Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. George Boniface Simbachawene

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibakwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nianze kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Afya na Naibu wake kwa bajeti nzuri ambayo kwa kiasi kikubwa imejikita kutatua matatizo ya afya kwa Watanzania. Pia niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa michango yao mizuri tumeisikia na kwa kuwa tuna shida ya muda pengine si rahisi sana kujibu kila hoja na hivyo nitajikita kwenye maeneo manne ambayo yamezungumzwa sana na Waheshimiwa Wabunge wengi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la kwanza lilikuwa ni mpango gani upo kwa ajili ya kumalizia maboma ya vituo vya afya na zahanati katika maeneo yetu. Napenda tu nichukue nafasi hii kuwakumbusha Waheshimiwa Wabunge, kwa kuwa ni wawakilishi lakini pia wanaishi katika maeneo hayo, kwamba vyanzo vikuu vya mapato kwa ajili ya maendeleo ya wananchi wetu na hasa katika sekta zote ikiwemo sekta ya afya kwenye mamlaka zetu za Serikali za Mitaa ni hivi vifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kwanza kabisa ni nguvu kazi, nguvu ya wananchi. Lazima tutambue kwamba wananchi hawa nguvu yao ni rasilimali ya Taifa, kwa hiyo lazima itumike katika kutatua matatizo yanayogusa maisha yao. Tukumbuke tu kwamba nchi yetu ni nchi inayofuata misingi ya Siasa ya Ujamaa na Kujitegemea na ndivyo Katiba yetu inavyosema. Bado tunaamini kwamba kwa nchi masikini kama yetu tunapaswa kutumia nguvu za wananchi wetu katika kutatua kero za wananchi na kujiletea maendeleo. Vile vile tabia hiyo inajenga umoja lakini pia inajenga ownership kwa wananchi juu ya miradi inayowahusu ya huduma za jamii kwao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini chanzo kingine cha pili ni vyanzo vya ndani vya mapato ya Mamlaka za Serikali za Mitaa ambavyo, nilipowasilisha bajeti ya TAMISEMI, nilisema, asilimia 40 ya fedha za ndani zitakwenda kwenye maendeleo na maendeleo yenyewe ni pamoja na kuchangia ujenzi wa miundombinu kwa ajili ya huduma za kijamii ikiwemo huduma za afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti eneo la tatu ni Mfuko wa Maendeleo (Local Government Development Grant) ambayo kwa miaka mitatu nyuma ilikuwa haitoki lakini bajeti ya mwaka 2016/2017 tulitenga kiasi cha billioni 158 na hadi mwezi Desemba tumepeleka kiasi cha billioni 56 kwenye Halmashauri mbalimbali na wamezitumia katika kuhakikisha kwamba wanamalizia maboma yaliyojengwa ya kutolea huduma za afya pamoja na elimu. Zimetolewa fedha hizi na kwa hivyo ni mipango na vipaumbele tu vya halmashauri ndivyo vinavyotakiwa ili kuweza kutekeleza miradi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka wa fedha 2017/ 2018 tumetenga kiasi cha shilingi billioni 251.184. Fedha hizi zikigawanywa vizuri kwenye Halmashauri zetu na zikatumika kwa mujibu wa mwongozo tulioutoa wa asilimia karibu themanini kwenda kwenye miradi ya Maendeleo nina hakika zitaweza kupunguza matatizo ya umaliziaji wa maboma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo kubwa ni mamlaka ya Serikali za Mitaa kuweka Mipango yake kwa kutambua vyanzo hivi; ndiyo itatupeleka kumaliza matatizo haya ya upungufu wa miundombinu ya utoaji wa huduma za afya. Wananchi watakaojitoa na kujituma Serikali itapeleka fedha za kutosha kupitia mfuko huu ili waweze kumalizia kuezeka na kufanya finishing ili huduma ziweze kutolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili, ni utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi kama ilivyoelezwa juu ya kuwepo kwa zahanati katika kila kijiji na kituo cha afya katika kila kata. Tunazo kata karibu 4,200 kwa nchi nzima na tathmini tulizozifanya kwa ramani iliyotolewa na Wizara ya Afya ni takribani shilingi billioni 2.4 zinahitajika katika kukamilisha kituo kimoja cha afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo, pamoja na mipango mingine ambayo Serikali inayo lakini ni jukumu la Mamlaka za Serikali za Mitaa, kwanza kuweka kwenye mipango yao lakini pia kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa vituo hivyo ingawa tunayo mipango mingine ambayo tunaendelea nayo kwa kushirikiana na Wizara ya Afya kuhakikisha kwamba tunakwenda kidogo kidogo kwa vituo vichache vichache na hatimaye tuweze kumaliza kwa nchi nzima angalau kwa kila Halmashauri kuwa na kituo kimoja kipya ukiondoa vile vya zamani. Kwa kufanya hivi tutakuwa na vituo vingi sana kuliko vituo tulivyovijenga toka tulivyopata uhuru. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, rai yangu hapa kwa Waheshimiwa Wabunge ni kwamba, tujitahidi basi kuwahamasisha wananchi, kutenga yale maeneo kama tulivyosema na wale waliokwishatenga yale maeneo si kwamba tumewaacha, hapana, tunafahamu na tuko kwenye michakato mbalimbali wa kuhakikisha kwamba tunatafuta funds ili tuweze kuanza ujenzi wa vituo hivyo. Lakini mipango iwepo kwanza kwa wananchi wenyewe wa mamlaka husika na hicho kidogo kilichoko ikiwa ni ku-clear na kuanza hata kidogo kwa kutumia ramani iliyopo waanze halafu Serikali inakwenda ina-respond na ku-support pale ambapo wameanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine lililozungumzwa ni asilimia tano ya wanawake, zile ndizo tunazosemaga asilimia 10 kwa wanawake na vijana, lakini hapa nizungumzie tano ambayo ndiyo inayohusika na Sekta ya Wizara ya Afya. Kwa mwaka 2016/2017 hadi kufikia mwezi Desemba tumepeleka kiasi cha shilingi billioni 15.6 kwenye Halmashauri ikiwa ni kiasi cha asilimia hizo zilizotengwa kutokana na mapato ya ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti nilisema kwamba mapato ya ndani ni pamoja na OC inayotoka Hazina ukijumlisha na Own Source na makusanyo ya ndani ya Halmashauri, ukijumlisha ndipo unapata the total, ile total yake ndiyo unachukua asilimia 10 unapata ile inayotakiwa kupelekwa kwa wanawake na vijana. Kwa hivyo, naamini kabisa hadi sasa wanufaika 18,000 kwa nchi nzima 233 wakiwemo wanawake wamenufaika na fedha hizi billioni zaidi ya 15 zilizopelekwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, si jambo ambalo halifanyiki linafanyika, lakini nitoe rai kwa Mamlaka ya Serikali za Mitaa kuhakikisha kwamba wanapeleka kiwango hiki cha fedha kadri wanavyokusanya ili wasiwe na audit query kwa sababu jambo hili sasa Waheshimiwa Wabunge tunalisimamia kwa karibu. Niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa kusaidia kuzishauri Halmashauri lakini pia huko kwenye Halmashauri mliko ndiko zinakotolewa hizo fedha na ndiko zinakopatikana. Kwa hiyo, washauri wazuri na tuwaelekeze ili waweze kutekeleza agizo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti dhana ya ugatuaji wa madaraka katika sekta ya afya. Wakati mwingine kunazungumzwa kwamba kuna mkanganyiko. Niseme tu kwamba hakuna mkanganyiko wowote katika utoaji wa huduma ya afya kwa maana ya ugatuaji madaraka. Wizara ya Afya kazi yake ni kusimamia Sera ya Afya ya Taifa na katika kusimamia Sera ya Afya ya Taifa jukumu lake kubwa ni kuseti miongozo na standards ya utoaji wa huduma ya afya nchini; ambapo kwa kufanya hivyo tunazingatia viwango vya kimataifa, mahitaji ya kimataifa lakini pia na mahitaji ya ndani; wao ndio wanaosimamia sisi TAMISEMI ni watekelezaji wa maelekezo hayo. Kwa hiyo, wala hakuna mkanganyiko na Serikali ni moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ugatuaji huu duniani kote maeneo ambako utoaji wa huduma za afya na maendeleo ya watu yamekuwa realized imetokana na dhana ya upelekaji madaraka kwa umma. Unapopeleka madaraka kwa umma unawapa the ownership na kwa kusema hivi hata mara moja haiwi mkanganyiko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ifahamike kwamba unaposema TAMISEMI imepewa jukumu unamaanisha nini? Waheshimiwa Wabunge unaposema TAMISEMI imepelekewa jukumu hili, unamaanisha uwepo wa Mkuu wa Mkoa kama Mwenyekiti wa Kamati ya Maendeleo ya Mkoa akisimamia rasilimali zote zinazokwenda kwenye Mkoa wake. Unazungumzia na wataalam wote tuliowapeleka kwenye Mkoa, unazungumzia uwepo wa Mkuu wa Wilaya na watalaam alionao, lakini pia unazungumzia uwepo wa Mamlaka ya Serikali za Mitaa, Mkurugenzi na wataalam waliopo na Madiwani wanaosimamia kwa niaba ya wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hii ownership hii ndiyo iliyofanywa kwa nchi zilizoendelea kama Uchina, ndiyo inayofanywa na Japan. Sisi hatuwezi kuanzisha mfumo wa peke yetu, tukaanzisha jambo ambalo hatuwezi kuwa na ownership ya wananchi, maendeleo lazima yawe yanaguswa kwa ownership ya wananchi wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niseme tu TAMISEMI tuna uwezo wa kufanya kazi hii na tunapata support nzuri sana kutoka Wizara za Kisekta ikiwemo Wizara ya Afya katika Sekta ya Afya na tunakwenda vizuri na tunashirikiana vizuri sana, tuendelee na utaratibu huu utatusaidia kuivusha nchi yetu kwenye matatizo tuliyonayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga hoja mkono.