Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Jerome Dismas Bwanausi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lulindi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. JEROME D. BWANAUSI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kukushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu. Nianze tu kwa kumpongeza sana Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa anayoifanya.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nianze kwenye sekta ya kilimo ambayo kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu imo kuanzia ukurasa wa 26 hadi 32. Nijikite kwenye zao la korosho. Kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu wetu, ndugu yangu Majaliwa Kassim, kwa kazi kubwa sana aliyoifanya wakati alipofanya ziara kule Ruangwa na kutoa tamko la Serikali la kuondoa tozo tano ambazo zilikuwa ni kero za wananchi, tunashukuru sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie tatizo la korosho ambalo ni zao la pili kwa kuiingizia pato Serikali yetu, ukiacha tumbaku ambayo ni ya kwanza. Lakini hali ya wakulima wetu Mheshimiwa Waziri Mkuu anajua, hali za wakulima wetu ni hali mbaya sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi kuna sakata linaloendelea katika Wilaya ya Masasi ambalo wakulima hawajalipwa fedha zao kati ya shilingi 200 hadi shilingi 400 kwa kila kilo, lakini hadi sasa kuna wingu ambalo halieleweki wakulima wale watalipwa lini?
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili linawafanya wakulima wetu wawe katika mazingira magumu sana. Wanahangaika, wanapalilia, wanapulizia, wanakwenda kuokota korosho zao, wanapeleka kwenye Vyama vya Msingi, vinakwenda kwenye Vyama Vikuu na hadi pale kupata soko, lakini baadhi ya wachache wakiwemo baadhi ya Maafisa Ushirika ambao siyo waaminifu wanashirikiana na baadhi ya Viongozi wa Bodi za Wakulima wa Vyama vya Msingi kuwaibia wakulima.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakulima wa Wilaya ya Masasi safari hii tumesema tunahitaji fedha walipwe wakulima, nani amechukua, ameziweka wapi, hiyo siyo hoja yetu! Ninamshukuru sana Waziri wa Kilimo, Mheshimiwa Mwigulu baada ya mazungumzo naye amekubali kufanya ziara kwenda Masasi kujionea hali halisi na ninaamini kabisa kwa utendaji wake mzuri ataweza kuwaridhisha wakulima wale na kuwapa matarajio na mategemeo makubwa jinsi ambavyo Serikali inajitahidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ili kuwasaidia wakulima wa korosho katika mikoa yote ambayo inalima korosho ni lazima kufanya reshuffle ya Maafisa wa Ushirika. Maafisa wa Ushirika waliokaa katika Mkoa wa Mtwara sasa wamekaa wengine zaidi ya miaka 10 wengine miaka 15, katika mazingira hayo wanatengeneza mtandao wa kutengeneza hata Bodi za Wakulima kule kwenye Vyama vya Msingi na kuhakikisha wanajipatia kipato kutokana na hali hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda Ofisi ya Waziri Mkuu ilifanyie kazi hili kwa nguvu zake zote ili kumfanya mkulima sasa ajengewe matumaini kwamba Serikali hii ya Awamu ya Tano ni Serikali inayowajali wanyonge. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu sekta ya afya. Nimesoma kitabu cha hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, amesisitiza sana jinsi ambavyo Serikali itajitahidi sana kuhakikisha kwamba inaboresha sekta ya afya, nimueleze tu Mheshimiwa Waziri Mkuu, sasa hivi ameelekeza kwenye ukurasa wa 55 kwamba tujitahidi sana tuhakikishe tunawahamasisha wananchi waweze kujiunga na Bima ya Afya. nimthibitishie tu Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba kazi hiyo zimeshaanza kufanywa na wananchi wamehamasika lakini nina mashaka juu ya jambo hilo, kukakatishwa tamaa wananchi kwa sababu wamekata Bima, lakini wanapokwenda kwenye zahanati zetu hakuna dawa! hivyo hawaoni umuhimu wa kuwa na Bima ya Afya kama hawapati dawa kwenye zahanati zetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Ofisi ya Waziri Mkuu ijikite kuhakikisha kwamba haya yote yanakwenda sambamba, tunahamasisha suala la Bima ya Afya, lakini tunaongeza dawa kwenye zahanati zetu na watendaji wetu ili wananchi wawe na uhakika kwamba wakienda zahanati wanapata dawa.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nilitaka niliseme ni juu ya suala la barabara. Mheshimiwa Waziri Mkuu umeelezea juu ya jitihada ya Serikali jinsi ambavyo itaimarisha sekta ya barabara lakini nataka tu nikuhakikishie Mheshimiwa kwamba wananchi wanaimani kubwa na Serikali ya Awamu ya Tano sana, haya yote mnayoyasema na mnayotuambia tunakubali kwamba awamu hii mambo mengi yatatekelezwa, lakini nasisitiza suala la barabara kutoka Mtwara - Newala - Tandahimba hadi Masasi ambayo ni barabara ya uchumi. Napenda Mheshimiwa Waziri Mkuu na Waziri wa Ujenzi atekeleze agizo la Mheshimiwa Rais alilolisema ataweka wakandarasi wanne ili kuhakikisha barabara hiyo inamalizika kwa haraka ili kutatua tatizo lililoko pale. (Makofi)
Mheshimiwa Waziri Mkuu katika maelezo hayo ambayo umetupa matumaini lakini kuna suala la barabara ya kutoka Masasi kwenda Nachingwea ambayo inaunganisha hadi Ruangwa hadi Nanganga kwenye Jimbo la Mheshimiwa Waziri Mkuu. Barabara hii tumeisemea muda mrefu, kwa kweli kuna kila sababu barabara hii ijengwe. Ni barabara muhimu inaunganisha mikoa miwili, ni barabara ya uchumi na kwa hakika wewe mwenyewe huwezi kujisemea, sisi lazima tuseme kwamba barabara hii sasa tunataka ijengwe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka nijikite katika eneo hilo lakini pia nimalizie kwenye sekta ya elimu. Mimi niseme tu kwamba Mheshimiwa Waziri Mkuu wetu bahati nzuri alikuwa mwalimu. Naamini kilio cha walimu sasa kitapewa kipaumbele. Kilio kile ambacho kwa kweli muda mrefu wao wamekuwa wakilalamikia kuhusu marupurupu yao, kuhusu nyumba, kuhusu stahili zao nyingine, hatutegemei Serikali ya Awamu ya Tano walimu wawe ni sehemu ya manung’uniko kama ilivyokuwa miaka mingine.
Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri Mkuu hili lipewe kipaumbele ili Walimu waweze kupewa umuhimu katika jamii na ndiyo sekta ambayo inaajira pekee kuliko sekta nyingine na Walimu ni wengi naamini kabisa Serikali hii na Walimu wameshaanza kuwa na imani, tuendelee kuwapa imani zaidi ili wafanye kazi yao vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hotuba ya Waziri Mkuu.