Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha mchango wangu kwa sekta ya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kuanzia kwa Mheshimiwa Rais, Waziri na Naibu wake na watendaji wote.

Kwanza, kuongeza bajeti ya Wizara kwa zaidi ya mara kumi; kuendelea kutoa vifaa tiba vya hospitali na vituo vyake yaani vitanda, magodoro na kadhalika; kutoa ajira ya madaktari wawili katika hospitali ya Wilaya ya Mbulu na kwingineko katika Wilaya za nchi yetu na kugawa pikipiki katika Halmashauri zetu nchini, naomba katika mgao ujao Halmashauri za Wilaya ya Mbulu wapewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali iboreshe mfumo wa utoaji na upokeaji wa dawa katika hospitali za Wilaya vituo na zahanati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wajumbe wa Bodi ya Afya ya Wilaya na Bodi ya Vituo vya Afya na Kamati ya Afya ya Zahanati wapatiwe semina ya majukumu yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali iondoe mpango wa kila Halmashauri za Wilaya kukamilisha kituo kimojawapo katika vituo vilivyoko kwa mwaka ili kuweka nguvu mahali pamoja hali itakayosaidia kuwa na vituo vitano kwa miaka mitano. Hivi sasa fedha za bajeti hugawanywa na Madiwani kiasi kwamba hakuna mafanikio.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali ijitahidi kulipa madeni ya watoa huduma wa zabuni za chakula katika Halmashauri ya Mbulu, ni zaidi ya miaka saba sasa madeni hayo hayajalipwa. Japokuwa Serikali imesitisha watoa huduma ya chakula kwa wanafunzi wa chuo na huduma ya wagonjwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Wilaya ya Mbulu ni taasisi kongwe kwa umri wake, kwa hiyo ninaomba Serikali yetu ione utaratibu wa kukarabati majengo ya hospitali hiyo. Naomba Serikali itusaidie kupata gari la ambulance kwani kwa sasa gari lililopo ni chakavu sana na wagonjwa wa rufaa ya kwenda Haydom ni kilometa 100, rufaa ya kwenda hospitali ya KCMC ni kilometa 360. Hivyo, naomba Serikali ituonee huruma kwa kutupa gari kwa ajili ya maisha ya watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwezi Februari 2017 nilifanya kikao cha watumishi wa afya hususani wale walioko katika Hospitali ya Wilaya, katika kikao hicho watumishi walitoa kilio cha kukosa kwa muda mrefu fedha zao za on call allowance(malipo ya posho ya masaa ya ziada), naomba Waziri wetu baada ya bajeti atoe kauli ili watumishi wawe na amani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado naendelea kusema kuna umuhimu mkubwa wa dawa za Serikali kuwekewa alama kwa ajili ya kupunguza uvujaji wa dawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali iwaajiri watumishi wa afya, bado tuna upungufu mkubwa sana wa watumishi wa afya katika Hospitali ya Wilaya, vituo na zahanati katika Halmashauri za Vijiji hali inayopelekea huduma za afya kuwa hafifu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itazame upya mfumo wa TFDA ili kupunguza uharibifu wa rasimali za umma kwa ajili ya afya ya mlaji. Mfano, simu fake, viroba na kadhalika, hali inayosababisha kudhoofisha uchumi wa jamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho katika Hospitali ya Wilaya ya Mbulu kuna chuo cha PHN. Tunaomba Mheshimiwa Waziri wetu wa Afya aweze kufanya ziara katika chuo hicho na hospitali hiyo. Hata hivyo, kuna jengo lililokuwa linajengwa na Serikali Kuu, jengo hilo lililojengwa chini ya kiwango, hivyo chuo chetu kinafanya kazi katika mazingira magumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naomba kuunga mkono hoja kwa asilimia mia moja .