Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nimpongeze Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Wakurugenzi wote wa vitengo mbalimbali vya Wizara ya Afya. Pamoja na juhudi za Serikali za kuisaidia sana Hospitali ya Muhimbili, lakini bado kuna changamoto nyingi ikiwemo ya upungufu wa Wauguzi na Madaktari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuwepo na wagonjwa wengi katika Hospitali ya Muhimbili kunatokana na kutoimarika kwa Hospitali za Mikoa na Wilaya, kunasababisha Hospitali ya Muhimbili kuzidiwa na wingi wa wagonjwa. Naomba Serikali iangalie upya na kuzidi kuziimarisha hospitali zetu za Mkoa na Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kuongeza teknolojia ya kupunguza muda wa kupata mionzi. Sambamba na hilo, naomba Serikali wafanye tafiti mbalimbali kutafuta kila kinachosababisha ugonjwa na kuongezeka kwa haraka sana. Kansa inaua watu wengi sana. Kwa sasa inaonekana hakuna dawa kutokana na watu kukosa elimu ya kutosha kutokana na viashiria vya ugonjwa huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na ongezeko kubwa la wagonjwa MOI. Wagonjwa wa mifupa wamekuwa wengi wanakaa kwenye waiting list ya kusubiri operation kwa muda mrefu sana kutokana na kitengo hiki kuzidiwa na wagonjwa, lakini pia upungufu wa Madaktari. Pamoja na kwamba natambua kinachosababisha hayo ni wenye bodaboda, ndio walio wengi na wanasababisha ajali kuwa nyingi sana, majeruhi wamezidi MOI kutokana na ajali za barabarani: Je, Serikali inaisaidiaje MOI kudhibiti ongezeko la ajali za barabarani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali isaidie MOI kwa kuongeza kujengea uwezo Hospitali za Amana, Temeke na Mwananyamala. Serikali ikizijengea uwezo Hospitali hizo za Mkoa wa Dar es Salaam zinaweza kusaidia sana katika kuipunguzia MOI msongamano. Naomba pia hospitali hizo ziweke vitengo vya mazoezi ya viungo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza sana Kitengo cha Emergency cha Muhimbili. Kwa kweli wanafanya kazi nzuri sana kiasi cha kufanya wananchi wajenge imani ya kupona hapo. Kwa kweli wagonjwa walio wengi wanaokuja mahututi wanaamka hapo; kama kufa, wanaenda kufia kwenye wodi kama hawatapata huduma stahiki. Naomba vitengo vya emergency vya Hospitali ya Temeke, Amana na Mwananyamala nazo ziwe na vifaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na juhudi za Mkuu wa Mkoa kuamua kusaidia katika kujenga majengo ya huduma za dharura katika Hospitali za Temeke, Amana na Mwananyamala, lakini naomba Serikali iongeze nguvu kwa kuleta vifaa kwa hizo emergency Unit zilizopo, tupate angalau huduma kwa kipindi hiki cha mpito.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa uamuzi wake wa kujenga vyumba vya upasuaji kwa kila hospitali au zahanati kwa lengo la kuokoa afya ya mama na mtoto. Changamoto kubwa iliyopo Muhimbili imezidiwa na wingi na akinamama; wazazi ni wengi lakini watoa huduma ni wachache na hasa Wauguzi. Kwenye wodi moja unakuta wauguzi ni wawili. Naomba Serikali ituongezee Wauguzi na Madaktari katika Hospitali ya Temeke, Amana, Mwananyamala na Vituo vya Afya vilivyopo katika Mkoa wa Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Dar es Salaam ina ongezeko kubwa la wageni wanaokuja takriban mabasi 300 yanaingia kila siku kutoka mikoani. Hivyo tunahitaji ongezeko la bajeti katika huduma za afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, magonjwa ya akili yameongezeka sana, kwa mfano Hospitali ya Temeke imetoka kwenye wagonjwa watano hadi saba mpaka wagonjwa 105 mpaka 120, lakini hakuna wodi za wagonjwa wa akili katika Hospitali za Mikoa ili kupunguza msongamano wa wagonjwa wa akili Muhimbili. Naomba Madaktari wapewe posho Maalum ya Mazingira Hatarishi ya maisha yao kwani wagonjwa wanaowahudumia ni wa hatari sana. Sambamba na Madaktari na Wauguzi wa Wagonjwa wa Akili, Serikali ifanye utafiti, ni tatizo gani linafanya ongezeko la maradhi ya akili kuongezeka kwa kasi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ugonjwa wa watoto kudondoka ni tatizo kubwa sana. Walianza wanafunzi wa Shule za Msingi na Sekondari na sasa wanaanguka hata watoto wadogo ambao hawajaanza shule. Naiomba Serikali iangalie kwa kina, ni nini kimekosekana au ni madini gani yamekosekana mpaka watoto wanaanguka ovyo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Vituo vya Madawa ya Kulevya vimezidiwa sana. Kulingana na juhudi za Serikali kupiga vita madawa ya kulevya, ambazo naunga mkono, ongezeko la wagonjwa hao ni kubwa sana na huduma inahitajika sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali iongeze vituo vya Methadone katika Hospitali ya Kigamboni kuwasaidia vijana kuepukana na tatizo la nauli ya kufika Temeke. Pia Kituo cha Muhimbili, Mbagala na Chamazi kinachohudumia wagonjwa wa akili, naomba kiwekwe kituo cha Methadone kusaidia vijana wa Mbagala, Chamazi,

Tuangoma, Kijichi na Mbagala Kuu wapate huduma hiyo kwa urahisi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza sana Serikali kwa kutengea hii Hospitali ya Chanika ambayo itatusaidia sana katika kupunguza idadi ya wagonjwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Muhimbili, wodi ya wazazi mpya, kwa sisi Dar es Salaam tunaita Jengo la Rais Magufuli. Nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kuwasaidia akinamama wajawazito. Kwa kweli jengo lile ni mkombozi wa wanawake. Limesaidia sana kiasi cha kujiuliza, wale akinamama kama kungekuwa hakuna jengo lile tungewaweka wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, akinamama wanaruhusiwa saa 8.00 mchana lakini wanatoka hospitali saa 2.00 usiku kusubiri bili za kawaida na Bima ya Afya. Kitengo cha accounts kiongezewe nguvu, kero hii ni kubwa. Usiku una mambo mengi, wazazi wanaweza kuibiana watoto ikawa tatizo kwa hospitali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, asilimia mia kwa mia.