Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Jumaa Hamidu Aweso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Pangani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. JUMAA H. AWESO: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru kwanza kwa kunipa nafasi hii adhimu na mimi nichangie hotuba ya Waziri Mkuu iliyopo mbele yetu. Pia naomba niipongeze Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi kubwa inayoifanya. Lakini pia nimpongeze Dkt. John Pombe Magufuli ni jembe, tena ni jembe la palizi ambalo limekuja kwa ajili ya kuwasaidia Watanzania. Pia nimpongeze pia Waziri Mkuu kwa kazi kubwa anayoifanya, najua zipo changamoto nyingi lakini nasema bahari kubwa ndiyo ivukwayo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchangia katika suala zima la uwezeshaji wa wananchi kiuchumi. Pamoja na mafanikio ya kukuza uchumi katika Taifa letu, pia kuna changamoto kubwa ya umaskini wa watu wetu, ninaiomba Serikali ihakikishe kwamba inatengeneza mazingira ya uwezeshaji wananchi kiuchumi ili kuhakikisha kwamba inawasaidia katika kuepukana na umaskini uliokithiri katika jamii yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali yetu imeahidi katika Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi kutenga shilingi milioni 50 katika kila kijiji, hii itakuwa ni solution ya kuwasaidia Watanzania kwa sababu wapo mama lishe, wapo wajasiriamali wadogo wadogo wakiwemo bodaboda, kilio chao kikubwa ni mitaji, leo ukitaka mtaji unawaambiwa upeleke hati ya nyumba, kiwanja huna hiyo hati utaitoa wapi! Naamini kupitia Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya shilingi milioni 50 katika kila kijiji itasaidia sana Watanzania na wananchi wa Pangani.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ningependa nilizungumzie ni suala zima la kilimo. Watanzania wanategemea sekta ya kilimo, lakini kilimo kilichopo sasa, ukuaji wake ni wa kusuasua na kutegemea kudra za Mwenyezi Mungu. Ninaiomba Wizara ya Kilimo ihakikishe kwamba inajikita katika sekta ya kilimo cha umwagiliaji kwa sababu nchi yetu Mwenyezi Mungu ameijaalia, kuna mito na maziwa mengi tukijikita katika kilimo cha umwagiliaji nadhani suala la chakula kwetu litaisha kabisa.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mji wetu wa Pangani tumejaaliwa kuwa na Mto wa Pangani ambao unamwaga maji baharini, ninamwomba kaka yangu Mheshimiwa Mwigulu Nchemba ahakikishe kwamba anatutengenezea scheme ya umwagiliaji ili kuhakikisha kwamba jamii yetu ya Pangani tunajikita katika kilimo cha umwagiliaji ambacho kitakuwa katika mazao ya mbogamboga ambayo itaweza kulisha Wilaya ya Pangani na Mkoa wa Tanga pia tunachangia Pato la Taifa katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo ninapenda kulizungumzia ni suala zima la miundombinu ya barabara. Ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya barabara ni kichocheo cha maendeleo katika jamii yoyote. Lakini katika Wilaya yetu ya Pangani, barabara yetu imekuwa ni ahadi ya muda mrefu lakini mpaka sasa barabara hii imeweza kuzorotesha maendeleo katika jamii yetu ya Pangani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaiomba Serikali ya Awamu ya Tano iangalie kwa jicho la huruma kuhakikisha kwamba inajenga barabara hii ya Pangani, Tanga - Pangani - Sadani ili kuweza kuinua uchumi wa Pangani.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia Wilaya ya Pangani ilivyo ni kama kisiwa, ili uende Pangani lazima uende kwa makusudio maalum, unaenda kuzika au umesikia kuna kitchen party ndiyo watu waweze kwenda, madhara ya barabara hii ni makubwa, ingawa tumekuwa na fursa nyingi ya kiutalii, tuna uvuvi bahari kuanzia mwanzo wa mji mpaka mwisho wa mji. Ninaiomba Serikali itengeneze barabara hii ya Pangani ili kuhakikisha kwamba uchumi wa Pangani unapaa, badala ya kuwa pangoni, sasa tupae angani. Ninaamini Serikali hii kwa kazi inayofanya barabara hii itatengenezewa kwa wakati.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo nataka nilizungumzie ni sekta ya uvuvi. Jamii yetu ya Pangani tunategemea sekta ya uvuvi, Lakini uvuvi tunaoufanya ni wa kutumia zana duni na ukitaka kwenda kuvua lazima utegemee ndoano na chambo; hivi samaki akishiba huyo samaki utamvua wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Wizara ya Uvuvi iangalie sasa suala la uvuvi ili kuhakikisha kwamba inawasaidia wavuvi wa Pangani kwa kuwapatia pembejeo na zana na kuhakikisha tunatengenezewa bandari ya uvuvi kwa ukanda wa Pangani na Tanga ili kuhakikisha kwamba wavuvi wa Pangani wanafaidika ni rasilimali bahari tuliyonayo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo napenda nizungumzie ni suala la afya. Huduma ya afya bora ni njia nzuri ya kuinua uchumi katika jamii yoyote, lakini katika sera ya Serikali inasema kwamba itajenga zahanati katika kila kijiji na kituo cha afya katika kila Kata, lakini Pangani tuna kituo kimoja tu cha afya na asilimia kubwa ya wananchi wanakaa ng’ambo ya Mto Pangani ambapo hutegemea huduma katika hospitali yetu ya Wilaya ya Pangani. Hospitali ya Wilaya ya Pangani bado haijajitosheleza, ukitazama x-ray hakuna, bado dawa ni shida, leo ukitaka x-ray mpaka uende Tanga.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaiomba Serikali ya Awamu hii ya Tano katika bajeti yake ihakikishe kwamba inashirikiana na sisi kuhakikisha tunatengeneza vituo vya afya vya ziada ili kuisaidia jamii yetu ya Pangani katika suala zima la afya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo ningependa kusema kwamba wapo watu ambao wanajigeuza bundi kukitakia Chama cha Mapinduzi mabaya kife, lakini nasema watakufa wao na ofisi zao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kazi iliyofanya Chama cha Mapinduzi ni kubwa, ukiangalia katika Wilaya yetu ya Pangani mpaka mwaka 2005 tulikuwa na shule mbili tu za Serikali, lakini sasa hivi tuna shule saba hata mimi mtoto wa mama ntilie nimefika Chuo Kikuu, dogo hilo? Mungu atupe nini, hata Mwenyezi Mungu anasema katika vitabu vya dini waamma biniimati rabbika fahadith (zielezeeni neema za Mwenyezi Mungu kwa kushukuru). Sasa leo usiposhukuru kidogo unataka ukashukuru wapi?
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imefanya kubwa lakini ninachokiomba iendelee kutengeneza miundombinu ya elimu, vilevile kuboresha maslahi ya elimu kwa watumishi ili kuhakikisha wanafaidika na kazi wanazozifanya.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo sina maneno mengi ya kusema, naunga mkono hoja asilimia mia moja.