka shilingi 1,000 kukagua kila dakika ambayo unakuwa umeifanyia ile filamu. Ukitoa hiyo unakuja kupeleka tena unafunguliwa file pale COSOTA, unalipa zaidi ya shilingi 40,000. Baada ya hapo unapeleka TRA wanakupa sticker ambayo ni shilingi nane ndani, shilingi nane nje, jumla shilingi 16 kwa kila copy. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukimaliza hapo unaenda tena ku- negotiate na yule distributor ambaye ni Mhindi na ukishakubaliana naye kwa bei ambayo mliyokubaliana, anakata asilimia 30 kwa ajili ya kupeleka kwenye kodi ya Tanzania. Unaweza ukaona jinsi ambavyo wasanii wa filamu wanaumia. Hata hivyo strategy waliyoitumia kwenye kutetea haki zao, wametumia mlango mwingine wa kutokea badala ya kutafuta strategy ambayo wangepata support yote. Kwa hiyo, nimwombe Waziri huu ni muda sasa wa kukaa chini na wasanii kuunganisha nguvu zote, tunahitaji Waziri wa Mambo ya Ndani, tunahitaji COSOTA, tunahitaji BASATA na Waziri wa Habari na Michezo tuweze kukaa chini na wasanii tuweze kujua shida zao ambazo zinawasumbua.

Mheshimiwa Spika, kuhusu tatizo la hati miliki; katika hii Sheria ya Hati Miliki namba Saba ya mwaka 1999 imepitwa sana na wakati. Wasanii wanaibiwa sana kazi zao, piracy imekuwa kubwa lakini wezi wanaokamatwa na kazi hizo hamna adhabu kali ambayo wanapata. Tumeona kwamba kuna mtu alikamatwa na container zaidi ya bilioni sita zilikuwa zimetumika lakini baadaye anakuja kupigwa fine ya milioni tano. Mnaweza mkaona kwamba huu ni mzaha na inakatisha sana tamaa ya wasanii wa Tanzania katika hali kama hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, juzi msanii Diamond alikuwa analalamika, TRA wamempelekea kodi ya milioni mia nne. Unaweza ukajiuliza kwamba adaiwa milioni mia nne kwa kiasi gani alichoingiza? Downloads ambazo inafanyika, mnaweza mkaona kwamba sasa hivi wasanii wanabawanwa, TRA wanatamani kuvuna kutoka kwa wasanii kitu ambacho bado hawajakipandikiza. Tumekuwa na ule msemo kama wa zamani kwamba shamba likiwa na bangi ni lako lakini likiwa na dhahabu ni la Serikali. Tunataka kuchuma kitu ambacho hatujakipanda. Ndiyo maana nasema, inabidi Serikali sasa ianze kuweka na kuwekeza kutoka kwenye shule za msingi mpaka Chuo Kikuu tuanze kuwajenga wasanii.

Mheshimiwa Spika, hata juzi, msanii Darasa alienda Arusha, TRA wakavamia show yake, wakasema kwamba haya mapato inabidi tugawane asilimia 18 yaani wameibuka tu from nowhere. Darasa ameenda Arusha kwa gharama zake, ameenda kufanya matangazo, amelipa Ukumbi, wameenda wamefunga mageti saa 12 wanamwambia lazima tukate asilimia 18 pale Arusha, matokeo yake wamekuja kufungua mageti saa sita usiku, kijana wa watu aliyejiajiri kupitia muziki amepata hasara, amepata watu 200, 300 TRA wakakata hela zao.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo TRA kama mnataka pesa kaeni chini na wasanii tutengeneze strategy nzuri itakayosaidia wasanii wa Tanzania wanapowekeza kupitia kitu kama hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.